Bukobawadau

SERIKALI ZA VIJIJI ZATAKIWA KUHUSISHA MAAFA YA MABADILIKO YA TABIANCHI NA MIPANGO YA MAENDELEO

Mshiriki wa Mafunzo  ya  utekelezaji mradi wa Kuimarisha mfumo wa habari za hali ya hewa na mifumo ya tahadhari ya mapema nchini akichangia wakati wa mafunzo hayo kwa wajumbe wa kamati za maafa za kata ya Makiba, wilayani Arumeru mkoani Arusha, mafunzo hayo yameratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia mradi huo , Tarehe 13 Juni, 2015.
 Mratibu mradi kitaifa wa Kuimarisha mfumo wa habari za hali ya hewa na mifumo ya tahadhari ya mapema nchini, Alfei Daniel akifafanua jambo wakati wa mafunzo ya utekelezaji wa mradi huo kwa wajumbe wa  kamati za maafa za kata ya Makiba, Wilayani Arumeru mkoani Arusha, tarehe 13 Juni, 2015, wengine ni wawezeshaji wa mafunzo hayo.
 Washiriki wa mafunzo ya utekelezaji mradi wa Kuimarisha mfumo wa habari za hali ya hewa na mifumo ya tahadhari ya mapema nchini, kutoka kamati za maafa za kata ya Makiba, wilayani Arumeru mkoani Arusha, wakiandika maudhui ya mafunzo hayo yaliyoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Tarehe 13 Juni, 2015.
 Washiriki kutoka kamati za maafa za kata ya Makiba, Wilayani  Arumeru mkoani Arusha, wakiwa katika picha ya pamoja na Mratibu mradi kitaifa wa Kuimarisha mfumo wa habari za hali ya hewa na mifumo ya tahadhari ya mapema nchini, Alfei Daniel (wa kwanza kushoto) mara baada ya kufunga mafunzo ya utekelezaji wa mradi huo, tarehe 13 Juni, 2015.


Serikali za vijiji zatakiwa kuhusisha Maafa ya mabadiliko ya tabianchi na mipango ya maendeleo.
Ofisi ya Waziri Mkuu, Idara ya Uratibu  Maafa  kupitia mradi wa kuimarisha mifumo ya  habari za hali ya hewa na mifumo ya tahadhari nchini imezitaka serikali za  mitaa  na vijiji nchini kuhusisha maafa yatokanayo na mabadiliko ya tabianchi na mipango yao ya maendeleo, ili kuhakikisha jamii inakuwa na uchumi bora na uwezo wa kupunguza athari za maafa hayo.
Akiongea wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wajumbe wa Kamati ya Maafa wa kata ya Makiba Wilayani Arumeru, mkoani Arusha, Mratibu Mradi huo Kitaifa, Alfei Daniel tarehe 13  Juni, 2015, alisema serikali za vijiji zitumie taarifa za athari za mabadiliko ya tabianchi za vijiji vyao ambazo zitakuwa zinaainishwa kupitia mradi huo  kama sehemu ya kuandaa mipango mikakati ya maendeleo vijijini.
“Kupitia mradi huu tutakuwa tunatoa taarifa za hali ya hewa kwa eneo husika na kwa wakati, Ufahamu juu ya Hali ya hewa, mabadiliko ya tabianchi, maji na mazingira  ni muhimu sana na ni kiungo kikubwa katika kuandaa mikakati na mipango ya maendeleo vijijini, hii itasaidia kuimarisha uwezo wa serikali za vijiji kuwalinda wananchi kwa athari zinazoweza kusababishwa na mabadiliko ya tabianchi” alisisitiza Daniel
Aliongeza kuwa uwepo wa miundombinu hafifu vijijini, upungufu wa wataalamu wa masuala ya hali ya hewa pamoja na taarifa za hali ya hewa kutowafikia wanavijiji kwa wakati, kumekuwepo na matumizi madogo ya taarifa za hali ya hewa kitendo ambacho huziweka jamii za vijijini katika mazingira magumu hasa kwenye shughuli za kiuchumi pindi yanapotokea maafa ya mabadiliko ya tabianchi kama ukame na mafuriko.
Akiogea wakati wa mafunzo hayo Diwani wa Kata ya Makiba, Wilayani Arumeru Mkoani Arusha, Mwanaidi Kim alifafanua kuwa ni muhimu vijiji kuhusisha maafa yatokanayo na maafa ya mabadiliko ya tabianchi katika mipango ya maendeleo kwani athari zake zinapotokea shughuli za maendeleo hukwama.
“Katika kata yangu kuna vijiji sita ambavyo ni; Makiba, Patanumbe, Valesika, Engatani na Kaloleni, lakini katika vijiji hivi vyote kuna ishara ya upungufu wa chakula, Hivyo kama mtu hana chakula ni vigumu kufanya shughuli za maendeleo lakini  kupitia mradi huu athari hizi hazitatupata  tena  kwani tutakuwa tunapata taarifa za hali ya hewa kwa wakati na sisi tunapanga vizuri mipango yetu ya kimaendeleo” alisema
Mradi huo ambao utatekelezwa nchi nzima, kwa sasa unatekelezwa kwa majaribio tangu mwaka 2014 hadi 2018 katika Halmashauri ya wilaya ya Meru, Mkoani Arusha  na Halmashauri ya wilaya ya Liwale, mkoani Lindi.
Next Post Previous Post
Bukobawadau