Bukobawadau

LOWASSA,SUMAYE,NGELEJA WAJIELEZA KAMATI YA MANGULA

 Waziri Mkuu Mstaafu Ndugu Edward Lowasa akizungumza na Waziri Mkuu wa Zamani Ndugu Fredrick Sumaye kabla ya kuanza kuhojiwa na Kamati Ndogo ya Maadili kwenye Makao Makuu ya Chama Cha Mapinduzi Dodoma
 Ndugu William Ngeleja akisubiri kuhojiwa na Kamati Ndogo ya Maadili kwenye Makao Makuu ya Chama.
Dodoma.Waliowahi kuwa Mawaziri Wakuu; Edward Lowassa na Frederick Sumaye jana walifika mbele ya Kamati Ndogo ya Maadili ya CCM kutoa maelezo juu ya tuhuma za kufanya kampeni za urais kabla ya wakati

.

Mbali na wastaafu hao, mwingine ambaye jana alifika mbele ya kamati hiyo ambayo ilikuwa chini ya Makamu Mwenyekiti wa CCM Bara, Philip Mangula na Katibu Mkuu wa chama hicho, Abdulrahman Kinana ni Waziri wa Nishati wa zamani na Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja.

Mjumbe mwingine wa kamati hiyo aliyehudhuria kikao hicho kilichofanyika kwenye Ukumbi wa White House jana ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi. Wajumbe wengine ni Dk Maua Daftari, Shamsi Vuai Nahodha na Pindi Chana ambao hata hivyo, hawakuhudhuria.

Hata hivyo, wanachama wengine watatu, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe, Waziri wa Nchi (Ofisi ya Rais Uhusiano na Uratibu), Stephen Wassira na Naibu wa Sayansi na Teknolojia, January Makamba ambao wote wanatazamiwa kuitwa leo mbele ya kamati hiyo.

Vyanzo kutoka ndani ya chama hicho vilieleza kuwa Membe alikuwa katika ziara ya Rais Jakaya Kikwete na alitarajiwa kurejea nchini jana jioni.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kukamilika kwa mahojiano ya makada hao watatu jana, Kinana alisema shughuli ya kuwahoji wengine itaendelea leo.

"Kazi haijakwisha, kesho (leo) tunaendelea."

Waliyosema baada ya kuhojiwa

Akiwa amevalia mavazi rasmi ya CCM, Lowassa alihojiwa kwa takriban saa moja na nusu kwani aliingia katika kikao hicho saa 4:56 asubuhi na kutoka saa 6:40 mchana akiwa ametumia takriban saa moja na nusu na alitoka akiwa mwenye furaha.
Alipoulizwa kuhusu mahojiano hayo Lowassa: "Mazungumzo yalikwenda vizuri. Yalikuwa na lengo la kujenga chama kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015," alisema Lowassa huku akitabasamu.

Muda mfupi baada ya Lowassa kutoka, Sumaye aliingia kuanzia saa 6:46 na kutoka saa 8:05.
Baada ya kutoka, Sumaye pia hakuwa tayari kuzungumzia kuhusu mahojiano hayo... "Tunawasubiri wakubwa watakavyotoa jawabu." Alipoulizwa sababu za kutumia muda mwingi katika kikao hicho alisema: "Tulikuwa tunakunywa chai."

Kwa upande wake, Ngeleja ndiye aliyetumia muda mfupi zaidi kwani aliingia katika ukumbi wa mahojiano saa 8:10 na kutoka 8:50.

Aliwaambia waandishi wa habari waliokuwa nje ya ukumbi huo kuwa mazungumzo hayo yalikuwa ni ya kichama na kikazi zaidi na kwamba hizo ni taratibu za CCM kuwaita wanachama wake kwa ajili ya kutoa maelekezo.
Kuhusu kutangaza nia ya kugombea urais kabla ya muda uliopangwa na chama, Ngeleja alisema wanaongozwa na kanuni na taratibu na kwamba wakati wa kutangaza kugombea urais haujafika.

Alisema hakuitwa kuhojiwa kwa kutangaza nia ya kuwania urais kabla ya muda... "Sijatangaza, sijasema, sina ugomvi huo."
chanzo ;Mwananchi
Next Post Previous Post
Bukobawadau