KDCU Ltd. Kagera nao walia na ufisadi
Na Prudence Karugendo
WANA ushirika
wa Chama kikuu cha Ushirika cha Karagwe District Co-operative Union (KDCU LTD.)
cha wilaya za Karagwe na Kyerwa, mkoani
Kagera, nao wameanza kulia na hujuma za kifisadi zinazofanywa na uongozi wa
chama chao hicho cha ushirika dhidi ya wanaushirika wake, wakulima wa zao la
kahawa katika wilaya hizo mbili.
Ufisadi
unaofanyika katika chama hicho unawafanya wakulima hao wa kahawa wafikirie
jambo moja kati ya mawaili, ama kuachana na ukulima wa kahawa na kutafuta zao
mbadala la biashara au kuachana kabisa na mfumo wa ushirika ili waanze kuuza
mazao yao ya biashara kwa makampuni binafsi yanayowalipa pesa nzuri kwa muda
muafaka bila kuwakopa.
Wanasema
makampuni binafsi yanayoshughulika na ununuzi wa mazao yamedhihirisha ubora
wake kutokana na kutokuwa na urasimu uliojaa ufisadi kama unavyojionyesha kwenye ushirika.
Eti
mpangilio wa ushirika, kuanzia kwa mwenyekiti, meneja, Bodi mpaka kwa
wawakilishi wa vyama vya msingi, ni urasimu
mtupu unaokifanya chama kikuu cha ushirika kitumie karibu mapato yake yote, na
hata pesa ya kukopa, kwa ajili ya uendeshaji wa mpangilio huo mbovu usiojali
maana ya uwepo wake kwa wakulima. Kwahiyo eti kinachofanywa na ushirika ni
kumfanya mkulima, ambaye ndiye uti wa mgongo wa chama cha ushirika, aambulie
patupu!
Baada ya
wanaushirika hao wa Karagwe na Kyerwa kutoa madai hayo, wanayosema
wameishayafikisha hata kwa Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, na kuyapa
kichwa cha habari “Okoa jahazi la wakulima unusuru KDCU Ltd. kabla ya
kufilisika” bila kuona mafanikio yoyote, ndipo nikawaomba wanionyeshe ushahidi
wa hicho wanachokisema.
Bila kwenda
mbali wakanitolea ripoti ya makisio (Bajeti) ya KDCU Ltd. ya mwaka 2014 – 15.
Wanasema
pamoja na KDCU kupata hasara ya sh. 1, 321, 679, 652/= katika msimu uliotangulia
wa 2013 – 14, bado uongozi wa chama hicho, bila kujali hasara hiyo ambayo ni pamoja na deni la sh.1,237,000,000
la benki ya CRDB,
unapanga bajeti ya kukiendesha chama hicho iliyo na mambo mengi yasiyokuwa na
umuhimu wowote kwa chama chenyewe na kwa wakulima, isipokuwa kwa kuongeza
gharama inayounufaisha uongozi tu pamoja na wanaoutetea na kuulinda ufisadi
ndani ya ushirika huo.
Eti chama
chao, kwa mujibu wa makisio ya mwaka 2014 – 15, ambayo nakala yake ninayo, KDCU
Ltd. inafikia kuwaweka kwenye bajeti
hata watu wa nje, ambao sio wanaushirika, ila wakiwa na maslahi binafsi kwa
uongozi wanaoukingia kifua ili usiwajibishwe na wanaushirika au mamlaka ya juu
kinchi. Watu hao ni kama Mrajis Msaidizi wa Mkoa, maafisa ushirika wa wilaya na
wanaoitwa wageni rasmi.
Wakati hayo
yakifanyika kipato cha mkulima, mwanaushirika, kinazidi kufifia, kisingizio kikubwa kikiwa ni kwamba bei ya
kahawa inateremka kwenye soko la dunia!
Gharama hizo
zilizo kwenye makisio ya mwaka huu ni pamoja na kumpangia mwakilishi wa chama
cha msingi nauli ya sh. 60, 000/= kwenda na kurudi kwenye mkutano mkuu, ambayo
kwa basi ni sawa na nauli ya kutoka Karagwe kwenda Dar es salaam, wakati
mazingira ya wilaya za Karagwe na Kyerwa hayana umbali wa aina hiyo na hivyo
kuyafanya makisio hayo yasionyeshe uhalali wowote kwa nauli hiyo.
Maafisa
ushirika, ambao ni waajiriwa wa serikali, wakiwa wanalipiwa kila kitu na
mwajiri wao wanapofanya kazi zao, nao eti wanaingizwa katika mahesabu ya chama
cha ushirika ambapo nao kinawapangia bajeti kana kwamba kimewaajiri chenyewe!
Tena eti kwenye bajeti hii, kama inavyoonekana kwenye ripoti ya makisio,
wamepigiwa hesabu ya watu wawiliwawili!
Vilevile
Mrajis Msaidizi wa Mkoa amepangiwa bajeti ya kwake inayoonyesha kwamba safari
peke yake, Bukoba hadi Kayanga, Karagwe, kwenda na kurudi ni sh. 400, 000/=,
ambayo ni zaidi ya nauli ya ndege kati ya Bukoba na Mwanza! Na ikumbukwe kwamba
hakuna usafiri wa ndege kati ya Bukoba na Kayanga, na hata kama ungekuwepo
nauli yake haiwezi kuwa hiyo, sawa na ya kwenda Mwanza, kutokana na tofauti ya
umbali.
Mbali na
usafiri huo wa kutisha, Mrajis Msaidizi pamoja na maafisa ushirika, nao
wanapangiwa posho za vikao sh. 50, 000 x 2 x 4, posho za kujikimu sh. 50, 000 x
3 x 4 na kuongezewa asilimia 20 ambazo hazijulikani ni kwa ajili ya nini!
Wanaushirika
wa Karagwe na Kyerwa wanajiuliza ni kwa nini gharama hizo zibebwe na chama chao
wakati watu hao wanatimiza majukumu yao ambayo ndiyo yaliyowafanya wakaajiriwa
na serikali? Pia wanaushirika wanauliza,
watu hao ni waajiriwa wa serikali kweli au wanafanya kazi ya kujitolea?
Eti kama wameajiriwa na serikali inakuwaje sasa
wanalipwa na chama cha ushirika kwa kazi ambayo serikali inawalipa pia
mishahara na posho kwa kutumia kodi za wanaushirika ikiamini kwamba
inawawezesha wananchi kuendesha kilimo chao? Na kama watu hao wanafanya kazi ya
kujitolea kwa nini ushirika uingie kwenye gharama kana kwamba umewakodi?
“Na vile vile, kama KDCU kilipata hasara kubwa katika
misimu miwili iliopita na kuwa na madeni makubwa ya benki, kwa nini uongozi
umepanga kutumia Sh. 110,000,000 kila mwaka kwa mikutano mikuu ya kifahari ambapo
kila mjumbe analipwa Sh.180,000 kwa siku? Aidha, inawezekanaje leo chama hicho kipange kuwalipa
wajumbe wake 8 wa Bodi kiasi cha sh. 16,000,000 kama “bonus” bakshishi?
Kitapata fedha hizo kutoka wapi kama sio kutumia vibaya fedha za mkopo kutoka
benki za kununulia kahawa?”, wanauliza wanaushirika hao.
Kwa kadri
mambo yalivyo, kumejengeka hisia kwa wanaushirika hao wa Karagwe na Kyerwa za
kwamba madai ya kushuka kwa bei ya kahawa katika soko la dunia si ya kweli. Wao
wanaona hicho ni kiinimacho tu, eti kiuhalisia bei ya kahawa inashushwa na chama chao kikuu
cha ushirika kutokana na chama hicho, kwa njia za kifisadi, kujiingiza kwenye gharama zisizo na manufaa
yoyote kwa wakulima wala kwa chama chenyewe.
Wanatoa
mfano huo wa maafisa ushirika pamoja na Mrajisi Msaidizi wa mkoa kuonekana
kwenye orodha ya wanaopaswa kulipwa na chama chao (payroll), kama kitu
kimojawapo kinachowafanya wapate bei ya chini katika zao lao la kawaha huku
wakidanganwa kuwa bei inashuka kwenye soko la dunia.
Jambo
wanalojiuliza ni kwamba kama kweli bei ya kawaha inashuka kwenye soko la dunia,
kwa nini kushuka uko kumuathiri mkulima peke yake bila kuugusa mfumo mzima wa
chama cha ushirika? Wanasema haiwezekani chama cha ushirika kikawapangia nauli
wajumbe wake ya sh. 60, 000/= kwa umbali
siozidi km. 50, wakati nauli hiyo inatosha kumsafirisha mtu kwa umbali
usiopungua km. 1500, sawa na kutoka Karagwe kwenda Dar es salaam , wakati
hakina mapato ya uhakika.
Eti kwa nini
KDCU inaangalia kushuka kwa bei ya kahawa kwenye soko la dunia wakati wa
kumlipa mkulima tu, na hailizingatii
hilo wakati wa kupanga “matanuzi” yake? Eti kwa nini wakati wa kupanga gharama
za matumizi chama hicho kinajiona kinao
utajiri mkubwa kupindukia na hivyo kuamua kupandisha gharama ya kila kitu kwa zaidi ya mara 10 wakati hali
hiyo haimnufaishi mkulima?
Wanachoshindwa
kukielewa wanaushirika wa KDCU Ltd. ni kwamba katika hali hiyo inayoonyesha
wazi kuwa chama hicho kinawahonga wahusika wanaopaswa kukisimamia, kuanzia
wawakilishi wa vyama vya msingi mpaka kwa maafisa ushirika na Mrajisi Msaidizi,
watu hao wanawezaje kukisimamia na kuhakikisha kinawatendea haki wakulima?
Maana eti
kama tayari chama kikuu kimeisha wafumba macho na kuwafunga midomo watu hao ili
wasiangalie wala kusema chochote, kusudi wanaushirika waendelee kuteseka na
umasikini ndani ya utajiri wao huku viongozi wa ushirika wakineemeka,
inaonyesha nini kama sio kuwakaanga wanaushirika kwa mafuta yao?
Jambo hilo
ndilo linalowaleta kwenye mawazo ya kwa nini ushirika uendelee kuwepo? Kwamba
kama hali ndiyo hiyo, kuhenyeka kwa ajili ya watu fulani walio wachache, wasio
na uadilifu, kwa nini wakulima wasiuze kahawa yao kwa makampuni binafsi
yanayoiona na kuijali thamani ya zao la kahawa huku wakiwathamini pia
wanaolizalisha zao hilo?
Pamoja na
malalamiko hayo ya wanaushirika wa Karagwe na Kyerwa, bado wanakisifu chama
chao hicho kwa kitendo cha kuonyesha uwazi na ukweli, japo ukweli huo unauma.
Wanasema KDCU inakubali kuonyesha kwamba Mrajis Msaidizi, pamoja na maafisaushirika
wa wilaya, wapo kwenye orodha ya wanaolipwa na chama hicho.
Hiyo ni
kwamba waajiriwa hao wa serikali wanalipwa mara mbili kwa kazi ileile moja waliyoajiriwa
kuifanya, kitu ambacho kinapingana na
sera ya utumishi wa umma.
Kwahiyo eti
kama ushirika unakufa pasitafutwe mchawi kwingine, eti mchawi ni watumishi hao
wa serikali walioajiriwa kuusimamia na kuulinda ushirika ili kuhakikisha
unashamiri na kuimarika. Eti sasa watu hao ndio wanaogeuka na kuuelekeza kuzimu.
Swali ni kwa nini serikali inawakubalia
wafanikishe uovu wao huo?
0784 989 512