Bukobawadau

MAHAKAMA KUU YASITISHA MGOMO WA MADAKTARI

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akizungumza na Waandishi wa habari kuhusu mgogoro wa serikali na Madaktari, Ofisini kwake jijini Dar es Salaam Machi 6, 2012. Picha na Ofisiya Waziri Mkuu.

MAHAKAMA Kuu Divisheni ya Kazi imewaagiza madaktari walioitisha mgomo nchi nzima, kuusitisha mara moja.
Mbali na kusitisha mgomo huo, madaktari hao wameagizwa kutumia vyombo vya habari ilivyotumia kutangaza mgomo huo, kuutangazia umma kwamba mgomo huo haupo tena na kwamba wanarejea kazini.
Uamuzi huo umekuja siku moja baada ya madaktari hao kuanza rasmi mgomo wao wakishinikiza kujiuzulu kwa Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Hadji Mponda na Naibu wake, Dk. Lucy Nkya, kama moja ya sharti la kuendelea na mazungumzo na Serikali juu ya
madai yao mbalimbali ya maslahi.
Uamuzi wa Mahakama hiyo ulitolewa jana usiku na Jaji Regina Rweyemamu baada ya kusikiliza maombi ya Serikali yaliyowasilishwa mahakamani hapo Jumatano na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema, kupinga mgomo huo uliotangazwa juzi na madaktari hao, kinyume cha utaratibu.

Katika maombi yaliyowasilishwa mahakamani juzi chini ya hati ya dharura, Jaji Werema, alidai kuwa mgomo huo ni hatari kwa maisha ya watu na unafanyika wakati majadiliano yameanza kati ya madaktari na Serikali na huku kukiwa na kesi Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA) ambayo haijamalizika.

Pia alidai kuwa mgomo ni batili kwa kuwa haukufuata utaratibu kwani madaktari hao wana kiapo cha taaluma yao, ambacho kinaeleza kuwa wao ni sehemu ya taaluma ambazo haziruhusiwi kugoma.

Awali, Mwanasheria Mkuu wa Serikali alifungua kesi katika Tume ya Usuluhishi na Uamuzi, Jumanne iliyopita, lakini licha ya kupelekewa hati ya kuitwa katka shauri hilo, madaktari hao hawakutokea na zaidi ya hapo wakatangaza mgomo.

Kutokana na hilo, Serikali ililazimizika kwenda Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi chini ya hati ya dharura juzi kuiomba izuie mgomo huo.

Mbali na kugoma, Mwanasheria Mkuu wa Serikali alidai madaktari hao walikuwa na njia za kufanya kabla ya kugoma ikiwemo, kwenda Tume ya Usuluhishi na Uamuzi au kwenda katika Kamati inayoshughulika Huduma Maalumu.

Washitakiwa katika kesi hiyo ni Chama cha Madaktari (MAT) na Jumuiya ya Madaktari ambayo
Serikali inadai kuwa ni batili kwa kuwa haijasajiliwa.

Katika kesi hiyo, Serikali iliwakilishwa na Wakili Mwandamizi, Edson Mweyunge na walalamikiwa, MAT walihudhuria katika shauri hilo.

Mwishoni mwa wiki, madaktari walitangaza kuanza mgomo juzi baada ya Serikali kukataa matakwa yao ya kujiuzulu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Hadji Mponda na Naibu wake, Dk. Lucy Nkya.

Kwa sasa, suala la mgomo wa madaktari ulioanza jana nchini kote ndilo linalogonga vichwa kwa sasa na limetokea licha ya rai ya Serikali kupitia kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda, kuwasihi madaktari hao kutogoma kwa sababu matatizo yao yanashughuliwa.

Katika hatua nyingine, Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) na Chama cha Wafanyakazi wa Afya na Serikali Kuu (TUGHE), vimewanasihi madaktari wanaogoma na kuwataka wazingatie kiapo chao cha kuhudumia jamii na kurejea kazini.

Katibu Mkuu wa Bakwata, Shehe Suleiman Lolila, alisema jana kwamba pamoja na madaktati hao kuwa na hoja ya msingi kuhusu madai yao, jambo la msingi zaidi wangeweka maslahi ya Watanzania mbele.

“Tayari Serikali imeonesha dalili ya kuzungumza nao, kuhusu madai waliyoyawasilisha, wangetumia fursa hiyo na kurejea kazini, kwa kuwa wao bado wanabaki kuwa watu muhimu na kugoma kwao kunaweza kuleta maafa makubwa katika jamii,” alisema.

Aliwataka kuangalia kiapo chao, lakini pia kujifunza kuwa na subira wakati masuala yao yakishughulikiwa, kwani hata dini imeweka wazi kuwa mtu anapokuwa na subira hupata mafanikio na thawabu kubwa.

Katibu Mkuu wa Tughe, Ali Kiwenge, alisema mgogoro wa madaktari kwa sasa unaumiza zaidi
wananchi hasa kisaikolojia.

“Kwa sasa mtu hata ukipigiwa simu tu ukaambiwa mtoto, baba au mama anaumwa, unaanza kuwaza utafanyaje, kwa mgogoro huu nchi iko kwenye wasiwasi mkubwa bila sababu za msingi,” alisema.

Naye Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Nicholaus
Mgaya, alipotakiwa kutoa maoni na ushauri wake, alisema atazungumza na vyombo vya
habari leo kuhusu mgomo huo.

Kwa upande wa hali katika hospitali nchini, Taasisi ya Tiba ya Mifupa ya Muhimbili (MOI) jana ilisitisha huduma za wagonjwa wa nje kutokana na kupungukiwa madaktari.

Ofisa Uhusiano wa MOI, Almas Jumaa, alisema katika taasisi hiyo wameathirika sana na mgomo kwani wamebaki madaktari 10 ambao ni wakuu wa vitengo na Idara kati ya madaktari 72 waliopo.

Katika hospitali nyingine za Dar es Salaam, wagonjwa walirudishwa nyumbani na kutakiwa kurudi hospitalini baada ya kusikia kwenye vyombo vya habari kuwa huduma zimerejea.

Katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, wagonjwa walikutwa wamekaa nje kwenye viti vyao
huku ndugu wakitafuta jinsi ya kuwahamishia katika hospitali zingine za binafsi.

Aidha, RC Sadiki aliwaondoa hofu madaktari wanaoendelea kutoa huduma katika hospitali za
mkoa huo, licha ya kushinikizwa wagome, na kusema Serikali itawapa ulinzi, kwa kuwa wamekuwa wakipokea vitisho.

Aliwaomba waendelee kuokoa maisha ya Watanzania wenzao, kulingana na kiapo walichokula
kwa kuwa tayari Serikali imekubali kushughulikia madai yao hivyo kugoma si ufumbuzi.

Mikoani katika hospitali za Bugando Mwana, KCMC Moshi, Dodoma na Morogoro kulikuwa na
mgomo baridi.
Next Post Previous Post
Bukobawadau