Lwakatare amwekea DPP pingamizi
Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Wilfred Lwakatare.
Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa Chama cha
Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Wilfred Lwakatare, amewasilisa
pingamizi la awali dhidi ya maombi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP),
katika Mahakama ya Rufani.
DPP amewasilisha katika Mahakama ya Rufani maombi
ya marejeo ya uamuzi wa Mahakama Kuu ya Tanzania wa kuwafutia washtakiwa
hao mashtaka ya ugaidi, akiiomba mahakama hiyo iitishe majalada ya kesi
hiyo na kuchunguza uhalali wa uamuzi huo.
Hata hivyo Lwakatare kupitia kwa jopo la mawakili
wake, jana aliwasilisha pingamizi la awali dhidi ya maombi hayo
akiainisha hoja mbili, ambazo mawakili wake watazitoa wakati wa
usikilizwaji wa maombi hayo.
‘‘Maombi hayo ya marejeo yana dosari ambazo
haziwezi kurekebishwa kwa kutokana na kushindwa kuambatanisha nakala ya
mwenendo ambao ndio maombi hayo yamejengwa.’’ anadai Lwakatare.
Katika hoja ya pili anadai kuwa kiapo kinachounga
mkono maombi hayo ya marejeo, kina dosari ambazo haziwezi kurekebishika
kwa kuwa kimehusisha na mambo mengine yasiyohusika.
Lwakatare na Rwezaura walikuwa wakikabiliwa na
mashtaka manne, matatu kati yake yakiwa ya ugaidi na moja la kawaida la
jinai, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, wakidaiwa kula njama na
kupanga kumteka Dennis Msacky na kisha kumdhuru kwa kutumia sumu.
Hata hivyo, Mei 8, mwaka huu Jaji Lawrence Kaduri
wa Mahakama Kuu aliwafutia mashtaka hayo matatu ya ugaidi na kuwabakizia
shtaka moja linaloangukia kwenye jinai ya kula njama za kutenda kosa la
kumdhuru Msacky kwa kutumia sumu.
Jaji Kaduri alifikia uamuzi huo kutokana na maombi
yaliyowasilishwa kwake na mawakili wa washtakiwa hao, wakipinga uamuzi
wa DPP kuwafutia mashtaka katika kesi ya awali, namba 37, ya mwaka 2013
na kisha kuwakamata na kuwafungulia tena kesi yenye mashtaka hayohayo
muda mfupi baadaye.
Kutokana na uamuzi huo wa Mahakama Kuu, ndipo DPP alipowasilisha maombi ya marejeo katika Mahakama ya Rufani.
Katika maombi hayo DPP pia anaiomba Mahakama ya
Rufani ifute uamuzi na amri za Mahakama Kuu,kuhusu uhalali wa mashtaka
yaliyokuwa yakiwakabili washtakiwa, akidai kuwa Mahakama Kuu haikuwa
sahihi.