Bukobawadau

UWT YAUNGA MKONO UAMUZI YA RAIS KUHUSU MAKANIKIA NA MIKATABA YA MADINI.


Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) inaunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais Dkt John Pombe Magufuli na kupongeza jitihada zake za kupambana na aina zote za ubadhirifu, dhulma na unyonyaji uliobainika kwenye mikataba ya uchimbaji na usafirishaji madini, na hivyo kuhakikisha maliasili za Taifa zinatumika kwa manufaa ya watanzania wote.
Pia, Umoja wa Wanawake Tanzania unatoa pongezi kwa wajumbe wa Kamati kwa weledi, uzalendo na ujasiri mkubwa wa kubainisha hasara kubwa iliyopatikana kwa Taifa letu kutokana na usafirishaji wa makanikia, na hivyo UWT inakubaliana na kuunga mkono mapendekezo yote ya Kamati na uamuzi wa Mheshimiwa Rais Dkt John Pombe Magufuli wa kutaka kurekebisha mikataba na sheria za usimamizi na uchimbaji wa madini nchini.
Aidha UWT inapongeza hatua za awali za mazungumzo yaliyofanywa leo tarehe 14/06/2017 baina ya Mhe Rais Dkt Magufuli na Mwenyekiti wa Kampuni ya Barrick Gold Corporation ambao ni wamiliki wa Kampuni ya Acacia Mining Limited Prof. John L. Thornton na kukubaliana kuhusu malipo ya fedha zilizopotea na kushirikiana katika ujenzi wa mtambo wa kuchenjulia dhahabu (smelter) hapa nchini.
Kufanikiwa kwa mazungumzo hayo, na marekebisho ya sheria na mikataba ya madini kutawezesha Watanzania kupiga hatua ya kujikomboa na umasikini, hususani Wanawake ambao wameendelea kukosa huduma za msingi za kijamii ikiwemo afya, elimu, maji na malazi bora. Wanawake wengi wanahangaika kwa kukosa mitaji ya biashara na mikopo ya wajasiriamali wadogo huku wakisumbuliwa kulipa tozo, ushuru na kodi za kero.
UWT inatoa rai kwa wananchi wote kumuunga mkono Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kujivunia utanzania wetu. Tunamuombea Mhe Magufuli, MwenyeziMungu azidi kumpa afya njema, moyo wa ujasiri, uzalendo na upendo kwa watanzania.
KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI

AMINA MAKILAGI (MB)
KATIBU MKUU
JUMUIYA YA UMOJA WA WANAWAKE TANZANIA.
14/06/2017
Next Post Previous Post
Bukobawadau