Bukobawadau

Bastola nje nje, zauzwa mitaani nchini

 Dar/Mikoani. Kukithiri kwa rushwa miongoni mwa baadhi ya maofisa wa Jeshi la Polisi nchini, kumesababisha silaha ndogondogo hususan bastola kumilikiwa na watu wasio na sifa nchini.
Uchunguzi wa kina wa gazeti hili katika mikoa mbalimbali nchini ikiwamo iliyopo mipakani inaonyesha kuwa, bastola zinamilikiwa na watu bila ya kufuata taratibu na nyingine zikitumika kwa ajili ya kufanyia uhalifu.
Hivi sasa hata vibaka ambao awali walikuwa wakitumia visu na mbao za misumari kupora mali za watu, sasa wanafanya uhalifu huo kwa kutumia bastola.
Mbali ya vibaka kumiliki bastola, wahamiaji haramu walioko ndani ya mipaka ya Tanzania inayopakana na Rwanda, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, wanadaiwa kuingiza silaha nzito, ambazo zinatumika kwa ajili ya matukio ya kihalifu.
Jinsi silaha zinavyopatikana
Uchunguzi unaonyesha moja ya njia ambayo imekuwa ikitumika watu wasiokuwa na sifa kupata bastola au bunduki ni kutumia mawakala au baadhi ya maofisa polisi, waliopo katika mikoa mbalimbali ambao huwatafutia vibali vya kumiliki.
Utaratibu wa kawaida ni kwamba waombaji wanaotaka kumiliki silaha ni lazima wajadiliwe katika kamati za ulinzi na usalama za mtaa au kijiji, wilaya na mkoa na kuhojiwa ili kujiridhisha kama mwombaji ana sifa.
Mkoa wa Kilimanjaro
Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa baadhi ya vijana wadogo wakiwamo wafanyabiashara, wana vibali vya kumiliki bastola mkoani Kilimanjaro na hawakupitia mchakato huo.
“Unataka kibali cha kumiliki bastola? Una milioni moja na nusu nikuunganishe na jamaa Dar anakufanyia process (mchakato) zote anakuletea kitabu,”alisema kijana mmoja jina tunalihifadhi.
Kwa mujibu wa vyanzo vya kuaminika, baadhi ya maofisa wa Jeshi la Polisi makao makuu na wale waliopo mikoani, wamegeuza suala la kumilikisha watu silaha kama mradi wa kujitajirisha.
“Tatizo la nchi hii ni corruption (rushwa) kwa sababu unajiuliza hivi hawa vijana wadogo kabisa wanamiliki bastola na hawakujadiliwa kwenye kikao chochote,”alidokeza mfanyabiashara mmoja.

Uchunguzi zaidi umebaini kuwa wapo wanaojiita wafanyabiashara, lakini ni matapeli wa kimataifa nao wamepewa vibali vya kumiliki bastola na wakati mwingine huzionyesha waziwazi wakiwa baa.
“Ufyatuaji wa risasi siku hizi umekuwa holela…ninavyofahamu ukifyatua hata risasi moja, lazima uandikishe maelezo polisi ulifyatua kwa sababu zipi siku hizi lakini hilo halifanyiki,” ilidokezwa.
Inadaiwa kuwa kutokana na kuwapo kwa ulegevu wa vyombo vya dola hususan Polisi, baadhi ya wamiliki wa bastola hizo wamekuwa wakizikodisha kwa majambazi ambao huzitumia katika uporaji.
Kwa mujibu wa uchunguzi huo, ulegevu huo katika kudhibiti matumizi ya silaha, kumetoa mwanya kwa baadhi ya wamiliki kukodisha bastola zao na kurudishiwa baada ya matukio pasipo kugunduliwa.
Dar es Salaam
Uchunguzi wa Mwananchi Jumapili unaonyesha kuwa kuongezeka kwa idadi ya watu wanaomiliki silaha kinyume cha sheria jijini Dar es Salaam, kumeongeza matukio ya uhalifu.
Baadhi ya watu ambao wapo karibu na maofisa wa polisi makao makuu wamekuwa wakitumia nafasi hiyo kuwatafutia watu vibali vya kumiliki silaha.
Watu hao wamekuwa wakijipatia Sh600,000 hadi Sh900,000 kwa kibali kimoja cha kumiliki silaha.
Hali hiyo imesababisha wahalifu wengi wakiwamo vibaka mitaani kumiliki silaha ambazo wanazitumia kupora watu mitaani.
Mussa Radhamn Mkazi wa Kigogo jijini Dar es Salaam anasema hali ni mbaya, hivi sasa hata vijana wasiokuwa na kazi wanamiliki silaha.
Alisema hivi sasa huwezi kupita uchochoroni kuanzia saa 4:00 usiku, lazima utakutana na vibaka wakiwa na bastola.
Wahamiaji haramu
LIMEANDIKA GAZETI LA MWANANCHI JUMAPILI SEPTEMBA 1,2013
Next Post Previous Post
Bukobawadau