Bukobawadau

MSIMAMO WA LIGI KUU ENGLAND;Manchester United Kileleni.

Manchester United imefanikiwa kukalia kiti cha Ligi ya Kuu ya England kwa mabao mawili yaliyopachikwa na Wayne Rooney na kuilaza West Brom.
Wayne Rooney aizamisha West Brom kwa mabao mawili
Wayne Rooney aizamisha West Brom kwa mabao mawili 

United imepata nafasi hiyo ya kukalia kiti cha uongozi baada ya Manchester City kuteleza kwa kulazwa bao 1-0 na Swansea.

Rooney aliifungia Manchester United bao la kwanza kabla ya mapumziko, alipounganisha mpira uliopigwa na Javier Hernandez ambao ulimpita mlinda mlango Ben Foster.

Mshambuliaji huyo wa Manchester United alifunga tena bao la pili kwa mkwaju wa penalti, wakati mlinzi wa West Brom Jonas Olsson alitolewa nje kwa kadi nyekundu baada ya kuoneshwa kadi ya pili ya njano.

Wakiwa wamesaliwa na michezo 10 kabla ya msimu wa ligi kumalizika, Manchester United sasa wanapewa nafasi nzuri ya kutetea ubingwa wake baada ya Manchester City kuteleza.

Matumaini ya Manchester City kunyakua ubingwa wa Ligi Kuu ya Kandanda ya England yaliingia dosari baada ya bao la kichwa dakika za mwisho la Luke Moore lilipoipatia Swansea ushindi wa bao 1-0.

Swansea City kwa ushindi huo sasa imeacha wazi mbio za kuwania ubingwa ligi ya England baada ya ushindi huo katika uwanja wao wa Liberty.
Kikosi cha Roberto Mancini kiliponea chupuchupu kufungwa dakika za mwanzo za mchezo wakati Joe Hart alipookoa mkwaju wa penalti wa Scott Sinclair baada ya Hart kumuangusha Wayne Routledge ndani ya sanduku la hatari.

Swansea ilipata bao lake hilo moja baada ya Moore kuunganisha kwa kichwa mpira wa pembeni wa Routledge zikiwa zimesalia dakika saba kabla mchezo kumalizika.
City hawakucheza vizuri ingawa Micah Richards dakika za mwisho alifunga bao ambalo lilikataliwa kwa vile alikuwa ameotea.

Manchester City sasa wanashikilia nafasi ya pili wakiwa na pointi 66 na Manchester United wamekusanya pointi 67.
chanzo cha habari ni BBC
Next Post Previous Post
Bukobawadau