Bukobawadau

MULEBA YAJIVUNIA ZIADA YA MADARASA

Na Edson Kamukara 
WAKATI wanafunzi wengi wakikwama kujiunga kidato cha kwanza mwaka huu kutokana na uhaba wa madarasa unaozikabiri baadhi ya halmashauri nchini, Wilaya ya Muleba, mkoani Kagera imetamba kuwa na madarasa ya ziada.

Mafanikio hayo yalibainishwa hivi karibuni na Ofisa Elimu Taaluma wa wilaya hiyo, Mlashani Rwenyagira alipohojiwa na gazeti hili ofisini kwake.

Alisema kuwa kwa sasa Wilaya ya Muleba inazo sekondari 35 za serikali na nane za binafsi ambazo kwa pamoja zina wanafunzi 15,143 kabla ya uteuzi wa kidato cha kwanza.

“Kwa mwaka huu, tulitarajia kupeleka sekondari asilimia 70 ya wanafunzi kati ya 9,872 waliofanya mtihani wa darasa la saba mwaka jana.

“Kwa idadi hiyo ni kwamba tunahitaji vyumba 179 vya madarasa lakini vilivyopo mpaka sasa ni 201, hivyo hatuna uhaba wa madarasa bali tuna ziada,” alisema.

Kwa mujibu wa Rwenyegira kati ya idadi hiyo, shule mbili ni za kidato cha tano na sita ambazo ni Kishoju na Rutabo.

Kuhusu mahitaji ya walimu, alisema wana uhaba kwa mchepuo wa sayansi kwani wengi wa wanaoletwa ni wale wanofundisha masomo ya sanaa.

Aliongeza kuwa licha ya kuwa na uhaba huo wa walimu wa sayansi, mchakato wa ujenzi wa maabara unaendelea na sasa zimejengwa katika shule 16 huku nyingine nne zikiwa kwenye ujenzi.

“Lakini pia ziko sekondari nne za Ibuga, Mayondwe, Kibanga na Kanyeranyere zinatumia maabara inayotembea (mobile Laboratory).

Pia Rwenyagira aligusia fedha za maendeleo ya shule akisema kuwa zinagawiwa kutegemeana na uwezo wa mfuko wa halmashauri na mahitaji ya shule husika.

Alifafanua kuwa kwa mwaka juzi, mgawo ulikuwa sh milioni 7 na kwa mwaka jana, shule 21 tayari zimepatiwa fedha hizo ambapo kila moja alipata sh milioni 8.8.

Kwa mujibu wa ofisa huyo, mwaka juzi bajeti ya elimu ya wilaya hiyo ilikuwa sh bilioni 1.4 lakini walipatiwa sh milioni 700 pekee ambayo iliunganishwa na ile wanayopewa na halmashauri kupitia vyanzo vyake.
Next Post Previous Post
Bukobawadau