Bukobawadau

JK hataki kuongeza muda

Dar es Salaam. Waziri wa Katiba na Sheria, Mathis Chikawe amesema Rais Jakaya Kikwete hana mpango wa kuongeza muda wa uongozi wake baada ya 2015 kama baadhi ya wanasiasa wanavyodai.
Kadhalika, waziri huyo amesema hakuna sheria inayomlazimisha Rais kusaini muswada wa sheria yoyote inayopitishwa na Bunge na wala inayoweka muda maalumu wa kutekeleza wajibu huo.
Akizungumza na gazeti hili jana, Chikawe alisema kwa vyovyote vile Rais Kikwete hawezi kuongeza muda wa kuwapo kwake madarakani kwa kuwa anaheshimu Katiba ya nchi iliyomuweka madarakani.
Waziri huyo alitoa kauli hiyo baada ya kutakiwa na gazeti hili kuzungumzia madai ambayo yamekuwa yakirudiwa mara kwa mara na Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba kwamba amenasa taarifa za siri za kuwapo kwa mipango ya kuongeza muda wa Serikali ya sasa kukaa madarakani.
“Ngoja nikwambie ndugu yangu, watu wanaongea tu, kwanza Rais mwenyewe hana mpango huo, anasema kazi aliyonayo ni ngumu na haoni sababu ya kuongeza muda,”alisema Chikawe na kuongeza:
“Mara zote ukizungumza naye anasema tuharakishe mchakato wa Katiba na ikibidi tuingie katika Uchaguzi Mkuu wa 2015 kama Katiba yetu inavyosema kwa kuwa kazi aliyofanya inatosha kabisa.”
Mapema mwezi Mei mwaka huu, Profesa Lipumba alisema kutokana na wasiwasi kwamba mchakato wa Katiba Mpya hautakamilika 2014, hivyo Uchaguzi Mkuu hautaweza kufanyika.
Kuhusu hatima ya Uchaguzi Mkuu iwapo Katiba Mpya itaanzisha mfumo wa Serikali tatu, Chikawe alisema: “Wananchi wasiwe na wasiwasi ikifika wakati huo kila kitu tutajua, lazima tutakuwa na sheria ya mpito ambayo itaweka mambo sawa mpaka kutufikisha katika Uchaguzi Mkuu.”
Rais kusaini muswada
Chikawe pia alizungumzia hatima ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Mpya ambapo alisema hakuna sheria inayomlazimisha Rais kusaini miswada inayopitishwa na Bunge.
“Hakuna sheria inayomlazimisha Rais asaini wala kumpa muda wa kusaini, mwenyewe anatumia busara na hekima tu katika kusaini sheria,”alisisitiza Chikawe.
Kauli ya Chikawe imekuja siku chache baada ya wenyeviti wa vyama vya CUF, NCCR -Mageuzi na Chadema kutoa tamko la kumtaka Rais Kikwete asisaini muswada huo mpaka pale yatakapokuwapo maridhiano ya wadau muhimu kuhusu muswada huo. Alisema kwa kutokusaini muswada huo, kunaweza kukaleta tafsiri mbili; kwanza ni wale wanaoweza kutafsiri kuwa ni dharau kwa wabunge waliopitisha muswada huo, kwamba walichofanya si sahihi na hakina maana.

Hoja ya pili alisema kwa kutosaini pia kunaweza kuzidisha msukumo kwa wanachama wa chama chake, lakini pia kutoka kwa wananchi ambao wanasubiri kwa hamu utekelezaji wa sheria hiyo.
Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa 2013 ambao ulipitishwa na mkutano wa Bunge uliopita baada ya mvutano mkali, umeendelea nje ya Bunge, huku kukiwa na madai kwamba ulipitishwa ukiwa na marekebisho ambayo yalifanyika kinyume na maoni ya wadau.
Madai mengine ni kwamba wabunge wa CCM waliongeza baadhi ya mambo kupitia majedwali ya marekebisho, hivyo kutoa mwanya kwa Serikali inayoongozwa na chama hicho kupitia kwa Rais kuwa na mamlaka zaidi ya uteuzi wa wajumbe husika.
Septemba 6 mwaka huu, wabunge wa CCM walitumia wingi wao kupitisha muswada huo katika mkutano wa Bunge ambao ulisababisha tafrani kiasi cha Mbowe na Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi kutolewa nje ya Bunge kwa amri ya Naibu Spika, Job Ndugai.
Katika tafrani hiyo, baadhi ya wabunge wa upinzani walirushiana makonde na askari wa Bunge, huku wabunge wote wa upinzani, isipokuwa Mbunge wa Vunjo (TLP), Augustine Mrema, wakisusia vikao vya muswada huo.
CHANZO;Mwananchi
Next Post Previous Post
Bukobawadau