Bukobawadau

ALICHOKISEMA ZITTO KABWE LEO

MBUNGE wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe kupitia ukurasa wake wa facebook, amesema
Maadili ya Viongozi wa Umma ni moja ya mjadala mkubwa Nchini Uingereza hivi sasa. Wabunge waandamizi wawili Jack Straw na Malcolm Rifkind wamekutwa na kashfa kubwa ya kutumia ubunge wao kufanyia ushawishi kampuni binafsi kwa malipo.
Kwa kuwa Bunge la Uingereza lina Kamishna wa Maadili na Kanuni za Maadili suala hilo limeshughulikiwa. Wabunge hao wameamua kung'atuka kwa aibu kubwa.
Suala kama hili linatokea sana nchini Tanzania ambapo hakuna kanuni za maadili za Wabunge ( kuna Azimio la Bunge la mwaka 2004 kutunga kanuni hizi lakini hakuna lililofanyika. Niliwasilisha muswada binafsi ili kuweka kanuni hizi ukafanyiwa mizengwe). Wabunge wa Tanzania kutumia nafasi zao kushawishi kwa maslahi ya makampuni binafsi na kulipwa kwa kazi hiyo ni jambo la kawaida kabisa.
Wabunge wafanyabiashara kutumia ubunge wao kufanikisha mipango ya biashara zao ni jambo la kawaida kabisa. Kuna Mbunge anatumia nafasi yake kutoa matangazo ya biashara kwenye gazeti lake yenye thamani ya zaidi ya shilingi 200m kwa mwaka. Kuna Mbunge ana gazeti linalotoka wakati wa Bunge la Bajeti tu kwa ajili ya kupata matangazo. Wengine wana zabuni za Bunge.
Wabunge takribani wote ni wafaidika wa misamaha ya kodi ama kwa mujibu wa stahili zao au kwa kutumia ushawishi wao kupata misamaha ya biashara wanazofanya.
Chama cha Labour cha UK kimeweka katika ilani yake ya Uchaguzi kwamba; Kwanza Wabunge wote wa Chama hicho itakuwa ni marufuku kwao kufanya kazi nyingine wakiwa wabunge, pili Chama hicho kikishika madaraka watatunga sheria kuzuia wabunge kufanya kazi nyingine.
Haya sio mapya Tanzania. Azimio la Arusha liliyaweka mwaka 1967. Uingereza wanataka kuyafuata mwaka 2015.
Turudi kwenye misingi
 
Next Post Previous Post
Bukobawadau