Bukobawadau

WAZIRI SITTA:Katiba mpya izuie rais kubeba familia yake

WAZIRI wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta amewasihi Watanzania wazuie katiba mpya isitoe rais dikteta na mwenye kutumia madaraka vibaya kwa kuinufaisha familia yake au jamaa walio karibu naye.
Sitta amesema analiona taifa linaelekea kwenye hatari kubwa, kwamba baadhi ya viongozi wanahangaika kuingiza mambo binafsi yenye maslahi ndani ya rasimu ya katiba mpya badala ya kuangalia utaifa.
“Hawa wanaoingiza mambo yao binafsi si watu wazuri kwa taifa letu, tukiwaacha waendelee na mchezo wao katiba mpya itakuwa chungu sana kwetu,” alisema.
Sitta alisema Watanzania wanatakiwa kutengeneza katiba nzuri itakayomzuia rais atakayechaguliwa kuwa mroho na kutumia madaraka yake kuinufaisha familia yake au jamaa walio karibu naye.
Kiongozi huyo alitoa onyo hilo jana jijini Dar es Salaam alipokuwa akifungua mkutano wa Baraza la Taifa la Vijana la Rasimu ya Katiba mpya unaotarajia kumalizika kesho.
Sitta alisema misingi ya utawala bora ndiyo silaha kubwa ya kuhakikisha viongozi wanaochaguliwa hawafanyi kazi kwa udikteta au masilahi binafsi.
“Nawasihi ndugu zangu tusikubali katiba mpya ijayo ikachezewa na wajanja wachache maana tukifanya hivyo kuna hatari tukatengeneza rais na serikali ya kidikteta” alisema.
Alisema kwa muda mrefu Tanzania imekuwa na historia ya kufuata misingi ya utawala bora hivyo ni vizuri jambo hilo likaendelezwa.
Sitta alibainisha kuwa katiba ni muhimu kwa mustakabali wa Tanzania na lazima wananchi wajenge utamaduni kuiheshimu na kuilinda huku wakiwaepuka watu wanaotaka kuwania madaraka kwa masilahi binafsi.
“Tunahitaji kiongozi mwenye kujali masilahi ya Watanzania, hatuhitaji yule mwenye kujali tumbo lake au la familia yake, haya yote yatafanikiwa kama tutaweka vipengele kwenye katiba yetu itakayowabana watu wa aina hiyo,” alisema.
Muundo wa Muungano
Waziri Sitta alisema rasimu ya katiba mpya ilenge kupunguza gharama za uendeshaji wake kwa sababu Watanzania ni masikini na wanahitaji maendeleo.
Alibainisha kuwa hakubaliani na mapendekezo ya rasimu ya katiba mpya iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba ya uwepo wa mawaziri 15 kwenye Serikali ya Muungano ilhali mambo ya Muungano yapo saba.
Aliongeza kuwa wabunge 150 na mawaziri 15 wa Serikali ya Muungano ni kutapanya fedha za walipakodi wanadidimia kwenye lindi la umasikini.
“Wananchi wanahitaji maendeleo, tujikite kupunguza matumizi na mbwembwe mbwembwe zisizo na tija kwa taifa,” alisema.
Alisema nchi nyingi za Afrika zimekuwa zikisuasua kupiga hatua kwenye maendeleo kwa kuwa fedha nyingi zinatumika kwenye uendeshaji wa serikali badala ya kupelekwa katika sekta zenye kuwainua kiuchumi wananchi.
Apinga marais watatu
Sitta alipendekeza kuwa kama muundo wa serikali tatu unaopigiwa debe na baadhi ya watu utafanikiwa ni vema vyeo vya marais wawili wa Zanzibar na Tanganyika vikafutwa ili kuiepusha nchi kuwa na marais watatu.
Alisema nchi mbalimbali zitaicheka Tanzania kama itakuwa na marais watatu ambao wote inaweza ikatokea wakakutana nje ya nchi.
“Tutakuwa watu wa ajabu sana huko kwa wenzetu, yaani sisi masikini halafu tuna marais watatu? Hizi gharama tunazotaka kumtwishwa mwananchi za nini?” alihoji.
Alisema kama kutakuwa na serikali tatu ni vema kukawepo na rais mmoja wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na wengine wakapewa majina mengine kama Makamu wa Rais au Waziri Mkuu.
Sitta aliongeza kuwa hapingi muundo wa serikali tatu, bali hakubaliani na hoja ya uwepo wa marais watatu.
Aliongeza kuwa hoja ya kutaka marais hao watatu inashabikiwa na wenye uroho wa madaraka, wanaodhani inaweza kuwa njia rahisi kwao kufikia malengo yao ya kisiasa.
“Kuna watu wana kiu kubwa ya kuitwa mheshimiwa rais, ndiyo maana wanapigia debe uwepo wa marais watatu, nawaona ni wabinafsi tu hawana jambo jingine,” alisema.
Next Post Previous Post
Bukobawadau