Bukobawadau

Ubadhirifu umekithiri vyama vya ushirika, asema Waziri Chiza

Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza, amesema uchunguzi kwenye vyama vya ushirika nchini umeonyesha kuwa ubadhirifu wa fedha na mali za wanachama ni mkubwa.
Akiwasilisha makadirio ya bajeti ya wizara yake bungeni jana, Waziri Chiza alisema taarifa za ukaguzi zimewasilishwa kwenye bodi za uongozi wa vyama na baadhi zimewasilishwa katika mikutano mikuu ya vyama husika.
“Mfano, taarifa ya Chama Kikuu cha Ushirika cha Wetcu Ltd, imewasilishwa kwenye mkutano mkuu maalumu na wanachama wamefikia uamuzi wa kuiwajibisha bodi kwa kuiondoa madarakani na kuteua ya muda,” alisema.
Chiza alitaja vyama vilivyofanyiwa ukaguzi maalumu kuwa, ni Shirikisho la Vyama vya Ushirika (TFC), Chama Kilele cha Ushirika wa Tumbaku (TTCA), Muungano wa Vyama vya Ushirika wa Akiba na Mikopo (Sccult), Vyama Vikuu vya Ushirika vya KNCU (1984) Ltd, Wetcu Ltd, Cetcu Ltd na Tanecu Ltd.
Vyama vingine n vya ushirika vya msingi 192 vinavyohusika na zao la tumbaku Mkoa wa Tabora na 14 vya Mkoa wa Singida,vyama vya ushirika vya msingi vya mazao (Amcos) 97 mkoani Pwani, 18 vya Wilaya ya Tunduru, vyama vya ushirika wa Akiba na Mikop vya Mzalendo, Kurugenzi Njombe, Mpwapwa Teachers, Fune, Gogogo, Luiche, Kisesa na Chawampu Amcos.
Kuhusu Uwakilishi wa Bodi ya Kahawa, Waziri Chiza alisema kumekuwa na hoja ya uwakilishi kwenye bodi hiyo na kanuni kuruhusu uuzaji wa kahawa mbichi na kwamba, tayari amefanya mabadiliko katika bodi.
“Serikali imefanya marekebisho katika Bodi ya Wakurugenzi wa Kahawa kwa kuteua bodi mpya ya wakurugenzi. Pia, rasimu ya marekebisho ya kanuni za sheria ya kahawa ya mwaka 2012 inayozingatia kudhibiti uuzaji kahawa mbichi na kuhakikisha kahawa yote inayouzwa inachakatwa imetayarishwa,” alisema.
Waziri Chiza alisema tathmini ya utekelezaji wa ASDP imeonyesha kuwapo kwa fedha ambazo hazikutumika katika miaka ya nyuma ngazi ya halmashauri.
Alisema hadi Desemba 2012 takriban Sh25.8 bilioni zilizotengwa kwa ajili ya miradi ya umwagiliaji zilikuwa hazijatumika.
“Sababu kubwa zilizochangia fedha hizo kutotumika ni upungufu wa wahandisi na mafundi sanifu wa umwagiliaji na mtiririko mbaya wa fedha,” alisema.
Next Post Previous Post
Bukobawadau