Bukobawadau

MCHAKATO WA UBUNGE CHALINZE-TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Chama cha Demokrasiana Maendeleo (CHADEMA) Jimbo la Chalinze kimeanza mchakato wa ndani wa kupata mgombea ubunge kwa ajili ya uchaguzi mdogo unaotarajiwa kufanyika mapema mwezi Aprili, mwaka huu, ambapo fomu za uteuzi zimeanza kutolewa kwenye Ofisi Jimbo, kuanzia tarehe 4 Machi na mwisho wa kuchukua na kurejesha fomu hizo itakuwa tarehe 7 Machi 2014, saa 10.00, jioni.

Kura za maoni ndani ya chama, zitafanyika tarehe 8 Machi katika Mji wa Chalinze na kufuatiwa na kikao cha kamati ya utendaji ya jimbo ili kufanya uteuzi wa awali kwa mujibu wa Katiba ya chama na hatimaye kikao cha Kamati Kuu kufanya uteuzi wa mwisho ili kupata mgombea atakayeshindana na wagombea wa vyama vingine.

Mpaka sasa wagombea waliochukua fomu kwenye ofisi ya jimbo ni watatu (3) na wagombea wengine watatu (3) wamechukulia fomu Ofisi za Makao Makuu ya Chama, Dar es Salaam, hivyo hadi sasa idadi ya wagombea waliotambuliwa rasmi ni sita.

Tunatumia nafasi hii kuujulisha umma wa Watanzania, hususan wanachama wa CHADEMA, kuwa fomu za kuwania uteuzi wa ndani zinaendelea kupatikana sehemu tatu, Makao Makuu ya Chama, Ofisi ya Jimbo la Chalinze na kwenye tovuti ya chama www.chadema.or.tz



Imetolewa Machi 5, 2014 

Iddi Omary Ucheche

Katibu wa CHADEMA, Jimbo la Chalinze
Next Post Previous Post
Bukobawadau