Bukobawadau

MKUU WA MKOA MPYA WA KAGERA AKABIDHIWA OFISI NA KUANZA KAZI RASMI KWA KUTOA MAAGIZO YAKE KWA WATENDAJI NA VIONGOZI WA MKOA HUO

Mkuu wa Mkoa mpya wa Kagera Meja Jenerali Mstaafu Salim Mustafa Kijuu amekabidhiwa rasmi ofisi na kuanza kutekeleza majukumu yake kama Mkuu wa Mkoa wa Kagera. Makabidhiano hayo yamefanyika siku ya Jumanne  Machi 22, 2016 kati yake na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Kagera Mhe. John Mongella aliyehamishiwa Mkoani Mwanza.
Katika hafla fupi ya makabidhiano hayo Mhe. Meja Jenerali Mstaafu Kijuu akiongea na wadau mbalimbali wa Mkoa aliwaomba wananchi wote wa  Kagera kuonesha ushirikiano wa kutosha katika kutekeleza majukumu yake aidha aliongelea mikakati yake katika kutekeleza majukumu yake hapa Mkoani.
 Watumishi wa Umma
Mhe. Meja Jenerali Mstaafu Kijuu aliwakumbusha watumishi wa umma katika Mkoa wa Kagera kuifahamu vizuri dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano kuwa ni kuwajibika kwa kufanya kazi kwa kasi inayotakiwa, kwa nguvu, maarifa, upendo na uadilifu mkubwa bila kusukumwa na mtu yeyote aidha, kila mtumishi afanye kazi kwa uwezo wake wote.
“Mtumishi wa umma anatakiwa kufahamu wajibu wake hasa kwa kuwatumikia wananchi ili kusukuma maendeleo yao mbele kwa kufanya kazi kwa kujituma bila kubabaisha, pili kufanya kazi kwa kutenda haki bila kudhurumu wananchi haki zao.”  Alitoa ilani Mhe. Meja Jenerali Mstaafu Kijuu.
Maagizo
Mkuu wa Mkoa Mpya wa Kagera Mhe. Meja Jenerali Mstaafu Kijuu aligiza kuundwa mara moja mabaraza ya kushughulikia haki za wananchi kama hayapo na kama yapo yaanze kufanya kazi zake mara moja kwa kuwahudumia wananchi ili kupata haki zao. Wakuu wa Wilaya kuhakikisha wananhimiza wananchi kufanya kazi kila mtu kwa nafasi yake bila kutega.
Sekta ya Afya, Vituo  vyote vya kutolea huduma za afya vinatakiwa kuwa katika hali ya usafi na kutoa huduma stahiki kwa wananchi. Watoa huduma wanatakiwa kuhakikisha kuwa dawa zinapatikana muda wote kama ambavyo Serikali imekuwa ikiagiza mara kwa mara.
Ulinzi na Usalaama wa Mkoa, Mhe. Meja Jenerali Mstaafu Kijuu alisema kuwa wale wote ambao wanafanya vitendo vya uvunjifu wa amani hasa kwa kuteka wananchi na vyombo vya usafiri maporini, atahakikisha anasafisha uchafu huo wote kwa kushirikiana na vyombo vya Ulinzi na Usalaama ili kukomesha tabia hiyo.
Wahamiaji Haramu, Mkuu wa Mkoa Mpya amewaagiza Wakuu wa Wilaya za mpakani kutoa au kugatua madaraka kwa Wenyeviti wa vijiji na Vitongoji ili waweze kufuatilia mienendo ya wageni wanapoingia nchini ili waweze kuwarudisha mara moja walikotoka. Aidha, aliwaagiza Afisa Uhamiaji Mkoa na Jeshi la Polisi kufanya kazi zao kikamilifu ili kuondoa wahamiaji haramu.
Chakula, Kwakuwa Mkoa wa Kagera hauna baa la njaa Mkuu wa Mkoa alisema kuwa wananchi wanatakiwa kuhamasishwa kutunza chakula hata kama hakuna baa la njaa ili kujihakikishia akiba ya mbeleni bila kuuza chakula chote cha akiba.
Ukusanyaji wa Mapato ya serikali, Mkuu wa Mkoa aliziagiza taasisi zote za Serikali kuhakikisha zina kusanya mapato kwa njia ya kielekitroniki ili Serikali ipate mapato ambayo yanarudishwa Mkoani kwetu ili yatekeleze miradi ya maendeleo kwa wananchi.


Mishahara Hewa, Mhe. Meja Jenerali Mstaafu Kijuu aliagiza kwa watendaji wa Serikali kama kuna watumishi hewa waondolewe mara moja kabla ya tarehe 30/03/2016 na baada hapo utafanyika uhakiki kwa kupokea mishahra dirishani  kama mwaka 1994 na atakayebainika atachukuliwa hatua kali za kisheria.
Elimu, viongozi na na watendaji wanatakiwa kutekeleza Sera ya Serikali ya Elimu Bure kwa kukabiliana na changamoto mabalimbali ambazo zimejitokeza mara baada ya kuanzishwa Sera hiyo kama uhaba wa madawati na vyumba vya madarasa na kufikia Juni 30, 20116 changamoto hizo ziwe zimefanyiwa kazi na kumalizika.
 Milioni Hamsini kila Kijiji, Mhe. Meja Jenerali Mstaafu Kijuu alimalizia kwa kuwaagiza viongozi  na watumishi  wa Serikali hasa ngazi za Serikali za Mitaa  kuwaandaa wananchi kwa kuwaelimisha juu ya uibuaji wa miradi ya maendeleo ili Milioni Hamsini zilizohaidiwa katika kampeini ambazo zipo karibu kuletwa ziwanufaishe wananchi katika vikundi na siyo kuzigawana tu.
Kwa upande mwingine aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Kagera aliyehamishiwa Mkoani Mwanza Mhe. John Mongella aliwashukuru wananchi wa wote wa Kagera kwa kipindi alichokuwepo Mkoani kwa ushirikiano wao mkubwa na kuwaomba ushirikiano huo wauendeleze kwa Mkuu wa Mkoa Mpya Mhe. Meja Jenerali Mstaafu Kijuu.
Historia Fupi
Mkuu wa Mkoa mpya Meja Jenerali Mstaafu Salim Mustafa Kijuu  amehudumu katika Jeshi la Wananchi Tanzania kwa miaka arobaini (40) na alistaafu Jeshini Januari 30, 2016 akiwa Kamanda wa Majeshi ya nchi kavu. Aidha, Aliteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Kagera tarehe 13/03/2016 na kuapishwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe Magufuli tarehe 15/03/2016.
Mkuu wa Mkoa mpya Meja Jenerali Mstaafu Salim Mustafa Kijuu  anakuwa Mkuu wa Mkoa wa Kagera wa 22 tangu uhuru mwaka 1961 amabpo Mkuu wa Mkoa wa kwanza wa Kagera alikuwa Marehemu Samwel Ntambala Rwangisa.






Next Post Previous Post
Bukobawadau