Bukobawadau

Shindano la Miss Utalii Kanda ya Ziwa lafutwa


BODI ya Taifa ya Miss Tourism Tanzania Organization (MTTO), imelifuta shindano la Miss Utalii Kanda ya Ziwa 2012, lililo fanyika New Mwanza Hotel, juzi, huku taifa likiwa kwenye maombolezo ya siku tatu kutokana na msiba mkubwa wa ajali ya meli ya Mv Skagit, mjini Zanzibar na kupoteza uhai wa watu wengi.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotumwa katika vyombo vya habari jana jijini Dar es Salaam na kutiwa sahihi na Mkurugenzi wa Utawala na Fedha wa Miss Utalii Tanzania, Abubakari Omary Bakari, ilisema shindano hilo limefanyika kimakosa na matokeo yake hayawezi kutambuliwa kwa namna moja ama nyingine.
Alisema uamuzi wa serikali ni wa mwisho, hivyo hawajaunga mkono kufanyika kwa shindano hilo wakati nchi ina majonzi ya kupoteza ndugu na jamaa waliokufa kwenye ajali hiyo.
“Shindano limefanyika bila kuzingatia misingi ya kiubinadamu na uzalendo kwa taifa, hivyo bodi imeamua kulifuta na waandaaji watafuata tena utaratibu mwingine,” ilieleza taarifa hiyo na kuongeza:
“Miss Utalii ni shindano lenye uzalendo, hivyo inapotokea matatizo kama haya na agizo la maombolezo kutoka kwenye serikali nadhani kuna kila sababu ya kuliafiki.”
Shindano hilo limeandaliwa na Fania Beauty Salon, chini ya Mkurugenzi wake Fania Hassan, ambaye sasa ana changamoto nyingine ya kujiweka sawa katika jamii, ukizingatia kwamba taifa lilikuwa kwenye maombolezo ya siku tatu.
Next Post Previous Post
Bukobawadau