Bukobawadau

WILAYANI KYERWA NA UTATU MTAKA FUJO!!

Picha kutoka maktaba yetu.
NA PRUDENCE KARUGENDO
KYERWA  ni wilaya mpya iliyoundwa kutoka katika wilaya ya Karagwe mkoani Kagera. Wilaya hiyo iko mpakani mwa Tanzania na nchi mbili za Uganda, upande wa Kaskazini na Rwanda kwa upande wa Magharibi, Kaskazini Magharibi mwa Tanzania.
Wananchi wa wilaya hiyo kisiasa kwa sasa wanaimba wimbo wa majuto ni mjukuu. Hiyo ni baada ya kukabiliana na hali ambayo hawakuitegemea, walidhani kutengewa wilaya ya kwao wakiwa wametolewa kwenye wilaya ya Karagwe,  kungewapatia faraja ambayo wangeitumia kuboresha ustawi wao. Lakini badala yake wanasema wameingizwa kwenye matatizo ambayo hawakuwahi kuyashuhudia tangu nchi yao iwe huru zaidi ya miaka 53 iliyopita.
Wengine wamediriki kusema kwamba hali ilivyo kwa wakati huu kule Kyerwa haikuwahi kuwa hivyo hata wakati wa wakoloni. Watu wameyakimbia makazi yao na kuhamia maporini ili kujinusuru na mashambulizi ya vyombo vya dola yanayofanyika kwa maelekezo ya viongozi wa wilaya hiyo waliochukizwa na maamuzi halali ya wananchi wakati wa uchaguzi wa serikali za mitaa.
Wana Kyerwa wanasema kwamba uchaguzi wa serikali za mitaa upo kwa mujibu wa Katiba ya nchi yetu, na kwamba uchaguzi huo umefanyika kwa kuvihusisha vyama vingi vya siasa ambavyo navyo vipo kwa mujibu wa Katiba ya nchi. Kwamba katika uchaguzi wa aina hiyo wao wana haki ya kumchagua mtu kutoka katika chama chochote ambaye wanamuona anawafaa. Hakuna sheria inayoamuru kwamba achaguliwe tu wa chama fulani, kiwe chama tawala au cha upinzani. Eti kama sheria ingesema hivyo wala kusingekuwepo na haja ya kuhangaika na uchaguzi.
Lakini wananchi hao wanashangaa kuona viongozi wa serikali wanawachukulia kama watu wahalifu kutokana na maamuzi waliyoyafanya ya kuamua wamchague nani na wamuache nani, kana kwamba maamuzi yao hayo yamevunja sheria au Katiba ya nchi.
Wanasema kwamba katika maeneo mbalimbali ya wilaya hiyo matokeo ya kura zilizopigwa yalitangazwa chini ya mtutu wa bunduki na mengi yakiwa yamegeuzwa kimabavu kwa kuwatangaza walioshindwa kuwa ndio wameshinda. Waliojaribu kuyahoji matokeo hayo ya kughushi walichukuliwa kwamba wanafanya fujo na hivyo kushambuliwa na vyombo vya dola huku wengine wakikamatwa na kuwekwa ndani kwa visingizio mbalimbali. Zaidi ya vijana 50 waliwekwa ndani.
Katika hali hiyo wananchi wa Kyerwa, bila kujali tofauti zao kiitikadi, wamelalamika sana wakisema kwamba kwa mtindo huo uongozi wa wilaya hiyo umeshindwa kabisa kuiongoza na hivyo kuviachia vyombo vya dola kuitawala kwa mabavu dhidi ya matakwa ya wananchi.
Sababu wanasema kwamba kuongoza ni pamoja na kuwashawishi wananchi ili wakikubali na kukiamini wanachoelezwa kuwa ni cha kweli. Lakini kiongozi anayeshindwa kufanya hivyo wananchi wanaachana naye na kumchukua yule anayeweza kuwashawishi wakamuamini. Ila walio madarakani hawataki kukiri kuwa wameshindwa kuwashawishi wananchi, ndipo wanapotumia ushawishi walio nao kwa vyombo vya dola kuanza kuwashambulia wananchi kama njia ya kulipiza kisasi kutokana na kukataliwa kwao!
Eti viongozi hao wa mabavu, walio chini ya chama tawala, wanachotaka kieleweke kwa wakubwa wao kitaifa ni kwamba wamefanikiwa kuwafanya wananchi wawakubali viongozi waliogombea kupitia chama tawala wakati sio kweli.
Jambo hilo limewafanya hata wale waliokuwa wanakipenda chama tawala waanze kufikiria vinginevyo, sababu wanasema kwamba tofauti za kiitikadi sio uhasama. Wapo watu wanaotofautiana kiitikadi lakini bado ni ndugu na marafiki. Hakuna mwana CCM aliye na ndugu mwana Chadema, kwa mfano, anayependa kumuona ndugu yake akilala porini kuwakwepa polisi wasije kumkamata kutokana na kutompigia kura mtu wa CCM.
Suala hilo ndilo limeifanya CCM kuanguka chali katika maeneo mengi ya vijijini tofauti na kawaida ya miaka nendarudi, na kinyume cha imani ya chama hicho kabla ya uchaguzi wa serikali za mitaa wa mwaka jana.
Kwa ufupi wananchi hao wa Kyerwa wanasema kwamba vyama vingi vya siasa havikuja kuwatenganisha wananchi na kuwavunjia undugu au urafiki. Wanasema hayo yote yanatokana na tatizo la kutokubali kushindwa kunakotokana na kutoiheshimu demokrasia ya vyama vingi vya siasa wala kuelewa maana yake. Wanaongeza kwamba tatizo hilo limo sana kwenye chama tawala ambacho kinawakumbatia sana watu wenye uwezo mdogo kiushawishi.
Aidha,  wamesema ni aibu sana kwa wakati huu, baada ya miaka 54 ya uhuru wa nchi, chama tawala kinakosa watu wenye kujenga ushawishi ili wananchi wakikubali chama hicho,  na badala yake kinaegemea kwenye mabavu na vitisho vya vyombo vya dola. Wanakumbusha jinsi Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, alivyokuwa na uwezo mkubwa wa kujenga hoja na kushawishi tangu kwenye harakati za kudai uhuru wa nchi hii.
Kwamba uwezo huo wa Nyerere ulimfanya asifikirie hata mara moja kutumia mabavu ya kivita kuudai uhuru. Eti baada ya miaka 53 ya uhuru makada wa chama tawala ndipo wanafikiria mabavu ya kivita baada ya kushindwa kuwashawishi wananchi!
Kitu wanachokionyesha wananchi hao wa Kyerwa kuwa ndilo tatizo kuu linalowavurugia usalama wao ni kile wanachokiita “utatu mpenda fujo”. Wanasema utatu huo unaundwa na mbunge wa wilaya hiyo, Eustace Katagira, MNEC wa CCM wa wilaya hiyo, Daniel Damian na Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya hiyo, Kashunju Runyogote.
Wananchi wa Kyerwa wanasema kwa nguvu zote kwamba fujo zinazofanywa na utatu huo, hata kama zinafanywa zionekane ni za kukihami chama tawala, eti hazina uhusiano hata kidogo na chama hicho. Eti hizo ni fujo binafsi zilizolenga kwenye maslahi binafsi ya watu wanaounda utatu huo. Kwamba kwa hapo utatu huo unakitumia chama tawala kama kinga ya mambo yao binafsi wanayoyafanya bila chama hicho kuwa na habari nayo.
Fujo za utatu huo ndizo zinazowafanya hata walio wana CCM katika wilaya ya Kyerwa kuanza kujiuliza kwa nini chama chao kisizimulike fujo hizo? Sababu eti hazionyeshi uhusiano wowote na chama chao wala kuonyesha kama wahusika wanayafanya hayo kwa mapenzi ya chama chao, sababu eti wanayoyajua wao kwamba ndicho chanzo cha fujo hizo hayana manufaa yoyote kwa chama hicho.
Wananchi hao wanaeleza kwamba katika utatu huo wa fujo kuna biashara ya ulanguzi wa kahawa ambayo haitakiwi ifanywe na mtu mwingine yeyote. Pia eti asilimia kubwa ya ardhi ya wilaya ya Kyerwa imehodhiwa ndani ya utatu huo, eti maeneo mengi makubwa ya ardhi yamefungwa kwa matumizi ya wananchi wengine, bila kujali ni wana CCM au wa vyama vingine, kiasi cha wananchi kukosa mahali pa kufanyia shughuli zao za kawaida, kama kulima mazao ya msimu kama vile karanga, njugumawe, viazi mviringo nakadhalika.
Pia kutokana na tatizo hilo la kuhodhi ardhi, wanachi wanasema wanapata shida ya malisho kwa mifugo yao. Eti hilo ni tatizo lisilokuwa na uhusiano wowote na CCM. Kwamba chama hicho kisingependa kuona hata walio wananchama wake wanapata usumbufu unaolazimishwa na utatu huo wa fujo.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kyerwa, Kashunju Runyogote, anasemwa na wananchi hao kuwa aliwahi kukabiliwa na kashfa ya ubadhirifu wa pesa za halmashauri ya Karagwe, kabla ya kutenganishwa na Kyerwa, kiasi cha chama chake kutuma wakaguzi kuangalia kuna nini kwenye halmashauri hiyo. Inadaiwa alitumia pesa hiyo kwenda kufanya “matanuzi” kutalii nchini Rwanda.
Kwahiyo inapaswa ieleweke kwamba manyanyaso wanayoyapata wananchi kwa visingizio vya kiitikadi na kuwafanya waishi kama wananchi haramu kwenye nchi yao, siyo yote yanafanyika kwa msukumo wa kukipenda chama hicho tawala. Ila wapo wanaotumia jina la chama hicho kufanya mambo yao machafu kwa wananchi,  hata kwa walio wanachama wa chama hicho,  kwa ajili ya maslahi binafsi bila chama hicho tawala kuwa na habari.
Rai yangu ni kwamba CCM inatakiwa kulifanyia kazi suala hilo kabla hali ya mambo haijawa mbaya zaidi kiasi cha kukifanya chama hicho kushindwa kuimiliki.
0784 989 512
Next Post Previous Post
Bukobawadau