Bukobawadau

WA TZ WEPESI WA KUSAMEHE

 Kifo cha Gaddafi, Watanzania ni wepesi wa kusamehe na  kusahau
Na Prudence Karugendo
JUMA lililopita niliandika makala yenye kichwa cha habari “Kifo cha Gaddafi ba maajabau ya Watanzania” lakini kutokana na hitilafu za kiufundi makala hiyo ikaonyesha anwani ya Padri Privatus Karugendo. Huyo ni mtu tofauti na Prudence Karugendo, mtazamo wake na wa kwangu zinapishana katika baadhi ya mambo.  Naomba radhi kwa usumbufu wowote uliotokana na hitilafu hiyo.
Lakini hatahivyo ujumbe wa makala hiyo uliwafikia walengwa, Watanzania. Waliobahatika kuupata ujumbe wa makala hiyo waligawanyika katika sehemu tatu, wapo waliotokea kuuelewa na kukubaliana nao wakati wengine wakiwa wameuelewa lakini hawakutaka kukubaliana nao kutokana na sababu wanazozielewa wao wenyewe. Pia wapo ambao hawakuuelewa kabisa ujumbe wa makala yangu hiyo, wakaishia kutoa maoni yenye vichekesho vya kuduwaza.
Hoja yangu kuu katika makala yangu hiyo ya juma lililopita ilikuwa kwamba mtawala wa Libya aliyeangushwa na baadaye kuuawa na wapinzani wake, Muammar Gaddafi, hakuwa mtu mwema kwetu, sisi Watanzania, na pengine Waafrika weusi kwa ujumla.
Nilijaribu kukumbusha maovu aliyotufanyia Gaddafi, sisi Watanzania, kwa kusukumwa na ukwasi wa mafuta ya nchi yake mwishoni miaka ya 1970 na mwanzoni mwa 1980. Maovu hayo yanaonekana kusahaulika vichwani mwa baadhi ya Watanzania,  wengi wao wakiwa wameingizwa kwenye vishawishi vya Gaddafi vilivyokuwa vinakuja kwa njia ya zawadi za “lambalamba”, tende na halua. Utamu wa tende na halua ukawa umemsafisha Gaddafi machoni mwa Watanzania huku kumbukumbu zote chafu za mtu huyo zikiwa zimefutika kabisa!
Pia nilieleza kwamba Waarabu wa Afrika Kaskazini mpaka Kaskazini Magharibi wanajiita Waafrika kwa lugha ya kisiasa tu, lakini kilicho ndani ya roho zao wanakielewa wao. Na hiyo si siri, ni kwamba wao wanajitambua kuwa sio Waafrika bali Waarabu, kitu ambacho hakina ubishi wowote. Sie weusi ndio tunaodai wale ni Waafrika wenzetu wakati wao, katika nyakati tofautitofauti, hawakubaliani na jambo hilo.
Ndiyo maana kitendo cha Gaddafi kutumia nguvu zake zote kutaka Afrika iungane na kuwa nchi moja kilikuwa kinanipa mashaka makubwa sana. Ni kwa sababu nilikuwa naelewa kwamba hakuna muungano unaokubalika kati ya mtu mweusi na Mwarabu.
Mifano hai ipo mingi. Bara la Afrika ni la watu weusi, lakini kule Kasikazini kulikovamiwa na kukaliwa na Warabu tunaona kwamba weusi hawapo kabisa kitu ambacho kinawafanya baadhi ya watu waamini kwamba Warabu ni watu wa asili katika maeneo hayo. Lakini ukweli ni kwamba Waarabu ni wavamizi tu waliowahamisha wenyeji weusi kuja kusini wengi wao wakiwa wameangamizwa.
Mfano mwingine ni wa hivi karibuni wa nchi ya Sudan. Tumeona jinsi Waarabu wa Sudan, tena Waarabu koko,  walivyoshindwa kuishi kwa amani katika nchi moja na weusi wa Sudan Kusini mpaka ikalazimika nchi hiyo itengwe ili weusi wa Kusini nao wawe na nchi yao.
Kwa ufupi ni kwamba mpango wa Gaddafi kutaka kuharakisha muungano wa Afrika binafsi nilikuwa nautafsiri kama mpango wa kuyaharakisha maangamizi ya weusi. Kama hilo halikuwa kichwani mwa Gaddafi, tuseme hizo ni fikra zangu potofu, ni kitu gani kilichomzuia Gaddafi, mtu msomi na mweledi wa historia na asili za watu, kuanza na kuwatafuta watu wa asili ya Libya ili awarudishe kwao kama walivyowahi kufanya Wayaudi kwa ndugu zao waliokuwa wamesambaa katika sehemu mbalimbali za dunia? Katika kufanya hivyo ndipo tungemuamini Gaddafi kwamba alikuwa amedhamiria kuwaona Waafrika wakiwa kitu kimoja bila kujali tofauti zao za rangi.
Lakini kumuamini mtu aliyekuwa akiwabagua hata Waarabu wenzake kwa misingi ya kwamba wanatoka sehemu alikozaliwa mfalme aliyempindua yeye Gaddafi mwaka 1969, kwamba angeweza kuiunganisha Afrika ya weusi na ya Waarabu kuwa kitu kimoja, ilikuwa sawa na watu weusi kuuchezea moto ambao baadaye ungekuja kuwaunguza kijuha! Kwa hilo siamini kabisa kwamba Gaddafi alikuwa na dhamiri ya haki.  Na kilichompata sasa ni ile adhabu iliyoumbiwa ndani ya kosa kama alivyowahi kuielezea Mwalimu Nyerere. Gaddafi kapanga kuwaangamiza Waafrika kaangamia mwenyewe. Kapanga kosa na kupata adhabu ndani ya kosa lilelile.
Tukirudi kwenye usahaulifu wa Watanzania tutaona kwamba hali hiyo inaweza kutupeleka kwenye maangamizi endapo hatutaifanyia marekebisho. Watanzania ni wepesi sana wa kusamehe na kusahau. Tunaweza tukasamehe ndiyo, lakini kusahau ni kosa la mauti. Kusahau ndiko husababisha kosa kujirudia tena na tena  kwa njia ileile na kumfanya anayeathirika na kosa husika kuonekana zuzu!
Katika makala iliyopita nilieleza juu ya Vita ya Kagera, vita ambayo tulilazimika kupigana ili kuikomboa nchi yetu baada ya kuvamiwa na kutekwa na mtawala mwendawazimu wa Uganda, Idd Amin Dada. Na nilieleza jinsi Muammar Gaddafi wa Libya alivyojiunga na mwendawazimu huyo wa Uganda ili kumsaidia kuimarisha uvamizi wake nchini mwetu. Tendo hilo la kishenzi tungeweza kulisamehe, kama tulivyolisamehe, lakini kulisahau ni ujinga uliopitiliza.
Bahati mbaya baadhi ya Watanzania wameishausahau uovu huo aliotufanyia Gaddafi, wanakumbuka tu tende na halua ambazo Gaddafi amekuwa akizileta siku za karibuni kuelekea kuangamia kwake.
Inawezekana asilimia kubwa ya Watanzania wa sasa haikuwepo wakati huo wa Vita ya Kagera, lakini hatahivyo vita hiyo iko kwenye historia ya nchi yetu tunayoienzi kama ilivyo tarehe ya uhuru wa nchi yetu ambao ulishuhudiwa na asilimia ndogo sana ya Watanzania waliopo kwa sasa.
Baadhi ya makamanda wastaafu wa Jeshi la Wananchi Tanzania,  walioongoza Vita ya Kagera,  wameisoma makala yangu ya juma lililopita na kutoa mitazamo yao. Mmoja wa makamanda hao wastaafu aliyejitambulisha kuwa alikuwa akiongoza kikosi cha uhandisi cha utegaji na uteguaji wa mabomu, amenieleza kama ifuatavyo.
Kamanda huyo anasema kwamba jukumu la uandishi ni kuelewesha, kukumbusha, ikiwa ni njia ya kuelimisha. Anasema uandishi wa Tanzania juu ya Vita ya Kagera ulimsamehe Gaddafi na kujikita zaidi kwa Idd Amin na hivyo kuwafanya Watanzania wamuone Amin ndiye mbaya wao tu wakiwa wameyaacha pembeni madhara ya Gaddafi ambaye kwa kiasi kikubwa ndiye aliyemuwezesha Amin kutufanyia jeuri hiyo.
Kamanda huyo anasema kwamba tathimin iliyokuwa imefanywa na wataalamu wa JWTZ baada ya Amin kuivamia nchi yetu ilikuwa ni ya kumtandika Amin na kumsambaratisha kabisa ndani ya kipindi cha mwezi mmoja na nusu na miezi miwili bila kujali zana za kivita alizokuwa amejidhatiti  nazo zilizozizidi tulizokuwa nazo sisi. Lakini kujiingiza kwa Gaddafi katika vita hiyo kulitugarimu miezi minane mpaka kutangaza ushindi kamili na miezi mingine mine kusafisha kabisa mabaki ya Amin.
Ni kwamba uchumi wa nchi yetu ulipata majeraha yaliyosababishwa na ubabe wa Gaddafi wa kuingilia vita hiyo ambayo bila yeye tungeweza kuimaliza kama tulivyopanga bila kuathiri sana uchumi wetu. Lakini sasa Gaddafi kautia kilema uchumi wetu maana tokea wakati huo umeshindwa kutengamaa tena.
Jambo la kujiuliza ni kwamba uzuri wa Gaddafi ambao umetajwa kwa nyakati tofauti na viongozi wetu wa kitaifa wakiwemo Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe, unatokana na nini hasa kwetu Watanzania?
Ina maana Watanzania waliouawa Kagera na Amin akiwezeshwa na Gaddafi walikuwa wametolewa kafara? Na je, vijana wa Kitanzania, wapiganaji, waliokuwa wanapigana kuikomboa nchi yao mara wakalipuliwa kwa kuviziwa na askari mamuluki wa Gaddafi nao walitolewa kafara?
Kuna ushuhuda kwamba baadhi ya askari wetu wa kikosi cha kutega na kutegua mabomu, wakiwa wamepanda gari lililokuwa limesheheni milipuko walitegeshewa bomu na majeshi mamuluki ya Gaddafi lililolilipua gari hilo la vijana wetu kiasi cha gari lenyewe na waliokuwemo kuyeyuka kabisa na kutoonekana tena!
Baadhi ya askari wetu waliopoteza maisha katika shambulio hilo lililofanywa na majeshi ya Gaddafi, kwa mujibu wa mashuhuda wa JWTZ ni hawa wafuatao. 1. SSGT Brighton Lububula (alikuwa kaoa), 2. PTE Salum Ngwangwa (kapera), 3. PTE Mathayo Mamboleo (alikuwa kaoa), 4. PTE Bahati Mashimi (kapera), 5. SGT Weston Chikwera (alikuwa kaoa), 6. SGT Filbert Ndunguru (alikuwa kaoa), 7. SGT John Banda (alikuwa kaoa), 8. CPL Aureus Kawonga (alikuwa kaoa), 9. CPL Jacob Mbepera (alikuwa kaoa) na 10. PTE Salum Seif (alikuwa kaoa).
Familia za mashujaa hao zinajisikiaje kwa wakati huu zinaposikia mtu aliyesababisha kutoweka kwa wapendwa wao hao akisifiwa na viongozi wetu kuwa alikuwa mtu mzuri wakati kalaaniwa hata  nchini kwake? Nadhani ipo haja ya viongozi wetu waliotoa kauli za kumsifia Gaddafi kuwaomba radhi Watanzania hususan familia za hao waliopoteza wapendwa wao kusudi dhana ya kuwaenzi hao mashujaa wetu ibaki salama mahali pake.
Hatuwezi kudai kwamba tunawaenzi mashujaa wetu huku upande wa pili tukikisifia kile walichopoteza maisha wakipambana nacho hao mashujaa wetu, kwa maana ya kuenzi huku na huku.
Kuna wenye maoni ya kwamba ingefaa uwepo mdahalo hai wa kuyapima mazuri na mabaya ya Gaddafi kwa Watanzania kama njia ya kuipima thamani yetu kifikira na kimtazamo. Hatuwezi kuishusha thamani yetu kwa kurubuniwa na vitu vidogo kama “lambalamba”.
Ndiyo maana hata Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, aliwarudisha kwao askari wote mamuluki wa Gaddafi, waliotekwa kwenye vita ya Kagera, bila masharti yoyote wakati Gaddafi alikuwa tayari kutoa mabilioni ya shilingi kwa kila mmoja wao. Nyerere hakuwa mtu wa kurubuniwa na lambalamba, ingebidi tumuenzi kwa vitendo katika hilo.
Nimalizie kwa kusema kwamba, kwa uzuzu wetu tunayalaani mataifa ya Magharibi kwamba ndiyo yaliyosababisha kuangushwa kwa utawala wa Gaddafi na hatimaye kifo chake tukiwa tumesahau kwamba hata yeye Gaddafi, kwa jeuri ya pesa ya mafuta, alikuwa akishindana na hayo mataifa ya Magharibi kiubeberu. Mifano ya ubeberu wa Gaddafi ni kama hiyo ya kumsaidia Amin kuivamia na kuiteka ardhi ya nchi yetu ikiwa ni pamoja na kuua maefu ya Watanzania bila kosa lolote, kuvifadhiri vikundi vya kigaidi bila sababu yoyote ya msingi ila tu kuonyesha umwamba na jeuri ya pesa nakadhalika. Kwahiyo tunapoyalaani mataifa ya Magharibi kwa ubeberu tusisahau kwamba hata Gaddafi alikuwa mwenzao.
Swali la mwisho tujiulize, iwapo ubeberu wa Gaddafi alioufanya kwa Tanzania wa kumwezesha Amin kuivamia nchi yetu ungefanikiwa kuiangusha serikali ya Nyerere, je, Gaddafi angekuwa hajafanya kama kile kilichofanywa na NATO kwa utawala wake? Je, hapo kuna tofauti gani kati ya NATO na Gaddafi? Kinachoonekana ni kuzidiana uwezo lakini malengo ya Gaddafi naNATO yalikuwa ni yaleyale mamoja.
0784 989 512
Next Post Previous Post
Bukobawadau