Bukobawadau

WAPENI WATU TAARIFA WAJIANDAE NA KESHO YAO



Juhudi za uwekezaji nchini zimekuwa zikikumbana na upinzani mkali kutoka kwa wananchi kila mahala  kunapokuwako na mradi mkubwa wa uwekezaji, na ni ajabu kwangu na ninaamini kwa wengi wenye kutafakari mambo, kwamba hata sasa serikali imeshindwa kulimaliza tatizo hili
Migogoro mingi iliyojitokeza na ambayo kusema kweli si kwamba imemalizika kabisa kati ya wawekezaji na wananchi kwenye maeneo ya migodi ya madini, ilipaswa kuwa somo kwa watu makini kujiuliza ni nini kinaweza kufanyika kumaliza kabisa migogoro hii lakini hali ni tofauti.
Nadhani ni kwasababu ya tabia iliyojijenga miongoni mwa watanzania ya kulifanya kila jambo kuwa ni matokeo ya mbinu ovu za kisiasa na hivyo kila wananchi wanapopinga miradi ya uwekezaji, serikali ama baadhi ya watendaji wake wanakimbilia tu kudai kwamba ni hujuma za wapinzani wa kisiasa katika kuwachochea wananchi.
Mchezo huu ni hatari na unapaswa kukoma. Ndiyo, unapaswa kukoma kama kweli tunakusudia  kweli kuona maendeleo ya kweli. Ninazo sababu kadhaa za kuwataka wenye mtizamo hasi kwamba kila linapojitokeza tatizo badala ya kutafuta chanzo cha tatizo wanakimbilia kulaumu wale wanaodhani ni wabaya wao waache mara moja, na badala yake watumie nguvu hizo za fikra kufikiri, kusikiliza, kuchanganua na kupata njia mbadala ya kumaliza kutokuelewana kati ya wawekezaji na wananchi.
Ni muhimu watendaji wa serikali wakatambua kwamba ile dunia ya watu kuwafuata viongozi kama vipofu imepita na sasa wananchi wanahoji na hata kuwa na njaa ya taarifa za ni nini kinafanyika kwa kutumia rasilimali za nchi yao. Wananchi si wa Tanzania peke yake, bali wakaazi wa dunia wamepoteza imani na watawala na sababu zake ziko nyingi ambazo si hoja yangu ya leo, lakini itoshe tu kusema, wananchi wanataka uwazi katika mambo kadha wa kadha. Yako mambo ambayo wananchi “wa kawaida” kama wajulikanavyo na wanasiasa hayawasumbui na hawana haja ya kuyahoji, lakini mambo yanayogusa maisha yao ya kila siku, watawala ni lazima wakubali kwamba yatahojiwa na mbinu sahihi ya kukabiliana na hili ni kuwa na majibu yenye kushibisha nafsi na yenye mantiki badala ya ama ubabe ama maneno mepesi yasiyo mantiki.
Wote tunakumbuka jinsi ambavyo nguvu zimetumika kukabiliana na wananchi kule kwenye migodi ya Nyamongo na Buhemba na hata Bulyanhulu hali haikuwa shwari sana. Mwaka jana umeshuhudia vurugu kubwa mkoani Mtwara wananchi wakipinga kujengwa bomba la kusaifirsha gesi kutoka Mtwara hadi jijini Daressalaam. Hayo yote na mengine ni matokeo ya watendaji wa serikali ama kwa makusudi au kwa uzembe ama ujinga (nimetumia neon ujinga si upumbavu) wa kutambua kwamba huu ni ulimwengu wa taarifa zaidi kuliko ulivyokuwa ulimwengu uliopita ambapo wananchi waliwafuata viongozi wao bila kuhoji.
Nasema siungi mkono vurugu  na machafuko katika kutafuta taarifa sahihi, lakini nakubali ukweli kwamba ni hulka ya binadamu kwamba ikiwa atahitaji kitu Fulani na hawezi kukipata kwa njia ya kawaida, unategemea matumizi ya nguvu katika kufikia lengo hilo, na hivyo naona kama ni sahihi kwa serikali badala ya kusubiri hadi migogoro imekuwa mikubwa, iwape wananchi taarifa sahihi kwa wakati ili wananchi nao waweze kujiandaa kwa mabadiliko yatakayojitokeza kwenye maeneo yao kutokana na shughuli ama uwekezaji husika na jinsi ya kuziona na kuzitumia fursa zinazopatikana.
Ukiitazama Tanzania ya gesi na mafuta, utagundua kwamba haina tofauti na Tanzania ya dhahabu na Almasi katika utekelezaji wa miradi yake. Wakati katika Dhahabu na Almasi Tanzania ilipokea na kuajiri wageni wengi sana katika miradi karibia yote na kisingizio kikiwa ni kutokuwapo kwa wataalamu wanaofikia viwango vitakiwavyo katika tasnia husika, tatizo ni lilelile leo kwenye gesi na mafuta.
Ukweli na usemwe, kama taifa tunazo changamoto mbili kubwa zinazofanya suala la kutokuwapo na nguvu kazi stahiki kwa kazi husika iwe ukweli usiopingika. Moja ni ukweli kwamba asilimia kubwa ya rasilimali watu wa Tanzania ni watu wasiopenda kazi bali maslahi yatokanayo na kazi tu ama kwa lugha nyingine uvivu. Hili aliwahi kulisema Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa Samweli Sitta na wajuvi wakamzodoa, lakini mioyoni tunajua kwamba alisema ukweli. Utendaji wetu wa kazi ni mbovu, wa kivivu na unaohitaji kusukumwa mara zote. Watanzania wanaishi kama watu walio na uchumi mkubwa kabisa Afrika ilhali ni maskini wa kutupwa. Nimewahi kusikia mara kadhaa vijana wasomi wakikataa kufanya kazi kwenye mabenki si kwa sababu ya malipo ama mazingira ya kazi, bali kwamba ni kazi zinazochosha na kwamba muda wa kutoka kazini kwa wafanyakazi wa mabenki hauwapi uhuru wa kujichanganya na watu na “kusoshalaizi”, huu ni uvivu wa kufikiri. Hasa kwa kijana ambaye ndiyo kwanza ametoka chuo na hana uzoefu wowote wa kazi. Wakati katika nchi za wenzetu watu wanajitolea kufanya kazi pasipo malipo, vijana wa kitanzania wanatoka chuo na wanapopata kazi wanauliza kwanza, “mshahara shilingi ngapi”?.
Nieleweke sina ugomvi na maslahi mazuri mahala pa kazi, lakini ninajaribu kuonyesha mtizamo wa vijana walio wengi kuhusu kazi. Jambo la pili ni kwamba vijana wa Tanzania hawajaandaliwa vyema kuchukua majukumu yao katika sekta zenye uwekezaji. Jambo hili limefanya kwamba mara zote tunapokwenda kwenye uwekezaji wowote mkubwa, kilio chetu ni kile kile kwamba hatuna wataalamu wa Nyanja husika na mimi najiuliza, hivi serikali haikujua kwamba muda na wakati Fulani kutakuwa na uwekezaji Fulani na hivyo tuwaandae wananchi kwa kuwapa mafunzo na utayari kwa ajiri hiyo?.

Sitaki kuamini kwamba serikali ama inakuwa na haraka ya kufanya uwekezaji kila utafiti unapokamilika na maliasili kugunduliwa ama haina taarifa za ni wapi katika nchi yetu kuna maliasili gani na ambazo uwekezaji wake unaweza kuwanufaisha wananchi kwa ajira na kadhalika.
Ikiwa basi kwamba serikali haijui ni maliasili gani tunayo na ni lini tunaweza kuanza kuitumia kuinua uchumi wan chi yetu, ni kwanini kila baada ya utafiti, hatufungi milango na kuwekeza kwanza kwenye kufundisha watu wetu hadi tumekuwa na wataalamu katika Nyanja kadha wa kadha kabla ya kuanza uwekezaji wenyewe!?. Ni kwanini leo tuna wafanyakazi wengi wa kigeni kwenye miradi ya utafiti na uchimbaji wa gesi na mafuta kama tulivyokuwa kwenye dhahabu!? Je! Ni kweli kwamba hatujajifunza chochote kwenye dhahabu!?.
Huu ni uzembe wetu wa kufikiri na kupanga mikakakati endelevu ya jinsi ya kuboresha maisha ya wananchi. Hiki kimekuwa chanzo cha sheria zetu wenyewe kuhusu ajira hasa katika uwekezaji kukanyagwa chini ya nyayo za wawekezaji huku tukitazama tu na mara nyingine kutumia maguvu kuzima malalamiko ya watu wetu, huu ni ukorofi.
Ukiingia kisiwani Mafia kwenye mkoa wa Pwani kwa mfano, kitu cha kwanza utakachogundua ni ujenzi wa uwanja mkubwa na wa kisasa wa ndege kisiwani humo. Hili ni jambo jema, lakini ujenzi huu unaendana na utafiti kabambe wa gesi na mafuta kwenye kijiji cha Ndagoni kisiwani humo.
Mambo mawili yananijia akilini ninapolitazama hili katika muktadha mzima wa uwekezaji na maslahi yake mapana kwa watu wetu. Moja ni ukweli kwamba kiwanja hiki kinajengwa “kwa msaada wa watu wa Marekani”. Hakuna asiyefahamu kwamba Marekani haiwekezi pesa zake ati kwa upendo tu wa watu wa sehemu husika, bali kwa maslahi mapana ya taifa hilo yatokanayo na sehemu hiyo. Nieleweke tena, sina ugomvi na ujenzi wa uwanja, wala suala la Marekani kama taifa kuwa na maslahi labda katika gesi, mafuta ama utalii wa kisiwa hiki, lakini hoja yangu ni kwamba ukiwauliza wananchi wa eneo hili, utagundua kwamba hakuna mwenye taarifa za utafiti huu uko kwenye hatua gani na matarajio ni nini. Si ajabu wakati uwekezaji utakapoanza, wananchi watatakiwa “kulipwa fidia” ya maeneo yao na kupisha uwekezaji kwa kisingizio cha maslahi mapana bila kuandaliwa kuwa wahsiriki halisi wa rasilimali iliyogunduliwa kwenye eneo lao, na ole wa wale watakahoji haya ninayojihoji mimi leo kwenye makala haya wakati huo.
Swali gumu ni, serikali inaona ugumu gani kuwa wazi kwa wananchi wake na kuanza kuandaa mipango madhubuti ya kufungua vyuo vya ufundi kwenye kisiwa hiki, kuomba wale wenye uzoefu na utaalamu katika aina za taaluma za kifundi zitakiwazo kwenye gesi na mafuta hata kutoka kwa wanaokusudiwa kuwa wawekezaji wakubwa, kuja na kufundisha vijana wetu ili wakati utakapofika tuwe tayari na wataalamu?. Ni nini kinaifanya serikali haishirikishi wananchi kwenye taarifa za utafiti, mipango na malengo ya uwekezaji huu ili nao wajiandae kupeleka vijana wao shule kusomea mambo kadhaa wakijua kwamba soko la ajira litapatikana hapa?
Kwanini mipango ya makusudi kuboresha kilimo cha vyakula, matunda na mbogamboga zitakazohitajika kwa wingi wakati huo kwa kujua na kuwajulisha wananchi viwango vya ubora vitakiwavyo ili wajifunze na kulima kibiashara kwa ajiri ya wkati huo? Je! Ni kweli  kwamba unataka kurudia makosa yaleyale yaliyofanyika migodini ambapo hata machungwa yalikuwa yakiagizwa kutoka Afrika Kusini kwa kisingizio cha ya hapa kwetu kukosa viwango stahiki!? Kwani sisi tuna kasoro gani kwenye ardhi yetu inayotufanya tusizalishe kwa viwango vitakiwavyo?
Nadhani ni wakati watendaji wa serikali na watunga sera waamue kwa makusudi kulisaidia taifa hili kufaidika na uwekezaji vinginevyo tuendelee hivi hivi hadi tutakaposhtuka mali zimekwisha na hawa waitwao wawekezaji hawatuhitaji tena, huku tukiwa hatuna faida hata moja iliyopatikana kwa miradi hiyo kwa wananchi wetu. Tunakumbuka wote jinsi Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alivyokataa kuruhusu uwekezaji hadi pale watanzania watakapokuwa “wameelimika” na kuwa tayari. Najiuliza kila nionapo yanayoendelea leo, ikiwa wakati watawala wetu walipoamua kufungua milango ya uwekezaji, walipima na kujiridhisha juu ya kiwango cha utayari wa watanzania sisi kukabili changamoto za uwekezaji ama wanasubiri kuvuta shuka kunakucha?.
Salaam nawasalimia.
Mwandishi: G. Jonathan Kamenge
Next Post Previous Post
Bukobawadau