Bukobawadau

TOFAUTI YA VIPATO NDIO MWANZO WA UHALIFU NCHINI

Na Prudence Karugendo
 Nitataja  rushwa ili kurahisisha maelewano,  lakini vinginevyo nilipaswa kutaja mabalaa yote yanayohusu mambo ya fedha yanayoikumba jamii yetu ya Tanzania. Ujambazi, ubadhilifu, udokozi, usaliti pamoja na rushwa yenyewe vyote hivyo vina sura ya aina moja.
Isidhaniwe kuwa nataka kuongelea mishahara midogo tu, la hasha. Nia yangu ni kuongelea juu ya tofauti kubwa ya mishahara iliyopo miongoni mwa wafanyakazi wa sekta mbalimbali za umma,  lakini zaidi katika vyombo mbalimbali vya serikali pamoja na serikali yenyewe.
Pamekuwepo tofauti kubwa ya mishahara  miongoni mwa wafanyakazi au watumishi wa sekta mbalimbali katika nchi yetu kiasi cha kutia kichefuchefu. Katika idara nyingine watu wanalipwa mishahara minono utadhani hawako katika nchi masikini kama Tanzania lakini katika idara nyingine mishahara inayotolewa haina tofauti na zawadi, kana kwamba mtu au asasi husika haina mchango wowote katika uendeshaji wa nchi. Kwa vyovyote hii ni miongoni mwa sababu za msingi zinazopelekea milipuko ya vitendo vya jinai kama vilivyotajwa hapo juu.
Angalia, asasi mbili tofauti, zote zinamilikiwa na serikali. Nyingine zinapangiwa viwango vya mishahara  na nyingine zinaruhusiwa kujipangia viwango vya mishahara ya wafanyakazi wake. Matokeo yake afisa mmoja mkubwa sana wa asasi moja analipwa mshahara  sawa na karani wa asasi nyingine. Mfikirie mfanyakazi wa kada ya chini wa asasi inayoendeshwa na afisa huyu mkuu.  Mwisho wa siku wote wanasema tunaitumikia serikali tukufu ya Tanzania!
Kwa bahati mbaya hii haihusiani na viwango vya elimu wala vyeo.Yaani, unachotakiwa kuomba Mungu kama sio kupigania kwa jinsi yoyote ni kuajiriwa katika asasi fulani. Bila kujali elimu yako, cheo chako au utendaji wako, maisha yako yatakuwa bora, saba wa sabini wa rafiki yako ambaye wewe ulipofeli kidato cha nne yeye aliendelea mpaka chuo kikuu. Kwa  uvivu wake wa kuomba Mungu au kutojua njia za kupita akajikuta anapata kazi za kutangazwa magazetini katika asasi zile zinazopangiwa viwango vya mishahara. Matokeo yake anapata jina kubwa mitaani lakini mfukoni hamna kitu. Kwanini usimkoge?
Mfano halisi ni Nyundo na Shoka,  majina ya kubuni. Wote wamemaliza masomo pamoja  Chuo Kikuu. Kozi moja, shahada moja na viwango  vya kufaulu sawasawa.
Nyundo, anafanya mipango anaajiriwa katika idara ya kukusanya kodi, mshahara wake ni shilingi milioni na nusu kwa mwezi. Nasema amefanya mipango kwa vile nafasi aliyoipata haikuwahi kutangazwa ili kutoa haki sawa kwa wote kuiwania. Shoka kahangaika mpaka alipoona tangazo gazetini, Polisi inahitaji watu wa fani yake. Akaomba akapata. Mshahara unatajwa kwa makeke, TGNP 05. Lakini ukweli ni shilingi tisini na tisa elfu na mia saba ishirini kwa mwezi, kabla ya makato yoyote. Yaani mshahara wa mwezi wa Nyundo ni sawa na mshahara wa mwaka wa Shoka. Hana la kufanya lazima ajiunge na kazi hiyo.
Aidha mazingira yao ya kazi ni tofauti sana. Wakati Nyundo anashughulika zaidi na wafanyabiashara na wakwasi, Shoka yuko na vibaka, wavuta bangi na majambazi. Hata Kingereza chake atakisahau baada ya miaka michache. Wakati Nyundo kila siku atafurahia takrima za wakwasi kwa kuwafanyia kazi nzuri ikiwemo kuwawezesha kutolipa kodi sahihi, Shoka akithubutu kuchukua alfu mbili za kibaka ili amuachie, kesho habari zimeenea mitaani kote. Kibaka na ndugu zake, na aliyeibiwa na ndugu zake, wote wanamshutumu Shoka kwa kupenda rushwa na kufuga uhalifu. Elfu mbili itakumbukwa milele!
Mwisho wa siku si tu vijana hawa wanasema wote wanaitumikia serikali ya Tanzania, lakini wanakutana mitaani na wanatembeleana majumbani. Bado ni marafiki. Wakati Shoka anaishi katika banda la mabati alilopewa na mwajiri wake, Nyundo ameshapata bangaloo alilojengewa na mkwasi fulani.  Shoka analazimika kuwa mhimili wa urafiki wao. Kila siku yeye ndio atamtembelea Nyundo nyumbani. Wataponda starehe kidogo kwa ubavu wa Nyundo halafu atarudishwa  mpaka kwake kwa usafiri binafsi wa Nyundo. Pengine hiyo ni baada ya mwaka mmoja tu wa kazi.
Kwa mawazo ya kipumbavu tutaamini Shoka hatamani maisha ya Nyundo.  Tutaamini yeye hapendi kutembelea gari au kuwa na nyumba nzuri. Hapendi kula vizuri au kustarehe kama Nyundo. Tutaamini kwamba kila siku atakubali kuendelea kuwa fukara huku akimuangalia rafiki yake waliosoma wote  akizidi kutajirika. Tunasahau kwamba Shoka huyu ndiye tunaempa silaha akalinde benki. Ndiye huyu tunayemtuma akapambane na majambazi na vibaka. Kadhalika ndiye mwenye jukumu la kutuhakikishia usalama wa raia na mali zao akiwemo rafiki yake Nyundo.
Hata hivyo hakuna upumbavu usio na utetezi. Hata kama kwa sababu za kipuuzi. Shoka ataambiwa kazi yake ni wito. Yeye ni mtumishi wa serikali wakati Nyundo ni mfanyakazi katika asasi inayojitegemea japo inamilikiwa na serikali. Lazima ajitoe mhanga kwa ajili ya mafanikio ya nchi au wananchi wenzake. Kadhalika si ajabu kusikia kwamba hawa tunawapa mishahara mikubwa ili wasichukue rushwa au kwa vile kazi yao inaiingizia serikali fedha nyingi. Hata hivyo hatujawahi kusikia sababu za wengine kupewa mishahara midogo japo tunasikia kila siku umuhimu wao ukihubiriwa.
Unaweza kujiuliza ni nini tofauti iliyopo kati ya serikali na idara au wakala wa serikali hadi kuwafanya watumishi wengine waishi peponi na wengine jehanamu  ndani ya nchi moja huku wakipumbazwa  na miito isiyo na maana. Jiulize,  ni nini hasa maana ya wito? Wote tunaajiriwa na vyombo vinavyomilikiwa na serikali ileile, sheria za kazi ni zilezile, tunaitumikia jamii ileile. Basi kama kazi ya mwingine ni wito na ya huyu mwingine inaitwaje?
Fikiria tena,  unaelewa nini unaposikia huyu analipwa mshahara mnono ili asichukue rushwa, eti kwa vile kazi yake inamuweka katika vishawishi vingi vya rushwa?  Hivi ni kweli serikali inashindwa kudhibiti mtandao wa rushwa kiasi inalazimika kuwabembeleza wala rushwa kwa kuwahonga ili wasichukue rushwa za wakwasi na wafanyabiashara? Kuna faida gani basi ya kuweka TAKUKURU na vyombo vingine vya usalama na upelelezi kama hongo ya aina hii ingetosha kuzuia rushwa?
Naiita hii ni hongo kwa vile inaonekana wazi serikali inajua kwamba viwango vya mishahara yake ni vidogo sana kulinganisha na maisha halisi. Ndio maana kwa zile idara inazohisi ni nyeti, inaamua kuzihonga kupitia mishahara mikubwa ili wasitamani rushwa. Lakini ni idara  gani basi ambayo serikali inadhani sio nyeti na wala haina nafasi ya kutawaliwa na rushwa?  Au inadhani imefanikiwa kiasi gani kuzuia rushwa katika zile idara au mamlaka inazozipa mishahara minono?  Kila mtu anaweza kuwa shahidi wa yanayotokea katika idara hizo.
Wachumi wanatuambia ni kanuni ya pesa,  kwamba kadiri zinavyokuwa nyingi ndivyo zinavyohitajika zaidi. Hatuhitaji tena ufafanuzi wa wachumi kuweza kulielewa hili hasa tukizitazama asasi hizi zinazopewa mishahara minono. Mpe mtu mwaka mmoja tu wa kazi tayari anaweza kuwa na jumba la kifahari na usafiri wa bei kali, achilia mbali matanuzi yake ya kila siku. Ni kweli serikali inatuambia hilo ni zao la mishahara minono inayowapatia watumishi hao pekee?
Upande mwingine ni umuhimu wanaopewa watu wa idara hizo. Tunatakiwa kuamini kwamba wanapewa mishahara mikubwa kwa sababu shughuli zao ni muhimu zaidi kwa serikali kuliko wengine. Wakati fulani  mheshimiwa rais  aliwapongeza TRA kwamba wametoa mchango mkubwa katika mafanikio ya serikali yake. Haikuwa muda mrefu sana tangu serikali hiyohiyo ipambane na madaktari ikiwalazimisha kuwapunguzia kipato kidogo walichokuwa wakikipata, ikatangaza kuwaongezea mishahara TRA kwa asilimia hamsini! Ujumbe gani unawaendea madaktari wale? Ina maana madaktari hawana umuhimu wowote mbele ya serikali yao!
Si lengo langu kupinga umuhimu wa asasi hizo lakini ni lazima serikali ikiri kwa dhati kabisa kwamba hakuna idara yake iliyo ya kipuuzi. Kila idara ilianzishwa kwa sababu na madhumuni kamili na ina ulazima na umuhimu wa kuwepo. Na kwa bahati kila mtumishi anaujua umuhimu wake mbele yake, kama sio serikali anayoitumikia basi jamii anayoihudumia. Ni kweli watu wanahitaji barabara za Tanroad au huduma nyingine zinazowezeshwa na kodi, lakini pia wanahitaji elimu, wanahitaji matibabu, wanahitaji ulinzi na usalama  wao, wanahitaji mahakimu, nk. Haya yote yanatolewa na watu ambao nao wanahitaji kuthaminiwa kama wenzao.
Nyundo na Shoka wanawakilisha makundi mawili ya watumishi wa, ama serikali kuu au idara zake, ambao kwa kweli tofauti zao kwa kiasi kikubwa hazitokani na umuhimu wa majukumu yao kwa serikali wala kwa wananchi ila viwango vya malipo yao ya  mishahara. Wote tunajua kwamba katika hali halisi heshima ya mtu hujengwa zaidi na kipato chake. Hivyo elimu, madaraka na hata umuhimu wa mtu kwa jamii utaonekana iwapo tu kipato chake kitafanana na kiwango cha umuhimu au elimu yake. Vinginevyo hakutakuwa na haja ya kupasua vichwa vyuoni kama kuna njia za mkato ya kuajiriwa na asasi teule.
Awali nimesema  akina Nyundo na akina Shoka hawa wanaishi katika jamii moja, na kwa bahati zaidi ni ama majirani, marafiki au ndugu. Wanatembeleana  na wanajuana. Kila linalotokea upande mmoja upande wa pili unaliona. Kwa hulka za kiutu ni lazima akina Shoka wanatamani mafanikio ya akina Nyundo, hivyo itawalazimu kufanya wawezalo wayafikie. Na kwa bahati mbaya, kama tukiamua kuwa wakweli hakuna njia yoyote ya halali inayoweza kumuwezesha Shoka kuyafikia maisha ya Nyundo. Matokeo yake lazima uhalifu wa jinsi yoyote utokee.
Mara nyingi tunapenda kutoa sababu au masuluhisho ya juujuu kwa matatizo yanayotukuta. Na zaidi huishia katika kulaumu na kutumia nguvu nyingi katika kuadhibu bila kujali vyanzo vya matatizo hayo. Sasa hivi ujambazi unanuka kila pembe ya nchi, rushwa na ubadhilifu vimetawala kila ofisi ya umma, na uadilifu katika ngazi zote umebaki huwa hadithi za kisiasa tu. Ni nini chanzo chake?
Si ajabu tena kusikia askari kashiriki ujambazi. Bunduki aliyopewa akalinde zamu kaenda kufanyia ujambazi! Kila siku mabenki na vyombo vingine vya umma vinaibiwa kwa mabilioni na kwa kiasi kikubwa ni kwa mipango ya wafanyakazi wake! Hujuma na wizi katika miundombinu  vimetapakaa kila sehemu, kwanini hatutafuti vyanzo vya hali hii.
Kila siku utasikia majibu rahisi. Kama sio tamaa basi ni ukosefu wa uaminifu kwa wafanyakazi. Ni kweli maelezo hayo ni sahihi lakini kwanini watu wasiwe na tamaa? Kwanini mtu awe muaminifu kama kipato chake hakimtoshi hata kwa wiki akijibana?  Au hata kwa siku kama atajaribu kuishi kama jirani yake anayefanya katika asasi teule? Vipi mtu asiwe na tamaa wakati anawaona wengine wanavyoishi katika pepo iliyomo ndani ya Jahanam? Kuna kosa gani mtu kutamani pepo?
Tabia ya kutamani huletwa na kuona vilivyomo katika mazingira mtu aliyomo. Huwezi kutamani kitu usichokiona au kukijua. Tunatamani kula vizuri kwa sababu tunawaona wenzetu wanakula vizuri. Tunatamani nyumba nzuri kwa sababu tunaziona mitaani. Tunataka kufanya harusi za kifahari kwa vile wengine wanafanya hivyo. Mtu hawezi kutamani kuwa na jumba kama la Michael Jackson au kutembelea Cadilac kwa vile havipo kwenye upeo wake. Lakini vipi afisa muaminifu wa TAKUKURU kwa miaka kumi huku akipanga pale Buguruni asitamani kuwa na jumba kama la mdogo wake wa TRA pale Tabata alilolijenga baada wa miezi miwili tu ya utumishi?  Jiulize kitakachofuatia.
Katika mazingira ya kawaida si ajabu mtu wa kundi la Nyundo kuniona mnoko au fitina kwa kuongelea haya, lakini huu ndio ukweli unaopaswa kusemwa hata kama hautaweza kuibadili hali halisi. Hatuwezi kuzuia uhalifu katika mazingira yasiyo na uwiano wa kipato  kama haya. Na huu ni moja ya ushauri wangu kwa serikali hii na ijayo. Isiruhusu tofauti kubwa ya vipato miongoni mwa watumishi wake au wa idara, mamlaka wala  wakala zake kama ilivyo sasa.
Kama kuna muujiza wa kupandisha mishahara ya wote basi ipandishwe angalau tofauti isiwe kubwa kama ilivyo sasa, na kama haiwezekani basi patafutwe mbinu ya kuifanya  mishahara iwe na uwiano unaoeleweka. Hakuna atakaeacha kazi BOT kwa sababu eti mshahara umepungua. Kwanza kwa vile hatakuwa na pa kwenda lakini zaidi kutakuwa na uwiano wa vipato mitaani. Angalau hii itakuwa njia ya mkato ya kupunguza uhalifu.  Vinginevyo hakuna atakaekubali kuendelea kuwa masikini wakati anamuona jirani yake anachezea pesa, ilhali wote wanaitumikia serikali moja.
0784 989 512
Next Post Previous Post
Bukobawadau