Bukobawadau

KIKAO CHA KAZI RC NA WATENDAJI MULEBA LEO

MAANA HALISI YA MAABARA TATU ZILIZOKAMILIKA KILA SHULE MKOANI KAGERA YAONGEZA UCHAKARIKAJI WA WATENDAJI KUZIKAMILISHA KABLA YA DESEMBA 5, 2014

Mkuu wa Mkoa wa Kagera abadili upepo wa maana halisi ya maabara tatu  zilizokamilika mkoani hapa kuwa ni zile zenye miundombinu yote inayotakiwa kuwemo katika kila chumba kwenye vyumba vitatu  kama  mifumo ya gesi na maji pia samani  isipokuwa vifaa tu ambapo alibadili mtazamo wa watendaji walio wengi kuwa maabara iliyokamilika ni maboma ya vyumba vitatu tu.
Upepo wa maana halisi ya maabara iliyokamilika ulibadilika baada ya Mkuu wa Mkoa wa Kagera John Mongella  kuitisha kikaokazi cha watendaji wakuu wa serikali katika mkoa wa Kagera ili kujadili na kutoa taarifa ya ujenzi wa maabara  na kuweka mikakati jinsi ya kukamilisha maabara hizo ifikapo Desemba 5, 2014.
Katika kikao hicho kilichofanyika Wilayani Muleba tarehe 17/11/2014 Mkuu wa Mkoa aliwaonya watendaji hao wakuu waserikali katika ngazi za Halmashauri za wilaya kuhakikisha maabara zinakamilishwa na miundombinu yake na siyo kujenga maboma tu alafu kujiridhisha kuwa tayari maabara zimekamilika.
Mhe. Mongella aliagiza kuwa  rikizo zote na safari za  Wakurugenzi wa Halmashauri na Wakuu wa Idara kusitishwa mara moja ili kuhakikisha ujenzi wa maabara unakamilika ambapo alitoa tarehe ya mwisho ya kumkabidhiwa maabara zote kuwa ni tarehe  5/12/2014 mkoa mzima na hatopenda mzaha wala maelezo bali kukabidhiwa maabara tu.
 Akifafanunua ufanisi wa ujenzi wa maabara Mkuu wa mkoa John Mongella alisema kuwa ujenzi hautegemei mtu mmoja mfano Mkuu wa Wilaya au Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri  bali inatakiwa  kushirikiana kwa pamoja  kama mfumo wa utawala ulivyo kuanzia ngazi za juu mpaka chini kila mmoja anahusika moja kwa moja katika suala hilo la maendeleo.
Hadi sasa Mkoa wa Kagera unahitaji jumla ya maabara 570 zilizokamilika ili kutumiwa na wanafunzi wa elimu ya sekondari hasa katika  shule za kata ambazo hapo awali hazikuwa na maabara hata moja lakini ujenzi umefikia asilimia 31.8 ambapo bado kuna kazi kubwa ya kufanya ili kufikia asilimia 100.
 Maagizo: Katika kikao hicho Mkuu wa Mkoa wa Kagera alitoa maagizo makuu manne kwa watendaji ili wayafanyie kazi mara moja bila mzaa katika kusukuma maendeleo ya wananchi mbele .


 Kwanza, Wakurugenzi  Watendaji wa Halmashauri za Wilaya wakishirikiana na Madiwani kuhakikisha wanabadili vipaumbele vya maendeleo na kupeleka fedha zote katika kukamilisha ujenzi wa maabara, aidha  makusanyo yote ya vyanzo vya ndani yaelekezwe katika kukamilisha vyumba vya maabara kila wilaya.
 Pili, Kuimarisha na kuthibiti ukusanyaji wa mapato ya ndani ambayo ndiyo uti wa mgongo katika kutekeleza miradi ya maendeleo ya wananchi na uendeshaji wa Mamlaka za Serikali za Mitaa. Mkuu wa Mkoa alisema kuwa Halmashauri za Wilaya zinatakiwa kusimamia ipasavyo mapato ya ndani ili kuacha utegemezi unaosababisha miradi mingi ya maendeleo kukwama.
Tatu, Taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za serikali katika Halmashauri za Wilaya, Mkuu wa mkoa aligiza kila Halmashauri kuhakikisha inapata hati safi na hatovumilia mtendaji yeyote atakayesababisha hoja bali atakula naye sahani moja.
Nne, Ulinzi na Usalaama, Halmashauri za wilaya ziliagizwa kutenga bajeti ya kununualia sare za mgambo (Jeshi la Akiba) wakati wanapohitimu mafunzo yao. Aidha mkuu wa mkoa alisema atahakikisha mfumo wa utawala unafanya kazi katika kupambana na wahamiaji haramu, wavamizi wa mapori ya hifadhi na uharibifu wa misitu.
 Kikao kazi hicho cha Mkuu wa mkoa na watendaji wa serikali kilihudhuriwa na Wakuu  wa Wilaya, Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri na Manispaa, Wenyeviti wa Halmashauri,Wahandisi, Maafisa Elimu wa Wilaya, Maafisa Mipango wa Halmashauri  pia na Watendaji waandamizi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wakiongozwa na Katibu Tawala mkoa Bw. Nassor Mnambila

Na: Sylvester Raphael
Next Post Previous Post
Bukobawadau