Bukobawadau

'MREMBO'MBARONI KWA DAWA ZA KULEVYA UWANJA WA NDEGE

Kikosi Kazi cha Kupambana na Dawa za Kulevya, Uwanja wa Ndege wa Dar es Salam (JNIA) jana kilimkamata mwanamke mmoja, Salama Omari Muzara akiwa amemeza kete za dawa za kulevya aina ya Heroin ambazo idadi yake kamili haijajulikana.
Kamishna wa Polisi Kitengo cha Kupambana na Dawa za Kulevya, Godfrey Nzowa alisema, msichana huyo alikamatwa jana saa saba mchana akiwa njiani kuelekea Macao, China na Shirika la Ndege la Ethiopia.
“Alikuwa anasafiri kwenda Macao, China kwa ndege ya Ethiopian Airlines ambayo ilikuwa iondoke saa 10 jioni ndipo kikosi kazi cha polisi uwanja wa ndege kikamshuku kuwa amebeba kitu kisicho cha kawaida” alisema Nzowa.
Nzowa alisema, mwanamke huyo alikuwa na hati ya kusafiria namba AB548242 ambayo ilitolewa Oktoba mwaka jana na haikufahamika idadi kamili ya pipi alizomeza kwani mpaka sasa bado anazitoa. Nzowa alisema mpaka sasa mwanamke huyo tayari ameshatoa pipi kadhaa tangu alipokamatwa jana mchana ambapo kuanzia asubuhi leo hadi saa saba mchana huu ameshatoa pipi 27.
Kamishna Nzowa alisema hiyo ni sehemu tu ya mapambano ya dawa za kulevya nchini ambayo imesaidia kupunguza kwa kiasi kikubwa wasafirishaji na watumiaji wa dawa hizo.
Hivi karibuni, Mwanamitindo wa Tanzania, Jackline Cliff alikamatwa na kete 66 za dawa za kulevya aina ya heroin zenye thamani ya dola za Marekani 137,720 huko Macao, China.
Mwanamitindo huyo , aliyekuwa akisafiri kutoka Thailand akielekea Macao aliwaambia polisi kuwa alikuwa anaelekea Guangzhou ambao ni mji wa jimbo la Guangdong huko China.
Kamanda Nzowa alisema kikosi chake kinaendelea kuwasiliana na Polisi wa Macao ili kujua iwapo ataweza kurejeshwa nchini ingawa alikiri suala hilo limekuwa gumu kwani China hawana utaratibu wa kubadilishana wafungwa.
Next Post Previous Post
Bukobawadau