Bukobawadau

Ni CCM dhidi ya matakwa ya walio wengi

Na Prudence Karugendo
MONGOSUTHU (Gatsha) Buthelezi, ni mtawala wa kikabila (Chifu) wa kabila mojawapo pana katika jamii wa Wazulu, KwaZulu – Natal, nchini Afrika Kusini. Kutokana na kunogewa na utawala huo wa kijadi usio na aina yoyote ya demokrasia ndani yake, ilifikia wakati Buthelezi akaungana na makaburu wa Afrika Kusini kuzipiga vita harakati za wazalendo wa nchi hiyo za kuuondoa utawala wa kikaburu.
Makaburu ni watu weupe waliokuwa wanajinufaisha na utajiri wa Afrika Kusini kwa mabavu wakiwa wahamiaji toka Ughaibuni, huku wakiwa wamewatenga wazalendo wa nchi hiyo na kuwafanya watu wa daraja la tatu.
Lakini Buthelezi sio mweupe, ila alishawishika kuwa kibaraka wa weupe,  wakati fulani,  ili kuilinda hadhi yake iliyokuwa inapatikana kwa njia zisizo za kidemokrasia sawa na za makaburu walizozitumia kujipa ukubwa.
Kwa ufupi ni kwamba Buthelezi aliiogopa demokrasia kwa hofu ya kwamba pengine ingesababisha yeye kupokonywa kile alichokipata nje ya matakwa ya walio wengi. Maana kanuni kuu ya demokrasia ni kuyaheshimu matakwa ya walio wengi.
Hapa nchini kwetu kwa sasa wameanza kujitokeza akina Buthelezi wasio na idadi. Watu hao wanaonekana kuzipinga kwa nguvu zote harakati zinazoendelea nchini za kuijenga demokrasia ya vyama vingi. Wamejibanza kwa chama kimoja, chama tawala, na kukipigia debe eti kitawale milele sawa na Buthelezi alivyokuwa akijipendekeza, kiusaliti,  kwa makaburu na kuwaombea waitawale Afrika Kusini milele yote.
Wabaya hao wa demokrasia wanaufanya usaliti wao huo wakiwa wamejikinga kwenye kivuli cha CCM na kuonyesha kwamba wanakipenda sana chama hicho. Na chama hicho tawala, kama walivyokuwa makaburu wa Afrika Kusini, kinaamini kwamba ndicho pekee kilicho na haki ya kuitawala Tanzania pasipo kukiachia chama kingine chochote.
Lakini hatahivyo, sio kweli kwamba CCM hakiujui ukweli unaowafanya wananchi waitamani demokrasia, kinaujua sana. Ndiyo maana mpaka sasa, miaka 50 tangu nchi yetu ianze kujiongoza chenyewe kikiwa ndicho pekee kilichoushikilia usukani, bado kinadiriki kutamka kwamba nchi yetu bado ni changa! Sijui ni uchanga gani huo wa zaidi ya miaka 50!
Kwahiyo kwa kulielewa hilo CCM inaiangalia demokrasia kama adui yake namba moja, sababu demokrasia itawawezesha Watanzania kumbadilisha mshika usukani na kumuondoa huyu anayeifanya nchi iendelee kuwa changa hata baada ya zaidi ya miaka 50.
Ikumbukwe kwamba maendeleo yoyote hutokana na mabadiliko. Kitu kisicho na mabadiliko hudumaa, na katika udumavu hakuwezi kupatikana maendeleo.
Hata katika mwili wa binadamu, udumavu wowote katika viuongo vya binadamu uweza kusababisha ugonjwa wa saratani na baadaye kifo. Udumavu hauwezi kwa njia yoyote kumsaidia mwanadamu.
Tanzania kuendelea kutawaliwa na CCM ni kuukumbatia udumavu na kuyakataa maendeleo. Tanzania kuendelea kutawaliwa na CCM ni kuwa tayari kuendelea na uchanga milele yote.
Nchi zote zilizoendelea duniani zimefanikiwa kutokana na kuyakubali mabadiliko. Mabadiliko yanayoongozwa na demokrasia inayoyaheshimu matakwa ya watu. Hakuna nchi hata moja iliyowahi kuendelea kwa kuung’ang’ania udumavu unaoletwa na hofu ya mabadiliko.
Tuziangalie nchi kama Marekani, Uingereza, Canada, Japan na zote tunazoziendea na kuzipigia magoti ili zitusaidie. Hakuna hata moja iliyowahi kuendekeza udumavu kwa kuyaogopa mabadiliko.
Tunaona jinsi nchi hizo zinavyofanya mabadiliko karibu kila wakati wa mabadiliko (uchaguzi) ukifika.
Historia inatuonyesha kwamba zipo nchi ambazo watu wake walilazimika kufanya mapinduzi ya nguvu ya umma baada ya watawala wao kunogewa kutawala na hivyo kuyaogopa mabadiliko ambayo walihisi yangeweza kuwasababishia kupokonywa utawala wao. Baada ya wananchi kuona watawala wao wanawadumaza huku mambo yakienda hovyo wakaamua kuunganisha nguvu zao na kufanya mabadiliko ya lazima, mapinduzi.
Nchi mojawapo iliyoshuhudia wananchi wanalazimisha mabadiliko kinyume na matakwa ya watawala ni Ufaransa,  katika mapinduzi yaliyotokea kati ya mwaka 1787 – 99.
Bila ya mabadiliko hayo ya kulazimisha si ajabu Ufaranza tungekuwa nayo kundi moja kwa sasa, katika kundi la nchi zilizodumaa zikidai ni nchi changa.
Kwahiyo tutaona kwamba mabadiliko ni ya lazima katika jamii. Na mabadiliko yoyote ni haki ya wanajamii pasipo kutokea mtu wa kuihodhi haki hiyo.
Kwa kuliangalia hilo, kwamba ukosefu wa mabadiliko ndio unaozifanya baadhi ya nchi kukosa kujimudu, ndipo nchi tunazoziita za wahisani zikalazimika kuweka shinikizo la kila nchi kuwa na demokrasia ya vyama vingi kama njia mojawapo ya kuzisaidia nchi zilizodumaa kuondokana na udumavu. Nchi zilizodumaa ziliyahitaji mabadiliko. Demokrasia ya vyama vingi ni njia mojawapo ya kuyaelekea mabadiliko.
Hapa Tanzania, pamoja na kuikubali kwa  shingo upande demokrasia ya vyama vingi, bado mabadiliko yanaonekana kuleta hofu kuu, hasa kwa chama tawala. Watawala walio madarakani chini ya CCM wanaonekana kutoyaelewa majaliwa yao ndani ya mabadiliko yanayoweza kuletwa na demokrasia ya vyama vingi.
Udumavu tulio nao kisiasa unajionyesha kwa njia hiyo. Watawala wetu hawajawa tayari kuyapokea mabadiliko yatakayowafanya wao kuwa pembeni huku wengine wakitawala. Bado wana kasumba kama ile ya makaburu ya kwamba mtu mweusi hawezi kuongoza nchi hasa inayokaliwa na wazungu. Ndiyo maana tunasikia kauli za kwamba CCM itatawala kwa karne nyingi zijazo pamoja na ukweli wa kwamba chama hicho kimeidumaza nchi yetu, miaka zaidi ya 50 ya kujitawala bado inajiita nchi changa!
Ni kwa sababu hiyo tunakiona Chama Cha Mapinduzi kikifanya kila linalowezekana na lisilowezekana kuhakikisha mabadiliko yanayoweza kukiondoa madarakani hayafanikiwi. Kwa sasa tunaona hila za ajabuajabu zinazofanyika na nyingine kuonekana ni za hatari ilmradi tu zinaweza kukisaidia chama hicho kubaki madarakani.
Jambo la kujiuliza ni kwa nini CCM itawale zaidi ya miaka 50 huku nchi ikiendelea kuonekana changa na ombaomba lakini chama hicho kikose ujasiri wa kuyatamani mabadiliko na kutamani kuendelea kutawala chenyewe? Kwa nini CCM kiendelee kutamani kutawala katika hali kama hii ya kutia aibu? Kinatawala kikiwa kinawathamini Watanzania au kinatawala kikiwa kimewafanya Watanzania watu wa daraja la tatu kama makaburu walivyokuwa wanawachukulia wazalendo wa Afrika Kusini?
Nitoe mfano wa mtu aliyeithamini nchi yake na watu wake; Mwalimu Julius Kambarage Nyerere,  ulifika wakati Mwalimu akasema kwamba aliyoyafanya kwa nchi yake na watu wake yalikuwa yanatosha. Akasema kwamba ulikuwa wakati wa mtu mwingine kujitokeza na kujaribu, akasema kwamba angependa kuona mtu mwingine anajaribu kuiongoza nchi yake,  na pengine kuzidisha au kusahihisha pale ambapo yeye alishindwa. Huyo aliithamini nchi yake na kuitakia mema. Je, kwa nini CCM inashindwa kufanya hivyo kama kweli inaitakia mema nchi hii?
Wakati CCM kikijiona kuwa ndicho chama teule kinachopaswa kuitawala nchi yetu bila kukipisha kingine, kama ilivyokuwa imani ya makaburu kwa nchi ya Afrika Kusini, vilevile wapo kina Buthelezi wanaokiunga mkono chama hicho ili kitawale milele bila sababu yoyote wanayoweza kuionyesha kwa umma kwa nini wanafanya hivyo.
Katika zaidi ya miaka 50 CCM kimeshindwa kuifanya nchi yetu kuwa komavu inayoweza kujitegemea. Kwahiyo ipo haja gani ya chama hicho kuwafanya wananchi wayaogope mabadiliko? Na wanaokiunga mkono wanalo lipi la kutushawishi tuendelee kukiona kuwa ndicho pekee kinachoweza wakati ukweli tunauona kuwa chama hicho kimeshindwa tena vibaya?
Kama CCM ingekuwa na nia njema na nchi hii, kama alivyokuwa Mwalimu Nyerere, ingekubali bila woga wowote  kuwaacha wananchi wafanye mabadiliko kwa matakwa yao. Baada ya kipindi fulani wananchi wanaweza kuona kuwa pengine wamepotoka, kama mabadiliko yao yatakuwa yameenda mrama na kushindwa kuzaa matunda yaliyokusudiwa, na hivyo kuamua kukirudisha CCM kwenye usukani. Hiyo ndiyo demokrasia, kufanya  mabadiliko yenye mwelekeo wa maendeleo bila mizengwe wala shinikizo.
Ni kwamba watu wanataka mabadiliko, hiyo ni haki yao. Lakini kinyume na matakwa ya wengi CCM inataka ifanye kila mbinu kuyazuia mabadiliko hayo. Na kwa vile chama cha siasa sio mashine,  ila ni taasisi inayoongozwa na wanadamu, naweza kuamini kwamba yanayojitokeza ni mbinu zinazofanywa na watu wachache wakiungwa mkono na kina Buthelezi ili kuyazuia mabadiliko yanayotakiwa na walio wengi kwa manufaa ya hao wachache.
Wakati namalizia kuandika makala haya, msomaji mmoja wa Tanzania Daima, John Mnzajila, wa Gairo, kanitumia ujumbe mfupi wa maandishi akisema kwamba “Bado historia ya dunia inaonyesha kwamba chuki, fitina au uovu wowote ule kwa wengine havijawahi kushinda popote pale toka kuumbwa kwa ulimwengu”. Tuitafakari kauli hiyo.
0784 989 512 
Next Post Previous Post
Bukobawadau