Bukobawadau

KITUO CHA EATV NA HAWA FOUNDATION WAZINDUA KAMPENI YA KUCHANGISHA FEDHA KUWASAIDIA WASICHANA WANAFUNZI WA SHULE ZA SEKONDARI WAKATI WA HEDHI



Kituo cha televisheni cha EATV kwa kushirikiana na taasisi ya haki za wanawake (HAWA), wamezindua kampeni ya kuchangisha fedha kwa ajili ya wasichana na wanafunzi wa shule za sekondari nchini Tanzania,kununulia taulo za hedhi (pedi) ili kuwasitiri na kulinda utu wao.

Akizungumza katika mkutano na wanahabari,jijini Dar leo, Afisa Masoko wa EATV,Brendansoa Kileo amesema kuwa Kampeni hiyo inazinduliwa wakati tukielekea siku ya Wanawake Duniani Machi 8.


"Nasi kama kituo cha habari kinachofanya biashara zake nchini,tumeona kuwa tuna wajibu wa kutumia vituo vyetu vya EATV na East Africa Radio kuhamasisha jamii kuwachangia watoto wetu wa kike kutatua tatizo",alisema  Brendansoa.

Amesema kuwa kumekuwepo na tatizo la wanafunzi wa kike kukosa kuhudhuria shule kati ya siku tano hadi saba kwa kukosa pedi za kujisitiri wakati wa hedhi .“kwa mwaka inakadiriwa mwanafunzi wa kike hukosa kuhudhuria shule kwa siku 60 hadi 70 kutokana na kukosa pedi tu , hali ambayo imekuwa ikichangia kutofanya vizuri katika masomo yao”amesema Brendansoa.

Amesema kuwa wanafunzi wengi wamekuwa wakihatarisha afya zao kwa kutumia matambara kwa ajili ya kujisitiri wakati wa hedhi na kusababisha aibu pale ambapo vitambaa vinapovujisha damu.

Wakati huo huo Mkurugenzi wa Taasisi ya Haki  za Wanawake (HAWA) , Joyce Kiria ameongeza kusema kuwa ili kuchangia kampeni hiyo,wanatarajia kila Mwananchi atakayeguswa na tatizo hilo basi anaombwa kuchangia kuanzia kiasi cha shilingi Elfu Tano (5,000/=),ili
 kuwasaidia watoto wa kike kupata pedi na kuhudhuria shule. 

"Katika kampeni hiyo EATV na East Afrika Radio itahamasisha uchangiaji wa fedha na taasisi ya Haki za Wanawake (HAWA FOUNDATION),iliyosajiliwa kwa mujibu wa taratibu za nchi mwaka 2011,itahusika na kupokea na kusimamia fedha zote zitakazochangishwa na kusimamia ununuzi na usambazaji wa pedi hizo mashuleni",alisema Joyce Kiria.


Kiria aliongeza kwa kueleza taratibu za uchangiaji kuwa,unaweza kutuma fedha hizo kwa M-Pesa kupitia namba 5530307 ama kupitia akaunti ya CRDB namba 0150258750600.

Mkurugenzi wa Taasisi ya Haki  za Wanawake (HAWA) , Joyce Kiria akifafanua jambo kuhusiana na uzinduzi wa  kampeni ya kuchangisha fedha kwa ajili ya kuwasaidia wasichana na wanafunzi wa shule za sekondari nchini Tanzania,kuwanunulia taulo za hedhi (pedi) ili kuwasitiri na kulinda utu wao.

Pichani kulia ni  Afisa Masoko wa EATV,Brendansoa Kileo akizungumza mbele ya Waandishi wa Habari (hawapo pichani) mapema leo jijini Dar,kuhusiana na uzinduzi wa  kampeni ya kuchangisha fedha kwa ajili ya kuwasaidia wasichana na wanafunzi wa shule za sekondari nchini Tanzania,kuwanunulia taulo za hedhi (pedi) ili kuwasitiri na kulinda utu wao.Pichani kati ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Haki  za Wanawake (HAWA) , Joyce Kiria  pamoja na Afisa Masoko wa East Afrika Radio Basilisa Biseko.

Wa pilia kulia ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Haki  za Wanawake (HAWA) , Joyce Kiria akizungumza mbele ya Waandishi wa Habari kuhusu uzinduzi wa  kampeni ya kuchangisha fedha kwa ajili ya kuwasaidia wasichana na wanafunzi wa shule za sekondari nchini Tanzania,kuwanunulia taulo za hedhi (pedi) ili kuwasitiri na kulinda utu wao.


Baadhi ya Wanahabari wakifuatilia yaliyokuwa yakizungumza kwenye mkutano huo.

Next Post Previous Post
Bukobawadau