Bukobawadau

SIMBACHAWENE ASISITIZA USAFI WA MAZINGIRA KATIKA MJI WA DODOMA


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. George  Simbachawene amewataka viongozi wa Manispaa ya Dodoma  kuwa wabunifu katika kushughulikia suala la usafi wa mazingira ili kuufanya mji wa Dodoma kuwa wa kuvutia na wakati huo huo kuutokomeza ugonjwa wa kipindupindu.
Alisema ili waweze  kutekeleza jambo hilo mapema wanatakiwa kuanza utekelezaji katika masuala yasiyohitaji  fedha wakati wakitafuta fedha za kutekeleza mambo yanayohitaji fedha ili kuweza kufanya mabadiliko kwa haraka.

Akizungumza katika ziara fupi ya kutembelea maeneo mbalimbali ya mji wa Dodoma iliyokuwa na lengo la kuhamasisha utunzaji na usafi wa mazingira ya mji wa Dodoma ili kujikinga na kipindupindu katika maeneo ya River Pombe, Uwanja wa Barafu na katika Soko kuu la Majengo iliyofanyika leo mjini Dodoma, Mhe. Simbachawene amesema itakuwa ni aibu kuwa na kipindupindu katika mji wa Dodoma kwakuwa hivi sasa unapokea wageni mbalimbali kutoka nchini na nje ya nchi.
Mhe. Simbachawene aliwataka viongozi wa Mkoa wa Dodoma, Manispaa ya Dodoma  na Mamlaka ya Ustawishaji wa Makao Makuu kushirikiana na kuhakikisha mazingira ya mji wa Dodoma yanakuwa safi  likiwepo suala la kuifanyia mitaro usafi hasa katika kipindi hiki ambacho mji wa Dodoma upo katika harakati za kuwapokea wageni  wengi wakiwepo Mabalozi kutoka Nchi mbalimbali.
Alitaka uongozi wa Manispaa ya Wilaya ya Dodoma kuhakikisha wanaweka ulinzi katika eneo la Pombe River kwa kutumia Walinzi wa jiji au Jumuiya ya watu waliojenga karibu na eneo hilo  ili kulilinda eneo hilo na kuhakikisha wananchi hawatupi takataka katika eneo hilo.

Aliwataka wananchi wa Dodoma kujipanga kutumia fursa zinazojitokeza Dodoma kutokana na kuja kwa wageni wengi  ili kujiongezea kipato lakini wakati huo huo kuhakikisha huduma wanazotoa zinazingatia ubora kwa kuwa safi .
Mhe. Simbachawene aliwahakikishia wageni wanaohamia Dodoma kuwa Mamlaka ya Mkoa wa Dodoma na Manispaa zimejipanga katika kuhakikisha kuwa huduma za afya zinakuwepo  wakati wote na kuwatoa hofu za kukosa huduma za afya.
“ Serikali imejenga hospitali kubwa ya Benjamin Mkapa ambayo ubora wake  kwa utoaji wa huduma Tanzania inaweza kuwa ya kwanza kwa kutoa matibabu ya daraja la Kwanza. Kituo cha Afya cha Makole pia kimeboreshwa na kupandishwa hadhi ambapo sasa kitatoa huduma za hospitali. Lakini pia vituo binafsi vya afya na hospitali ya DCMC vimejipanga kusaidiana na Serikali katika utoaji wa huduma za Afya. Alisisitiza  Mhe. Simbachawene.
Naye Naibu Katibu Mkuu  Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa anayeshughulikia Afya Dkt. Zainab Chaula aliwasisitiza watendaji wa Mkoa na Manispaa ya Dodoma kuhakikisha wanasimaia vizuri usafishaji wa mazingira ili kuhakikisha kuwa magonjwa ya mlipuko kama kipindupindu yanatokomezwa kabisa.
Next Post Previous Post
Bukobawadau