Bukobawadau

MBOWE AHUKUMIWA,UTAA WA SIFA YA KUGOMBEA WAIBUKA

Hai. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amehukumiwa kulipa faini ya Sh1 milioni au kwenda jela mwaka mmoja baada ya kupatikana na hatia ya kumshambulia mwangalizi wa Uchaguzi Mkuu mwaka 2010.
Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi wa Wilaya ya Hai, Denis Mpelembwa. Mbowe, ambaye ni Mbunge wa Hai alilipa faini hiyo iliyochangwa chapchap na wabunge saba wa Chadema na wafuasi wa chama hicho waliokuwa mahakamani hapo.
Wabunge waliochanga fedha hizo ni, Mustafa Akuney wa Mbulu Lucy Owenya, Grace Kiwelu, Cecilia Pareso, Joyce Mukya, Rose Kalili na Paulin Gekul wote wa Viti Maalumu.
Utata wa kupoteza sifa ya kugombea
Hukumu hiyo iliibua mjadala mkali kwenye mitandao ya kijamii juu ya uwezekano wa kumzuia Mbowe ambaye pia ni Kiongozi wa Upinzani Bungeni kuwania tena ubunge au urais katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba.
Hata hivyo, Mwanasheria, Alex Mgongolwa akinukuu Katiba ya Tanzania Ibara ya 67 (1)(c); 67(2) (c na d) alisema hukumu hiyo haiwezi kumzuia kugombea ubunge kwa sababu hakwenda jela na kosa lake halihusu kukosa utovu wa uaminifu, kukwepa kodi wala kuvunja Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
Suala hilo linafanana na lililotokea katika mchakato wa uteuzi wa wagombea urais mwaka 2005 wakati aliyekuwa mgombea urais wa DP, Mchungaji Christopher Mtikila na mgombea mwenza wake, Saidi Soud Said walipowekewa pingamizi kutokana na kutumikia kifungo jela, Mtikila akitumikia mwaka mmoja kwa kosa la uchochezi, Said akitumikia chuo cha mafunzo kwa kosa la biashara ya vitambaa. Hata hivyo, pingamizi hilo lilitupwa na aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Jaji Lewis Makame (marehemu) baada ya kusikiliza utetezi wa Mtikila na Said, kuwa makosa waliyofungwa kwayo hayakuwa ya kukwepa kodi, kukosa uaminifu wala kukiuka maadili ya viongozi wa umma.
Mashtaka
Mbowe alikuwa anakabiliwa na mashtaka ya kumfanyia shambulio la kawaida, mwangalizi wa ndani wa Uchaguzi Mkuu Oktoba 31, 2010, Nassir Yamin katika kituo cha kupigia kura kilichokuwa katika Zahanati ya Lambo.
Yamin alikuwa ni mwangalizi wa kutoka Baraza Kuu la Waislamu wa Tanzania (Bakwata).
Akitoa hukumu hiyo, Hakimu Mpelembwa ambaye amehamishiwa Bukoba, alisema kitendo kilichofanywa na Mbowe hakikubaliki na kinapaswa kukemewa.
“Kitendo alichokifanya mshtakiwa akiwa Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema na Mbunge wa Jimbo la Hai ambaye alipaswa kuwa kioo cha jamii hakikubaliki na lazima kikemewe,” alisema.

“Kwa hiyo hukumu ya Mahakama ni kwamba atalipa faini ya Sh1,000,000 au akishindwa kulipa atakwenda magereza kwa mwaka mmoja,” alisema hakimu huyo.
Ushahidi
Akichambua ushahidi uliomtia Mbowe hatiani, Hakimu huyo alisema Mahakama imeegemea ushahidi wa shahidi wa kwanza, Yamin na shahidi wa pili John Mushi aliyekuwa msimamizi wa kituo.
Alisema ushahidi huo ulieleza kuwa siku hiyo Mbowe aliingia katika Kituo cha Zahanati ya Lambo katika Jimbo la Hai na kuuliza uhalali wa mlalamikaji kuwapo kituoni hapo.
Mashahidi hao waliiambia Mahakama kuwa walimuona Mbowe akimkunja na kumtoa nje kwa nguvu mwangalizi huyo wa ndani na baadaye mbunge huyo kuondoka katika kituo hicho.
Alisema ushahidi wa mashahidi hao uliungwa mkono na shahidi wa nne wa mashtaka, ambaye ni daktari wa Hospitali ya Wilaya ya Hai, aliyemtibu mlalamikaji na kujaza fomu PF3.
Alisema ushahidi wa daktari huyo unaonyesha kuwa mlalamikaji alikuwa na michubuko katika shavu lake moja na shingoni iliyotokana na kupigwa na kitu butu.
Hata hivyo, aliukataa ushahidi wa shahidi wa saba, Mkaguzi Msaidizi wa Polisi, Shafii aliyekuwa mpelelezi mkuu kuwa Mbowe alikiri kufanya kosa hilo alipoandika maelezo ya onyo polisi.
Hakimu Mpelembwa alisema japokuwa upande wa mashtaka uliwasilisha maelezo hayo kama kielelezo lakini baada ya kuyapitia, hakuna mahali ambako Mbowe alikiri kufanya kosa hilo.
Utetezi wa Mbowe
Hakimu Mpelembwa alisema wakati akijitetea mahakamani, Mbowe alikanusha kufanya tukio hilo lakini alikiri kufika katika kituo hicho na kumtaka mwangalizi huyo kumwonyesha kitambulisho chake.
“Katika utetezi wake, mshtakiwa alikanusha kumpiga Nasir Yamin wala kumfanyia kitu chochote kibaya, bali alimwamuru atoke nje kwani hakuwamo kwenye orodha ya waangalizi iliyotolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi.”
INAENDELEA KATIKA GAZETI MWANANCHI
Next Post Previous Post
Bukobawadau