Bukobawadau

VIGOGO WALIOSAFISHWA IKULU:WABUNGE WAJIWEKA PEMBENI


Dar es Salaam. Siku moja baada ya Ikulu kutangaza kuwasafisha mawaziri watano na Katibu Mkuu, Eliackim Maswi, wabunge wamejiweka pembeni na suala hilo wakisema Bunge lilishatimiza wajibu wake.

Juzi, Ikulu iliwasafisha mawaziri wanne walioshinikizwa kuachia ngazi na Bunge kutokana na kuhusishwa na sakata la Operesheni Tokomeza Ujangili na mmoja aliyejiuzulu kutokana na kashfa ya uchotwaji wa Sh306 bilioni kutoka Akaunti ya Tegeta Escrow, pamoja na katibu mkuu wa wizara.

Waliotangazwa na Ikulu kuwa safi ni Emmanuel Nchimbi, aliyekuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa na Shamsi Vuai Nahodha, aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani. Wawili hao wanatajwa kwenye kinyang’anyiro cha urais kwa tiketi ya CCM ingawa hawajatangaza nia.

Wengine ni aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Hamis Kagasheki na aliyekuwa Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, David Mathayo.

Hali kadhalika, Profesa Sopster Muhongo aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini ambaye alijiuzulu kutokana na kashfa ya escrow, pamoja na katibu mkuu wa wizara hiyo, Eliackim Maswi aliyesimamishwa kutokana na sakata hilo, wametangazwa kuwa safi.

Akizungumzia hatua hiyo, Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii, Mchungaji Peter Msigwa alisema kitendo cha Serikali kutangaza kuwa mawaziri hao hawakuhusika katika kutekeleza makosa yaliyotokana na Operesheni Tokomeza, kinaonyesha nia ya kuendeleza tabia ya viongozi kutopenda matatizo yaliyotokea wakiwa madarakani.

“Kilichofanyika ni kuionyesha dunia kuwa hakuna kuwajibika, unapopewa jukumu lazima uwajibike. Sijui Taifa hili linakwenda wapi? Nakosa hata maneno ya kuzungumza,” alisema Msigwa.

Msigwa, ambaye ni Waziri Kivuli wa Maliasili na Utalii ambayo ni moja ya wizara nne zilizohusika kwenye operesheni hiyo, alikuwa miongoni mwa wabunge waliokuwa mstari wa mbele kuchangia wakati Bunge likijadili ripoti ya kamati iliyochunguza suala hilo na kubaini ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu wakati wa utekelezaji wa Operesheni Tokomeza.

Mbunge wa viti maalumu (CCM), Esther Bulaya alisema kuwa katika taarifa hakuna kipya kwani haina tofauti na ile ya Kamati ya Bunge iliyoundwa kuchunguza suala hilo.

“Ukifuatilia kwa makini taarifa hiyo, utabaini ndiyo yaleyale yaliyokuwa yakijadiliwa bungeni na wabunge nikiwamo mimi,” alisema Bulaya.

“Jana (juzi) nilimsikiliza kwa makini sana (Katibu Mkuu Kiongozi) Balozi Sefue wakati akitoa taarifa hiyo kwa waandishi wa habari ila kichwani lilinijia swali moja tu; hivi madai yaliyotolewa na wananchi katika tume iliyoundwa kuchunguza jambo hili ya kweli au si kweli?” alihoji Bulaya.

“ Lakini Sefue mwenyewe amekiri kwamba madai yaliyotolewa na wananchi mengine yalikuwa yana ukweli ndani yake.”
Aliongeza kuwa binafsi hayupo tayari kuzungumza habari za mawaziri, kwani hajui utafiti au uchunguzi wao walipoufanya ila anachoweza kusema Bunge limefanya kazi yake ipasavyo bila kumpendelea au kuumumiza mtu yoyote.

Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola, ambaye hakuwa amepata habari hizo hadi jana alipoambiwa, aliungana na Bulaya kuwa Bunge lilitekeleza wajibu wake.

“Huko hatuhusika nako kwani huo ni mhimili mwingine,” alisema Lugola.

Mbunge wa Simanjiro, Christopher Ole Sendeka, ambaye anaongoza jimbo lenye wafugaji wengi, alidai kuwa taarifa hiyo haina jipya kwani ina mambo yaleyale yaliyojadiliwa na wabunge wakati ripoti ikiwasilishwa bungeni na kwamba kujiuzulu kwa mawaziri ilikuwa ni kisiasa na hakuna aliyeonewa.

“Sisi wabunge hatukusema Waziri Kagasheki kaua mtu, bali watendaji wake ndiyo walikuwa wazembe kwa kutokuwa makini na kazi zao,” alisema Ole Sendeka.

“Sisi wabunge na Bunge tumefanya kazi na hata wao wenyewe wamekiri katika ripoti yao na wamesema kama sisi tulivyoitoa,” alisema Ole Sendeka.

John Shibuda, mbunge wa Maswa Magharibi, alihoji kama kuwajibika ni kukubali kufanya kosa.

“Kwani (Rais wa Awamu ya Pili) Mzee Ali Hassan Mwinyi alipowajibika alikuwa ameua? Nipo njiani ninakwenda kwenye mkutano wa wafugaji kutoka kanda ya ziwa. Nitawasikiliza wana maoni gani kuhusu jambo hilo halafu nitakwambia,” alisema.

Uamuzi wa Ikulu kuwaondolea doa hilo mawaziri hao wanne umetokana na ripoti ya Tume iliyoundwa na Rais Jakaya Kikwete kuchunguza tuhuma za ukiukwaji wa haki za binadamu wakati wa utekelezaji wa operesheni hiyo iliyolenga kuondoa ujangili kwenye hifadhi za Taifa, lakini ikaishia kuua wananchi, kutesa na kupora mali zao.

Pia, Profesa Muhongo na Maswi wamesafishwa baada ya Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma kufanya uchunguzi na kubaini kuwa hawakuhusika kuchota fedha kutoka akaunti hiyo ya escrow wala kupewa rushwa na kwamba Maswi aliagiza fedha hizo zitolewe kwenye akaunti hiyo iliyokuwa Benki Kuu kwa kufuata ushauri wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Fredrick Werema, ambaye pia alijiuzulu kutokana na kashfa hiyo.

Balozi Sefue aliwaambia wanahabari kuwa tume iliyoundwa na Rais Kikwete ilijiridhisha kuwa mawaziri hao waliwajibika kisiasa na hawakuhusika moja kwa moja na vitendo hivyo na hakuna hatua inayostahili kuchukuliwa dhidi yao.

Rais Kikwete aliunda tume hiyo Mei mosi mwaka jana kuchunguza malalamiko yaliyotokana na utekelezaji wa Operesheni Tokomeza Ujangili.
Operesheni hiyo ilibuniwa na Wizara ya Maliasili na Utali kwa lengo la kupambana na ujangili na ilitekelezwa kwa ushirikiano na wizara za Ulinzi, Mambo ya Ndani na Kilimo na Mifugo
CREDIT:MWANANCHI
Next Post Previous Post
Bukobawadau