Bukobawadau

UZINDUZI WA JK WATUBADILISHA WENGI MTAZAMO

Na Bernard Kazinduki
KABLA  ya uzinduzi wa Bunge Maalumu la Katiba, uliofanywa na Rais Jakaya Kikwete siku ya Ijumaa, 21 / 3 / 2014, kichwa changu kilikuwa kimejaa mambo mengi juu ya mustakabali wa nchi yetu.
Kabla sijaeleza mengi kwanza nijitaje kuwa mimi ni mpinzani. Sikubaliani kabisa, kiitikadi na kisera,  na chama kinachotawala hapa nchini kwetu, CCM, kutokana na haya nitakayoyaeleza hapa chini.
Naamini kwamba kuendelea kutawala kwa CCM kunaifanya nchi yetu iendelee kudumaa. Sababu chama hicho kimeitawala nchi yetu kwa zaidi ya miaka 50, lakini nchi bado inaitwa changa! Wakati huohuo chama hicho kinajidai kutuonyesha mafanikio ya kitoto ambayo tunaweza kuyafananisha na mafanikio wanayoyafurahia wazazi ya mtoto wao mdogo kuanza kutambaa au kusimama dede!
Ikumbukwe kwamba wakati nchi yetu inapata uhuru wake toka kwa wakoloni, mwaka 1961, kimaendeleo Tanganyika ilikuwa sawa na nchi ya Korea ya Kaskazini. Najua kuna watakaoniona kichaa kuyalinganisha maendeleo ya Korea na ya Tanganyika kulingana na tofauti iliyopo kwa wakati huu. Lakini huo ndio ukweli wenyewe.
Kwa upande mwingine Tanganyika ilikuwa mbele kimaendeleo ikizitangulia nchi nyingi za Mashariki ya Mbali kama Thailand, Singapore, Malaysia, Indonesia nakadhalika. Lakini kwa sasa tofauti ya kimaendeleo kati ya nchi hizo na Tanzania, iliyokuwa Tanganyika miaka hiyo, haitofautiani na tofauti ya ardhi na mbingu!
Ni kubwa sana kiasi kwamba kwa mtu ambaye hakuwahi kuifuatilia tangu mwanzo akikusikia unasema kwamba nchi hizo zilikuwa nyuma ya Tanganyika kimaendeleo wakati fulani ni lazima akuone una kichaa.
Kwa ufupi ni kwamba hayo yote yanasababishwa na chama tawala hapa kwetu ambacho mwanzoni kilijulikana kama TANU, Tanganyika African National Union.  Kwa tafsiri isiyo rasmi, Muungano wa Kitaifa wa Waafrika wa Kitanganyika.
Ila miaka 15 baadaye, mwaka 1977, baada ya uongozi wa chama hicho kujiridhisha kuwa kilichokuwa kimelengwa kimeishapatikana, uongozi ukaushawishi uongozi wa chama kingine cha ASP, upande wa Visiwani, kwamba vyama hivyo viungane na kutengeneza chama kimoja. Ndipo kikaundwa Chama Cha Mapinduzi, CCM.
Mpaka leo sijaelewa jina hilo la CCN lina maana gani. Sielewi ni kitu gani kinapinduliwa kiasi cha kuliona neno hilo linafaa kuwa jina la chama kinachotawala nchi ya kidemokrasia. Ila kwa kuyaangalia mambo yalivyo nalazimika kuhisi kwamba pengine kilicholengwa kupinduliwa na chama hicho ni mafanikio yaliyopatikana katika kipindi hicho cha miaka 15 tangu nchi ilipopata uhuru wake mpaka mwaka kilipoanzishwa chama hicho, huku kaulimbiu ikiwa kwamba chama kimeshika hatamu, sawa na mpanda farasi.
Mara zote mpanda farasi ndiye huwa anashika hatamu, asipofanya hivyo ni lazima ataanguka wakati farasi akiendelea na safari zake.
Hayo tuyaache. Lengo la makala hii ni kutaka kumpongeza mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, kwa hotuba yake ya uzinduzi wa Bunge Maalumu la Katiba.
Kusema ukweli watu wengi wa upande wa upinzani, nikiwemo mimi, tulikuwa tunaichukulia hotuba hiyo ya rais kama ufagio wa kukifagilia chama chake ili katiba itakayoandikwa na Bunge Maalumu ikijengee mazingira ya kuendelea kudumu madarakani, hasa baada ya baadhi ya kanuni za Bunge hilo maalumu kutenguliwa, kwa namna ambayo zilionekana zimevunjwa makusudi, ili Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Sinde Warioba, atangulie kuwasilisha Rasimu ya pili ya Mabadiliko ya Katiba ndipo rais aje kulizindua Bunge.
Kilichosababisha kukawepo na mashaka juu ya uzinduzi huo ni utaratibu uliotumika wa kutengua kanuni iliyokuwa ikisema kwamba Bunge litazinduliwa kwanza ili Warioba awasilishe Rasimu katika Bunge ambalo tayari linafanya kazi, kwa maana ya kwamba tayari limeishapewa dhamana ya kufanya kazi ya kuichambua rasimu.
Lakini sasa kilichofanyika ni kama Warioba aliwasilisha Rasimu katika kitu tunachoweza kukiita “kijiwe”, mkusanyiko ambao haukuwa rasmi. Ni kwamba aliwakabidhi Rasimu watu ambao walikuwa hawajapewa rasmi majukumu ya kuichambua Rasimu hiyo, watu ambao bado walikuwa wanajiandaa kutengeneza Bunge Maalumu. Lile lilikuwa halijawa Bunge kwa sababu lilikuwa halijazinduliwa.
Jambo hilo liliwafanya wapinzani, nikiwemo mimi, pamoja na wale wanaounda UKAWA, Umoja wa Katiba ya Wananchi, wajawe mashaka ya kwamba mpango huo ulilenga kuyazima yale yaliyokuwa kwenye maelezo ya Warioba kuhusu Rasmu ya Katiba Mpya.
Hata kwa upande wa CCM, wapo ambao inaonekana hawaelewi kilichowapeleka Dodoma, watu wasioutilia maanani mustakabali wa nchi yao. Wao walidhani JK anakwenda Dodoma kumpiku Warioba ili suala zima la Katiba Mpya liwe la kukilegezea mambo chama chama chao. Mawazo yao hayalengi hata kidogo katika kuinufaisha nchi ispokuwa chama tu!
Lakini ajabu rais alipopanda kwenye mimbari pale Bungeni akauvua ukada wa chama chake na kuutupa pembeni na kubaki tu na uzalendo wa nchi yake! Kusema ukweli sikuuona ukada wa Kikwete kwenye hotuba yake isipokuwa nilikuwa nauona uzalendo tu.
JK alisisitiza kwamba katika tume 4 zilizotangulia suala la Muungano lilikuwa linajitokeza likionyesha matatizo ya kiufundi yaliyohitaji marekebisho. Tume zote 4 zilishauri marekebisho hayo yafanyike kwa Jamhuri ya Muungano kuwa na serikali 3. Lakini mara zote serikali hizo 3 zikawa zinashindikana na kubaki na serikali 2 tu, jambo lilisababisha tatizo au “kero za Muungano” kubaki palepale.
JK akawahimiza wajumbe wa Bunge Maalumu kwa kuwashauri kwamba mara hii wajaribu kulimaliza kabisa tatizo hilo. Baadhi ya wajumbe wa CCM, ambao naamini hawakumuelewa, wakidhani anaongea kichama, waliinuka kwenye viti vyao wakishangilia kwa vile walishajipanga kufanya hivyo ili kuwakomoa wapinzani!
Lakini mimi mpaka hapo niliona kuwa JK anakubaliana na serikali 3. Sababu kama tume 4 zimeshindwa kuliondoa tatizo kwenye Muungano baada ya ushauri wake wa serikali 3 kutupiliwa mbali, sasa mara hii JK anasema wajitahidi kulimaliza, ana maana gani kama sio kwamba tujaribu na serikali 3 ili tuone?
Sababu kwa kauli yake hiyo alionyesha wazi kwamba hakuna namna yoyote ambayo ingeweza kulimaliza tatizo lililoshindikana katika tume 4, isipokuwa ni kukubaliana na serikali 3.
Ila akatahadharisha kwamba kwa kufanya hivyo, kuzikubali serikali 3, ni kuwa tayari kuachana na Muungano. Akatoa mfano ulio hai wa uliokuwa Muungano wa Urusi pale kila jimbo lilipokubaliwa kuendesha mambo yake kivyake na juu kukiwepo na serikali kuu ya muungano.
Akasema kilichotokea ni serikali kuu kujikuta haina nguvu wala mamlaka katika mabadiliko hayo ya Perestroika na Glasnost,  wakati kila jimbo lilipogeuka kuwa nchi kamili. Na huo ndio ukawa mwisho wa muungano mkubwa wenye nguvu sana wa Urusi.
Kwahiyo rais alichokimaanisha hapo ni kwamba iwapo Katiba itasema Tanzania iwe na serikali 3 Muungano utakuwa haupo tena. Nadhani kwa mtu yeyote ambaye ni muumini wa muungano huu, kama alivyo yeye rais aliyekalia kiti cha mmoja wa waasisi wa Muungano huo, asingependa kuona muungano unamfia mikononi mwake kama ilivyotokea kwa Mikhail Gorbachev wa Urusi. Bilashaka JK anaogopa historia isije kumhukumu.
Wakati huohuo wapo waliokuwa wakisema kwamba rais alichotakiwa kukifanya ni kufungua Bunge na kuondoka zake! Lakini eti badala yake akaanza kuchambua Rasimu. Kwa upande wangu naona kwamba rais ambaye angefungua Bunge na kuondoka zake angekuwa anafanya kama Wahaya wasemavyo kwamba “Birangw’enyuma”, usemi unaoonyesha kutokujali, kwamba potelea mbali yatakayotokea sitakuwepo.
Lakini rais anayejali ni lazima angefanya kama alivyofanya JK. Sababu naye, akiwa raia wa nchi hii,  hiyo ilikuwa nafasi yake, kuchangia namna anavyoona Katiba ya nchi yake inafaa kuwa. Sidhani kama Jaji Warioba aliwahi kuchukua maoni yake kabla. Ndiyo maana kila JK  alipokuwa anamaliza kuongea anawambia wajumbe kuwa hayo ni maoni yake wao wataamua ni kipi wakifuate na kipi wakiache.
Nimalize kwa kusema kwamba kwa vyovyote ilivyo Rais Kikwete amenishawishi niwe upande wa serikali 2. Nadhani atakuwa pia amewashawishi watu wengi kwa njia hiyo. Ndiyo maana akawashauri wajumbe kwamba watumie nguvu ya ushawishi kuliko nguvu ya kulazimisha katika kuunda Katiba Mpya.
Next Post Previous Post
Bukobawadau