Bukobawadau

WATANO WAONGOZA KUCHANGIA BUNGENI

Dodoma. Tangu kuanza kwa Bunge Maalumu la Katiba, Februari 18 mwaka huu,  wajumbe watano  wanaonekana kuwa ndio wachangiaji wakuu katika mjadala wa Rasimu ya Kanuni za Bunge hilo.
Bunge hilo la Katiba limekuwa likijadili Rasimu ya kanuni za Bunge kwa takriban wiki moja sasa na mjadala huo bado hilo haujamalizika kutokana na mivutano miongoni mwa wajumbe kuhusu baadhi ya vifungu vya kanuni hizo.
Pamoja na Bunge hilo kuwa na wajumbe 629, wanaochangia kila mara ni Mbunge wa Simanjiro (CCM), Christopher Ole Sendeka, Mbunge wa Kigoma Mjini (CCM), Peter Serukamba, Mbunge wa Nzega (CCM), Hamisi Kigangwalla, Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika (Chadema) na Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Ezekiel Oluoch.
Mbali na kuchangia, wakati mwingine wajumbe hao wamekuwa wakinyoosha mikono au kusimama kwa lengo la kuchangia, lakini wanakosa nafasi.
Mfano mzuri ilikuwa ni jana wakati wa mjadala kuhusu Rasimu ya Kanuni za Bunge hilo, wakati Ole Sendeka na Oluoch waliposimama na kuchangia.
Katika mjadala wa juzi, wajumbe hao wawili kila mmoja alichangia mara tatu na mara nyingi walipochangia hoja zao ziliungwa mkono na wajumbe wengi.
Kigwangalla naye hayuko nyuma kwani katika mjadala wa juzi alipewa nafasi mara mbili kuchangia na wiki iliyopita huchangia mara mbili  kwa siku isipokuwa siku moja tu ambayo alichangia mara moja.
Mjumbe mwingine ni Mnyika ambaye katika mjadala wa juzi alichangia mara mbili kuhusu mkanganyiko juu ya kuchagua aina ya upigaji wa kura.
Naye Serukamba amekuwa mchangiaji wa karibu kila siku na Ijumaa iliyopita alichangia kuhusu kifungu cha 37 na 38 cha Rasimu ya Kanuni hizo.
Sasa imekuwa jambo la kawaida kwa  wajumbe hao kuchangia katika Bunge hilo.
Next Post Previous Post
Bukobawadau