Bukobawadau

HADITHI YA KUSISIMUA:MKE WANGU NUSU JINI,NUSU MTU!!

“Niliwahi kujiuliza kama iko siku na mimi nitapata nafasi ya kusimulia popote pale mkasa uliowahi kunikumba miaka ya nyuma. Ni kuhusu mke wangu niliyefunga naye ndoa ya serikali. Nilibaini kwamba alikuwa mtu lakini pia alikuwa jini kwa sababu mbalimbali,” anasema Abigaeli, mkazi wa Kibaha, Mkoa wa Pwani.

Anaendelea: “Siku ya kwanza kukutana na mke wangu ilikuwa kwenye kikao cha kupokea mahari ya mtoto wa kaka yangu aliyekuwa anataka kuolewa na Msambaa mmoja kutoka Lushoto, Tanga. Ilikuwa mwaka 2002.

Kuna kitu kilitokea kwenye kikao hicho na kama ningekuwa makini, nisingeingia kwenye matatizo makubwa yaliyowahi kunipata katika maisha yangu.Kitu hicho ni kwamba, baada ya kikao, msichana mrembo ambaye alikuja kuwa mke wangu alinifuata na kuniomba namba zangu za simu, nikamtajia, akaziingiza kwenye simu yake.

Alipoondoka, baadhi ya ndugu tuliokuwa pale tuliulizana yule msichana ni nani. Hakuna aliyekuwa na jibu. Bahati nzuri ndugu mmoja wa upande wa mwanaume aliyeleta mahari alikuwa hajaondoka, tukamuuliza kama walikuja na msichana yule, akakataa kutomtambua tena huku akisisitiza kwamba, walikuja kumi tu na yeye ndiye alibaki kumalizia mambo mengine.

Kaka aliniuliza aliponifuata kuniomba namba ya simu alisema anatokea upande gani katika tukio lile, nikamwambia kwa waleta mahari.Nilianza kuingiwa na wasiwasi tena mkubwa, niliwaza mengi. Kaka akanilaumu kwamba, siku nyingine nisikubali mawasiliano na watu ambao hawajulikani sawasawa. Lakini nilijitetea kwamba, mtu kusema kaja na watu wengine ambao kweli walikuwepo sidhani kama unaweza kumtilia shaka.

Wiki moja baada ya tukio hilo la kushangaza, nilipigiwa simu na mtu aliyedai kuwa yeye ndiye yule msichana, akasema anaitwa Munil. Alisema amenipigia simu ili kunijulisha kwamba, yule mchumba aliyekuja kutoa mahari kwa kaka amefariki dunia kwa ajali mbaya ya gari iliyotokea nusu saa iliyopita.
Nilishtuka sana kwani zilikuwa taarifa za ghafla sana kwangu.

Lakini jambo lingine sasa, niliamini yule msichana ni ndugu na wale walioleta mahari ila pengine yule mtu wa mwisho hakumjua.Nilimshukuru kwa taarifa kisha akakata simu. Nikampigia kaka kumuuliza kama analijua hilo, naye alishtuka sana akasema hajasikia, akaomba nimpe dakika tano tu ahakikishe kwa ndugu wengine halafu atanirudia. Lakini kaka hakuniuliza nilikozitoa habari zile.

Je, nini kiliendelea hapo? Usikose kusoma kesho usiku..........
Next Post Previous Post
Bukobawadau