Bukobawadau

UCHAGUZI WA MADIWANI KATA 27 CHADEMA KIDUME!!

Na Prudence Karugendo
UCHAGUZI  mdogo wa madiwani uliofanyika Jumapili iliyopita katika kata 27 nchini umenifunulia kitu kimoja muhimu. Baada ya kuutafakari uchaguzi huo mara moja nimegundua kwamba kumbe Chama Cha Mapinduzi hakina tena ushawishi kwa wananchi pamoja na mambo yote kiliyonayo, utawala, mabavu na kila kitu!
CCM kimebaki kutumia kila kitu kilicho kwenye upeo wake kuhakikisha kinabaki kileleni bila kujali mapenzi ya wananchi huku chini yakoje. Dalili zinaonyesha kuwa chama hicho kiko kileleni kwa nguvu zake chenyewe, na sasa uchovu unakifanya kianze kuteleza na kushuka taratibu pasipo kupenda. Kingekuwa kimeshikiliwa na wananchi apana shaka hali hiyo isingekuwepo, kingebaki imara kileleni.
Badala yake ni kwamba chama kikuu cha upinzani nchini, Chadema, ndicho kimedhihirisha kuwa ni chama dume kwelikweli! Sababu pamoja na nguvu ya ziada kinayokabiliana nayo bado kinapanda, hata kama ni kwa mwendo wa kinyonga, wakati kilicho juu kileleni kinashuka hata bila kupenda, utelezi umekizidi nguvu!
Hatahivyo wapo wanaochanganywa na matokeo yanayoonyesha kuwa CCM kimeshinda kata 23, Chadema kata 3 na NCCR Mageuzi kata 1, na hivyo kuchukulia kuwa CCM imepata ushindi wa kishindo. Kumbe mambo hayako hivyo. Wanaoyachukulia mambo kwa mtazamo huo ni wale wasioweza kuitafsiri hali halisi.
Kwangu mimi matokeo hayo yananifanya niipongeze NCCR Mageuzi iliyopata kata 1 kuliko CCM iliyopata kata 23. Ni kwa sababu kabla ya uchaguzi huo mdogo, tukiangalia uchaguzi uliotangulia, CCM ilipata kata 25 kati ya kata 27 zilizofanya uchaguzi huo mdogo, NCCR Mageuzi haikupata hata kata 1.
Lakini katika uchaguzi huo wa juma lililopita CCM imepata kata 23, nafasi mbili kwenda chini, na NCCR Mageuzi kata 1, nafasi moja kwenda juu. Tuseme NCCR Mageuzi imepata kata 1 na CCM imepoteza kata 2. Sasa nani apongezwe, aliyepata au aliyepoteza?
Tukija upande wa Chadema tutaona kuwa chama hicho kilikuwa kinatetea kata 2 tu lakini kikaja kupata kata 3, kimepanda. Sababu kupoteza ni kupoteza na kupata ni kupata. Haijalishi umepoteza au kupata kiasi gani.
Huwezi kufiwa na mtoto mmoja ukawaambia waombolezaji wasikupe pole eti kwa vile bado unao watoto wengine 30! Na huwezi kukataa hongera ya kuzaa kwa vile umezaa mtoto mmoja badala ya mapacha!
Hiyo ni kwamba mimi nikiulizwa nasema CCM imepoteza kata 2 katika 25 ilizokuwanazo kibindoni, na Chadema imeongeza moja katika kata 2 ilizokuwa imeziweka kibindoni. Sasa nimpongeze aliyepoteza niache kumpongeza aliyeongeza! Hayo yatakuwa ni mehesabu ya ajabu.
Mbali na matokeo hayo tunapaswa kuangalia uchaguzi unafanyika katika mazingira ya aina gani, kwakweli haya sio mazingira yaliyo sawa na huru hata kidogo.
Katika uchaguzi hapa nchini vyama vya upinzani vinaonekana kukabiliwa na upinzani toka kila upande. Vinakabiliwa na chama tawala, wakati huohuo vinakabiliwa na Tume ya Uchaguzi, Polisi na wakati mwingine hata Jeshi!
Ikumbukwe kwamba wakuu wa vyombo hivyo vyote wanateuliwa na rais ambaye ndiye mwenyekiti wa chama tawala. Je, wakuu wa vyombo hivyo vya dola wangependa kumwangusha bosi wao kwa kukiacha chama chake kishindwe katika uchaguzi? Hivi ni nani anayeyajua makubaliano yao yakoje anapowateua wakashike nyadhifa hizo? Maana mpaka sasa hakuna chombo chochote cha kuhahakiki uteuzi unaofanywa na rais, aliye pia mwenyekiti wa chama tawala.
Katika nchi nyingi ambazo utawala unajali zaidi umimi, kuliko maslahi mapana ya umma,  hususan katika Afrika, niliyoyataja hapo juu yanaadhiri chaguzi kwa mtindo huu: Mfano hapa kwetu,  Tume ya Taifa ya Uchaguzi ambayo muda wote ipo kushughulikia masuala ya uchaguzi unapojitokeza haijionyeshi kama ni ya kudumu. Tume hiyo inaonekana kufanya mambo yake kana kwamba inateuliwa kwa dharura tu kila uchaguzi unapotokea!
Kama sio hivyo kwa nini Tume hiyo inakubali kuendesha uchaguzi kwa kutumia Daftari  la Kudumu la Wapiga Kura lililopitwa na wakati? Katika daftari hilo ni wapiga kura wangapi wanaokuwa wamepoteza maisha lakini majina yao yakabaki kudumu kwenye daftari hilo yakionyesha kuwa hao ni wapiga kura halali? Na kwa upande mwingine ni wananchi wangapi wanaokuwa wamefikisha umri wa kupiga kura na hawamo kwenye daftari hilo kutokana na kukosa uboreshaji na kuonekana limepitwa na wakati?
Kwa nini uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura usiwe endelevu kama Tume yenyewe ilivyo endelevu? Wakati usio wa shughuli za uchaguzi Tume hiyo inafanya kazi gani nyingine inayoizuia kutambua nani kafikisha umri wa kupata haki yake ya kupiga kura na nani kapoteza haki hiyo kihalali, kwa maana ya kupoteza maisha?
Sababu haki za raia ni pamoja na uhuru wa kupiga kura, na uhuru huo, kwa mujibu wa Katiba ya sasa ya nchi yetu, unaanzia miaka 18. Sasa ni milioni ngapi za wananchi wanaofikisha umri wa miaka 18 kila mwaka tangu daftari hilo lifanyiwe uboreshaji kwa mara ya mwisho? Kwa nini wananchi hao wanyimwe haki yao hiyo ya msingi kwa uzembe wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi?
Je, Tume hiyo inafanya hivyo kwa kujiamria yenyewe au kwa kuelekezwa na walioiteua?
Kuna hoja ya ajabu inayojitokeza ya kwamba Tume inakwepa gharama za kila wakati za uboreshaji wa mara kwa mara wa daftari hilo! Lakini cha kushangaza ni kwamba wafanyakazi wa Tume hiyo wanapata mishahara kila mwezi! Mbona hatujiulizi kwa nini tuwalipe watu mishahara bila kazi yoyote wanayoifanya? Au gharama hizo zinamwendea nani?
Tume ya Taifa ya Uchaguzi ipo kuhakikisha haki ya kila raia ya kupiga kura inalindwa, ndiyo maana wafanyakazi wa Tume tunawalipa mishahara. Sasa inawezekanaje tuendelee kuwalipa mishahara ilihali wakilikwepa jukumu hilo muhimu tulilowakabidhi la kuilinda haki hiyo ya kila mwananchi kwa kisingizio cha kukwepa gharama? Kwa nini gharama isikwepwe kwenye mishahara yao ila tu kwenye jukumu muhimu lililowafanya wao wakaajiriwa?
Tukirudi kwenye uchaguzi mdogo wa madiwani uliopita tutaona yafuatayo. Mfano, katika kata ya Nduli mjini Iringa, karibu uongozi wote wa mkoa wa Iringa ulishinda katika kitongozji cha Nduli, siku ya uchaguzi, ukiwa umejihami na kikosi cha polisi cha kuzuia fujo kikiwa kimejikamilisha na silaha zake, wakati pale hapakuwepo na fujo yoyote. Lengo lao lilikuwa ni kuhakikisha mgombea wa chama tawala anaibuka mshindi hata kama hakupigiwa kura na yeyote!
Mara nyingi fujo na vurugu hutokea mahali ambako haki inapindishwa. Kama hupangi kupindisha haki huna haja ya kutegemea fujo na vurugu vitokee. Na kama haki imekwenda mahali pake, kwa walio wengi, huna haja ya kuwahofia sana wachache, walioshindwa, maana walio wengi wanaweza wakajilinda. Vinginevyo kulazimisha hofu mahali haki inapotendeka ni kuleta vurugu na fujo ukiwa umelenga kuipindisha haki.
Kule Nduli, Iringa, hakuna chombo chochote cha dola kilichowagusa viongozi hao wa mkoa ambao karibu wote hawakuhusika na uchaguzi wa diwani, lakini alipojitokeza mbunge wa Iringa Mjini, Mch. Peter Musigwa, aliyekuwa anahusika na uchaguzi ule, kwa vile Nduli ni kata ya nyumbani kwake,  mbali na kuwa mbunge wa jimbo, akiwa anaangalia mwenendo wa uchaguzi, akashikiliwa na polisi!
Yeye na mawakala wawili wa Chadema walishikiliwa kwa muda usiopungua masaa matatu. Wakati huo kura zikiendelea kuhesabiwa kwa kushuhudiwa na upande mmoja tu wa CCM! Matokeo yake CCM ikaonekana imeshinda kwa mshangao wa kila mmoja!
Kule Sombetini,  Arusha Mjini, mbunge Godbless Lema amepigwa sana na polisi. Pamoja na kwamba mbunge ni mwakilishi wa wananchi aliye na kinga ya kutofanyiwa upuuzi na vyombo vya dola, lakini yeye kapigwa! Kumpiga mbunge ni sawa na kuwapiga wananchi wote anaowawakilisha. Ni heri akapigwa mkuu wa mkoa lakini sio mbunge, sababu mkuu wa mkoa hamwakilishi yeyote pale zaidi ya kuyasimika mamlaka, utawala.
Naamini polisi waliofanya kitendo hicho cha kuwapiga wananchi bila huruma yoyote kupitia kwa mwakilishi wao sio vichaa, walikikusudia walichokifanya. Na kwa vile hatukuona tamko lolote toka serikalini la kuukemea unyama huo wa polisi, kuwapiga watu wanaowalipa mishahara ili wakawalindie usalama wao, ni lazima tuamini kwamba vijana hao walitumwa na serikali kufanya unyama huo.
Hivyo tunalazimika kujiuliza, serikali isiyowajali wananchi wake kiasi cha kuwapiga bila hatia yoyote, kwa vile yenyewe inayo mabavu ya kufanya hivyo, ipo kwa manufaa ya nani?
Kwa mantiki hiyo, matokeo hayo yanayoshangiliwa na wana CCM, wengi wao wakiwa hawaelewi jinsi yalivyopatikana, yamewafanya baadhi ya wana Chadema wafikirie kwamba ingebidi chama chao kibadili mbinu za mashambulizi ya kisiasa. Eti badala ya mashambulizi ya hanga sasa kianze mashambulizi ya ardhini kuikabili CCM.
Kinachosahaulika ni kwamba CCM imetumia njia hiyo ya ardhini kuwapofua wananchi kwa karibu miaka 60. Kwa maana hiyo mpaka Chadema ijiimarishe na kuweza kuwaondolea wananchi upofu uliosababishwa na CCM kwa kutumia njia hiyohiyo ya ardhini si ajabu ikahitaji muda usiopungua miaka 40!
Ninaposema CCM na miaka 60 wapo wanaoshangaa wakiwa wanaamini kwamba chama hicho kimezaliwa 1977! Ieleweke kwamba kilichozaliwa wakati huo ni jina wala sio chama. Kwani mtu akibadili jina na umri wake unabadilika?
Pamoja na kwamba ni muhimu Chadema kujiimarisha katika ngazi ya mashina kwa wakati huu, bado mashambulizi ya hanga ni muhimu sana. Yamekifanya chama kiwafikie wananchi kwa haraka sana kote nchini. Ndiyo maana hata CCM kimeanza kuiga mbinu hiyo ya hanga kinapojaribu kujifufua.
Naipongeza sana Chadema kwa ushindi wake ilioupata katika kata 3 kwa vile ni ushindi uliopatikana  katika mazingira magumu sana. Sababu katika hali ya hofu na kukata tamaa Chadema isingeweza kupata hata nusu kata, achilia mbali hizo kata 3, kulingana na nguvu za dola zilizotumika dhidi yake. Kwakweli Chadema ni chama dume, Watanzania tukiunge mkono tukiwa tumeutupilia mbali woga wa kila aina.
0784 989 512
Next Post Previous Post
Bukobawadau