Bukobawadau

LILE SAKATA LA MAITI MULEBA WANANCHI WAVUNJA JENEZA NA POLISI WAJERUHI MWANAHABARI!


 Jeshi la polisi wilayani Muleba mkoani Kagera  limemshambulia mwandishi wa habari wa gazeti la Mwananchi na Radio Kwizera  mkoani humo  wakati akifanya shughuli zake katika kituo cha afya cha Kaigara ambapo  wananchi walikuwa wakivunja chumba cha kuhifadhia maiti katika kituo hicho
Askari polisi waliambatana na mkuu wa wilaya ya Muleba Lambris Kipuyo ambapo walikuwa wakipiga mabomu ya machozi kutawanya wananchi na ndipo walimkuta mwandishi huyo  Shaaban Ndyamukama  akipiga picha za matukio  na kumtembezea kipigo kikali wakidai aliingia kufanya kazi bila ruhusa yao
Mwandishi huyo amejeruhiwa kwa virungu katika mguu wake wa kulia sehemu ya chini ya goti na bega la kushoto ambapo alinyanganywa kamera yake, recorder na simu yake ya mkononi huku wananchi wakipigwa mabomu ya machozi kuwatawanyika  kwa kuondoka eneo la tukio

Mwandishi huyo alilazimika kumweleza mkuu wa wilaya kuwa awaruhusu polisi kumwachia kwani  hana hatia yoyote katika tukio hilo lakini askari polisi walimburuza kadi kwenye gari la polisi na kushikiliwa kwa muda  hadi wananchi waliokuwa katika eneo hilo kumtaka DC Kipuyo amwachie mwanahabari huyo.
Papo hapo wananchi waliziba barabara  kushinikiza mwandishi kuondolewa katika gari la polisi ambapo mkuu wa wilaya licha ya kumpa maneno ya pole  alisema hiyo ni sehemu ya kazi
 “Pole kwa hayo nimewaagiza askari wakupatie vifaa vyako na uendxelee na shughuli zako a kawaida na usalama katika eneo hili utakuwepo na mwili wa marehemu utapelekwa kuzikwa panapohusika”Alisema Kipuyo
Katika kuhakikisha  anafanya kazi zake kwa usalama alilazimika kwenda katika kituo hicho cha afya Kaigara na kupata matibabu ambapo alikaa mpaka saa 8 mchana na kuruhusiwa  kwenda kupumzika mjini Muleba.

 Awali katika tukio hilo wananchi wenye hasira kali  wa  Kata ya Muleba Kijiji cha Bukono  wamevunja mlango wa  chumba cha kuhifadhi maiti cha kituo cha afya kaigara wilayani humo  mkoani Kagera wakitaka kuchukua maiti ya msichana wa miaka (16 ) aliyepoteza maisha mkoani Arusha alikokuwa akifanya kazi za ndani
Msichana huyo aliyetajwa kwa jina la Asera Triphone, alikuwa akifanya kazi za ndani kwa mama mmoja aliyetambulika kwa jina la Valentina Maxmilian   ambapo alimchukua kutoka kwa wazazi wake mzee Triphone Basheka  na mkewe   Georgina Triphone
Wananchi walifikia uamuzi huo  wa kubomoa chumba hicho baada ya kudaiwa kuwa  mwili uliokuwa katika jeneza ulikuwa umenyofolewa baadhi ya viungo vya mwili kama sehemu za siri mkono na sehemu ya mguu kuwa imekatwa kwa kile kilichosemwa ni imani za ushirikina
Inasemekana mara baada ya  kufikishwa mkoani  Arusha binti huyo alianza kufanya kazi  za ndani   na katika kufanya kazi hizo za ndani alipoteza maisha katika mazingira ya kutatanisha na mwili wake kurudishwa juzi kwa wazazi wake
Akielezea tukio hilo mama mzazi wa mtoto huyo Georgina Triphone alisema kwamba aliombwa mtoto wake kwenda kufanya kazi za ndani  januari mwaka 2013  na alikuwa akipata mawasiliano ya simu  kutoka kwa mwajiri wake.
Georgina,alisema tangu Juni 12 mwaka huu amekuwa, akipokea simu tofautitofauti kuhusu binti yake kuwa atakuja hivi karibuni kusalimia kupitia kwa mwajili wake.

 Alisema Juni 13 mwaka huu  ambayo ilikuwa siku ya Ijumaa  alipigiwa simu na mwajiri wa binti yake na kumueleza kuwa mwanaye anaumwa na baada ya muda wa masaa  mawili alimueleza mgonjwa amefariki dunia
 Hata hivyo wananchi walifungua jeneza na kumuona marehemu kuwa ni mtoto wa mama huyo lakini walishtuka baada ya kuona mwili huo ukiwa umevalishwa soksi mikononi na miguuni.
Shangazi wa marehemu katika ukoo aliyetambulika kwa jina la mama kishina alisema baada ya kuona hivyo waliamua kumvua hizo soksi na kukuta mwili huo ukiwa umeunguzwa kwa moto mikononi na miguuni huku kichwa kikiwa na alama za kukatwa na kitu chenye incha kali.
Alisema walipoendelea kuukagua mwili wa marehemu waligundua tundu lililokuwa kwenye eneo la moyo likiwa limefunikwa kwa pamba na pia  marehemu aliondolewa meno manne ya juu na kuwa sehemu zake za siri zilikuwepo.
Pamoja na hayo mkuu wa wilaya ya Muleba ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na uslamaLambris Kipuyo  amekanusha taarifa hizo akidai wakati binti  akipelekwa Arusha wanafamilia walijua matatizo yake ya kuugua kifafa
 
 Alisema  wananchi wajihadhari na kutoa taarifa za uongo na za uchochezi na kwamba  vyombo vya dola kujipanga kutafuta ukweli wa tukio hilo lakini katika hali isiyokuwa ya kawaida  mwili wa marehemu ulifikia kwao na mwajiri wake  kijiji cha  Buyango na kupelekwa  kwa wazazi kesho yake na kuzua taflani kubwa kwa jamii .
Next Post Previous Post
Bukobawadau