Bukobawadau

MAONESHO YA NANE NANE MKOANI KAGERA YAZINDULIWA RASMI NA MKUU WA MKOA NA KUKEMEA VIKALI VITENDO VYA UCHOMAJI MOTO HOVYO KAGERA

Maonesho ya Wakulima ya Nanenane ya mwaka huu 2016 Mkoani Kagera tayari yamezinduliwa  rasmi na Mkuu  wa Mkoa wa Kagera Meja Jenerali Mstaafu Salum M. Kijuu katika uwanja wa kilimo wa Kyakairabwa uliopo nje kidogo ya Manispaa ya Bukoba.

Akifungua Maenesho hayo Mhe. Kijuu Agosti 3, 2016 alitembelea mabanda na bustani mbalimbali za vipando vilivyoandaliwa na wadau mbalimbali wa kilimo, mifugo na uvuvi ambao ni kutoka katika Mkoa mzima wa Kagera zikiwemo Halmashauri za Wilaya zote za Kagera.

Aidha Mhe. Kijuu mara baada ya kutembelea shughuli za wadau wa kilimo, Mifugo na Uvuvi  aliongea na wananchi walihudhuria katika maonesho hayo na kutoa wito kwa wananchi ambao hawajafika katika viwanja hivyo kufika ili kujifunza shughuli mbalimbali za kilimo cha kisasa katika kujikomboa na umasikini kwa kutumia eneo dogo na kulima kwa tija.
Kaulimbiu ya maonesho ya Nane Nane kitaifa mwaka huu 2016 ni “Kilimo, Mifugo na Uvuvi ni Nguzo ya Maendeleo, Vijana shiriki kikamilifu Hapa kazi tu.” Akisistizia Kauli mbiiu hiyo Mhe. Kijuu aliwakumbusha vijana kushiriki katika shughuli za kilimo, ufugaji wa kisasa na ufugaji wa samaki ili kujiajili na kuacha kulalamika kuwa hakuna ajira.
Katika hatua nyingine Mkuu wa Mkoa alitoa agizo kwa Wakuu wa Wilaya wote wa Mkoa wa Kagera kuhakikisha wadhibiti vitendo vya uchomaji moto ambapo vitendo hivyo vimekithiri mkoani hapa kwa kuchoma mashamba ya misitu ya hifadhi, misitu ya kupandwa na mashamba ya wananchi hasa kwa kipindi cha miezi miwili ya Juni na Julai 2016.

Wakuu wa Wilaya waliagizwa pia kuhakikisha wanawasimamia viongozi katika ngazi zote na kuwabaini wananchi wanaojihusisha na vitendo vya uchomaji moto na kuwachukulia hatua kali za kisheria aidha, Kwa viongozi ambao hawatawajibika watachukuliwa hatua kali za kisheria wao wenyewe.
Agizo la pili la Mkuu wa Mkoa wa Kagera lilikuwa ni kuhusu Wanansiasa kufanya mikutano katika maeneo yao na si viongozi wa kisiasa kutoka katika maeneo mengine kwenda sehemu zisizo kuwa zao na kufanya mikutano ya kisiasa na kuwasumbua wananchi katika shughuli zao za maendeleo ambapo Mhe. Kijuu alisema hatakuwa tayari kuwavumilia viongozi wa namna hiyo katika mkoa wake.
Pamoja na kufungua rasmi maonesho ya Nane Nane Mkoani Kagera pia Mkuu huyo wa Mkoa alizindua wiki ya Unyonyeshaji Kitaifa ambayo inaadhimishwa Mkoani Kagera ambapo maonesho yake, Elimu na ushauri vinatolewa katika uwanja huo wa Kyakailabwa na kilele chake kitakuwa ni Julai 7, 2016.
Next Post Previous Post
Bukobawadau