Bukobawadau

MCHEZAJI WA SIMBA AFARIKI HUKO UGANDA KUFUATIA BAO LA FRANK LAMPARD

Fahad Musana, ambaye ni shabiki wa kutupwa wa klabu ya soka ya Chelsea, amefariki dunia baada ya mchezaji wa zamani wa klabu hiyo, Frank lampard, kuifungia Manchester City bao la kusawazisha, katika pambano lililopigwa jana baina ya timu hizo mbili.
Musana, mwenye umri wa miaka 24, na ambaye alikuwa mcheza kandanda la kulipwa nchini Uganda, alikuwa akitizama mechi hiyo iliyovuta hisia za mashabiki wengi katika kona mbalimbali za dunia, na alianguka na kuzimia mara baada ya Lampard kusawazisha bao, ikiwa ni dakika chache sana tangu aingie kutokea benchi, katika dakika za lala salama.
Alithibitishwa kuwa amefariki baada ya kuwasili katika hospitali ya kijeshi ya Bombo, na rafiki wa karibu wa marehemu amenukuliwa na vyombo vya habari akisema “Jamaa, amekuwa ni shabiki wa kweli wa Chelsea, ambaye angeweza kufanya lolote lile kwa ajili ya klabu hiyo. Tulifanya naye mazoezi asubuhi ya jumapili, na hata mchana tukala chakula cha mchana pamoja, hakika inasikitisha”
Tukio hili la kusikitisha, limethibitishwa na Shirikisho la vyama vya soka nchini Uganda (FUFA), ambalo limetoa tamko lake kufuatia mkasa huu wa kushtusha.
“FUFA, limekumbwa na mshtuko baada ya kupokea taarifa za kifo cha ghafla cha mchezaji wa klabu ya Simba ya Uganda, Misana Fahad, katika hospitali ya Bombo. Mwili wa marehemu bado uko hospitalini hapo, na taratibu za mazishi zinaandaliwa na taarifa zitatolewa baadae”, sehemu ya taarifa ya FUFA imesomeka hivyo.
Hii si mara ya kwanza kwa mashabiki wa soka kufariki kufuatia timu wanazozishabikia kushindwa kuibuka na ushindi katika mechi zao. Kumbukumbu za hivi karibuni sana kwa ukanda wetu wa Afrika Mashariki na Kati, ni za shabiki mwingine wa soka aliyefariki dunia msimu uliopita, baada ya timu aliyokuwa akiishabikia ya Manchester United kupoteza moja ya mapambano yake, ilipokuwa chini ya kocha David Moyes
Next Post Previous Post
Bukobawadau