Bukobawadau

MKOA WA KAGERA WAZINDUA RASMI USAMBAZAJI WA KATIBA PENDEKEZWA LEO FEBRUARI 20, 2015

Mkoa wa Kagera umefanya uzinduzi wa usambazaji wa Katiba inayopendekezwa leo Ijumaa Februari, 2015 katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa  Kagera na kuwahusisha wadau mbalimbamli kutoka katika Halmashauri  zote za Wilaya wakiwemo na viongozi wa dini, mashirika na taasisi za serikali na zisizokuwa za serikali.
Katika uzinduzi huo Mkuu wa Mkoa wa Kagera  Mhe. John Mongella aliwasistiza viongozi na wadau waliohudhuria katika uzinduzi huo kuwahamasisha wananchi kusoma Katiba pendekezwa na kuielewa ili wakati ukifika waweze kuipigia kura ya ndiyo au hapana bila kupotoshwa.
 Mhe. Mongella aliwaomba wananchi kuilewa Katiba pendekezwa bila kushawishiwa na miemuko ya vyama, dini, watu binafsi kwa mitazamo yao au makundi mbalimbali ili wakati ukifika waweze kutoa maamuzi yao wenyewe katika kupiga kura ya ndiyo au hapana.
Akisistiza kuhusu kupiga kura Mhe. Mongella amewaomba viongozi wa dini Wakuu wa Wilaya, Viongozi wa Taasisi na Mashirika ya serikali na na yasiyokuwa ya serikali  kuhakikisha wanawahamasisha wananchi kujiandikisha katika daftari la wapiga kura ili kupata haki ya kupiga kura ya ndiyo au hapana kwa katiba pendekezwa  na Uchaguzi Mkuu ujao mwezi Oktoba mwaka huu 2015.
Aidha, Mhe. Mongella aliwaomba wadau kuwafikiria kundi la tatu ambalo pengine wao hawataki kusema chochote kuhusu katiba pendekezwa kuwa nao waheshimiwe na kusikilizwa ukiacha makundi  yatakayopita kwa wananchi kuhamasisha wananchi kupiga kura ya ndiyo na kura ya hapana.
Pia alisema kuwa Katiba Pendekezwa  imeweza kuzingatia maoni ya wananchi kwa asilimia 80 na kuwa haiwezekani hata siku moja katiba kuwa au kusema kila kitu anachokihitaji mwananchi mmoja mmoja mfano watoto, wanawake, vijana, wanaume au kusema kila jambo ambalo lipo nchini.
Katika hatua nyingine Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera Bw. Nassor Mnambila alisema kuwa tayari zimesambazwa nakala za Katiba pendekezwa 54,300 katika mkoa wa Kagera kwa mchanganuo ufutao, Halmashauri ya Wilaya Missenyi nakala 6,000 Karagwe nakala 6600, Kyerwa nakala 5400, Manispaa ya Bukoba nakala 4200, Bukoba Vijijini nakala 8700.
Katika Halmashauri ya Wilaya ya Ngara nakala 6000, Muleba nakala 12900, na Biharamulo nakala 4500. Pia katika kikao cha uzinduzi ziligawiwa nakala 132 ambazo zinakamilisha nakala 54,432 jumla katika mkoa wa Kagera. Alisema pia nakala nyingine nyingi zaidi zitawasili hapo baadae ili wananchi walio wengi  waweze kupata nakala hizo na kuzisoma.
Next Post Previous Post
Bukobawadau