Bukobawadau

UTAPELI WA KANISA LA KIMAREKANI

Na Prudence Karugendo
KUNA  usemi wa kwamba wageni walikuja barani kwetu, Afrika,  kwa kutumia ushawishi wa neno la Mungu na kuwaambia wenyeji “fumbeni macho tusali”,  wenyeji walipofumbua macho kila kitu kilikuwa kimeporwa, ardhi, maliasili na kila kilichokuwa kwenye uwezekano wa kusombwa na wageni hao!
Hiyo ni dhana iliyo na kila ukweli wa kimuonekano, sidhani kama kuna yeyote anayepingana nayo, lakini inaongelea wakati huo. Kwa wakati huu wa dunia ya kiustaarabu, kuheshimiana na kutendeana haki, sidhani kama kuna nafasi tena ya kuukumbatia usemi huo.
Ila kuna jambo moja la kusikitisha na kustaajabisha lililofanywa na Kanisa moja la Kimarekani, SDA, na kuonekana ni la kiutapeli kupitiliza kiasi kwamba nimelazimika kutengeneza makala haya kwa lengo la kuuliza ubalozi wa Marekani hapa nchi kama unakubaliana na kitu hicho, vinginevyo ubalozi huo utasaidie kutupatia ufafanuzi kuhusu jambo hilo lililofanywa na Kanisa hilo la nchini kwake.
Bwana mmoja, Mtanzania, jina limehifadhiwa kwa sasa,  aliajiriwa na Baraza Kuu la Kanisa la SDA Tanzania, tangu mwaka 1986 mpaka 1999,  alipohamishiwa kwenye kitengo cha kanisa hilo kilichoitwa International Health Foods of the SDA church (T) Ltd., ambacho kilitengenezwa kama Mfuko wa Hifadhi wa kanisa hilo.
Kati ya mwaka 2002 / 3 kulitokea kutoelewana kati yake na uongozi wa kitengo hicho kulikoishia kwenye Mahakama Kuu ya Tanzania, ambako mwaka 2008 mahakama hiyo ilitoa hukumu iliyompa haki Mtanzania huyo.
Matokeo yake kitengo cha International Health Foods of the SDA church kiliamuriwa na Mahakama  kumlipa malipo yake yote ya nyuma tangu mgogoro huo ulipoanzia mpaka ambapo kampuni ingewasilisha malipo hayo.
Katika kuhakikisha kwamba kitengo hicho kingetimiza amri ya mahakama bila matatizo yoyote Mtanzania huyo aliomba na kupewa amri ya mahakama ya kuzuia mali za International Health Foods of the SDA Church, kwamba iwapo kitengo hicho kingeshindwa kumlipa mafao yake kama ilivyoamriwa na Mahakama  basi mali hiyo iuzwe ili kufidia mafao yake hayo.
Licha ya amri hiyo ya mahakama,  kitengo hicho cha Kanisa la SDA, kiliuza kinyemela mali yake mwaka 2008 na kuihamishia pesa iliyotokana na mauzo hayo kwenye akaunti ya Baraza Kuu la SDA mjini Pittsburg Marekani. Na katika kufanya hivyo sio tu kwamba kitengo hicho kilikiuka sehemu ya hati ya makubaliano ya kuanzishwa kwake inayoeleza wazi kwamba iwapo kitavunjwa mali zake zote zitakabidhiwa kwa Kanisa la SDA Tanzania, bali pia kilikana uhusika wa pesa iliyotokana na uuzaji wa mali zake kulipia deni la Mtanzania huyo! Kwa sasa kitengo hicho kimefutwa.
Mwananchi huyo, huku akionyesha nyaraka mbalimbali zinazohusiana na suala hilo,  anasema kwamba amejaribu kulifuatilia suala lake  tangu mwaka 2008 mpaka mwaka 2013,  akieleza hatma yake  huku akilitaka Baraza Kuu la SDA kumtendea haki kulingana na maadili ya kanisa. Lakini cha kustajaabisha hakupokea jibu lolote toka kwa wahusika!
Ndugu yetu huyo anasema kwa vile pesa iliyopatikana  kutokana na mauzo yaliyofanyika  kinyume cha sheria, kwa vile mali hiyo ilikuwa imezuiwa kwa amri ya mahakama ya Tanzaia kama dhamana kwa malipo yake halali, iko kwenye akaunti ya Baraza Kuu la Kanisa la SDA nchini Marekani, ndiyo maana anataka Baraza hilo ambalo, aliyekuwa mwajiri wa wake  ni kitengo chake,  lifanye  mpango wa kumlipa madai yake hayo.
Katika kuhangaika huku na huko, ndipo , kupitia akafanikiwa kupata mawasiliano na Mwanasheria Mkuu wa Baraza Kuu la Kanisa la SDA,  nchini Marekani. Baada ya kumweleza kisa chote mwanasheria huyo akajibu kwamba kitengo alichokuwa ameajiriwa  Mtanzania huyo kilianzishwa kama kampuni ya Kitanzania inayojitegemea, na  yenye ukomo wa madeni, “Limited liability company”. 
Akaongeza kwamba kampuni hiyo ndiyo iliyokuwa mwajiri wa mtu huyo, na kwamba ndiyo iliyomwachisha kazi kabla ya kusimamisha shughuli  zake na baadaye, kwa muda mfupi,  kufutwa kabisa hata kabla ya Mtanzania huyo kukata rufaa. Mwanasheria huyo akasisitiza kwamba madai ya mwajiriwa huyo  ni dhidi ya kampuni hiyo ambayo haipo tena,  na sio dhidi ya Kanisa la SDA la Marekani.
Jambo hilo ndilo linadhihirisha utapeli unaofanyika. Sababu tangu mwanzo kampuni hiyo ilianzishwa na kujulikana kama kitengo cha kanisa la SDA, na baada ya kuuzwa kwa mali yake na kampuni kufutwa pesa iliyopatikana  ilihamishiwa kwenye akaunti ya Baraza Kuu la Kanisa la SDA nchini  Marekani. Kwa nini kanisa liikane kampuni wakati linapokea pesa iliyotokana na mauzo haramu  ya mali ya kampuni hiyo likiiona pesa hiyo ni halali yake? Na kama linaona madai ya kuikana kampuni hiyo ni ya kweli halioni kwamba kuichukua pesa iliyotokana na kitu linachokikana kuwa ni utapeli?
Katika kumjibu Mwanasheria Mkuu wa Kanisa la SDA, Mtanzania huyo  alisema kwamba kampuni ya IHFA  ndiyo iliyokata rufaa katika Mahakama ya Tanzania dhidi ya uwamuzi wa awali uliompa haki zake, na wala sio yeye aliyefanya hivyo kama mwanasheria huyo  wa SDA anavyodai.
Mtanzania huyo  akaongeza kwamba, hatahivyo, Mahakama  ambako IHFA  ilipeleka rufaa kusudi  asipewe haki yake, ilitoa hukumu iliyokuwa inathibitisha usahihi wa hukumu ya mahakama ya awali, kwamba alipwe  haki zake zote.
Lakini wakati  anahangaika na masuala ya kimahakama,  IHFA Ltd. iliendelea na mipango  ya kuuza mali yake ilizokuwa zimeshikiliwa kwa amri ya mahakama na kufanikiwa kuiuza kinyemela  mwezi Julai, 2008.
Kitu kingine ni kwamba baadhi ya wadhamini wa IHFA Ltd. walikuwa ni maafisa waandamizi wa Kanisa la SDA toka makao makuu, Marekani,  kama inavyoonyeshwa kwenye hati iliyoanzisha kampuni hiyo ya kanisa.
Baada ya Mtanzania huyo kutoa maelezo hayo kwa mwanasheria wa Baraza Kuu la Kaniza la SDA hakuna jibu lililopatikana toka kwanasheria huyo wa kanisa zaidi ya kufanya kitu ambacho vijana wa kisasa wanakiita kuingia mitini! Mwanasheria huyo wa kanisa hakuendeleza zaidi  mawasiliano.
Hiyo inadhihirisha kwamba kilichofanywa na kanisa hilo la SDA kilidhamiriwa na kukusudiwa. Hivyo picha inayojitokeza ni ya kwamba baadhi ya makanisa yanakuja hapa  nchini kwa lengo la kuchuma tofauti na inavyodhaniwa kwamba yanaleta neno la Mungu. Sababu hakuna namna ambavyo Mungu anaweza kuelekeza kwamba nenda ukamuibie mwenzako.
Tutaona kwamba mtindo huo, kama ulioonyeshwa na Kanisa la SDA, hauna tofauti hata kidogo na dhana niliyoielezea mwanzo ya “walikuja wakasema fumba macho tusali, wenyeji walipofumbua macho kila kitu kilikuwa kimeporwa”!
Katika hali ya kawaida, hata kwa asiye na imani ya Kimungu, kumpora aliye fukara, masikini, ni jambo linalomwia gumu kulifanya, hata jambazi mzoefu anaona utata wa kufanya hivyo.
Kwahiyo kanisa hilo la SDA, kanisa la Kimarekani, taifa kubwa na tajiri kupindukia, linapofanya jambo la namna hiyo, utapeli katika nchi changa na masikini, linataka lionekaneje? Linaijengea picha gani nchi yake lilimoweka makao yake makuu?
Na je, Marekani kama nchi inayojiheshimu na kuheshimika inalitazama vipi jambo hilo linaloichafua kwa kuipaka matope? Ni kweli italiachia kanisa hilo liendelee na mtindo huo wa kukwapua penye kidogo na kuzidi kujaza penye kingi, palipojaa tayari?
0784 989 512
Next Post Previous Post
Bukobawadau