Bukobawadau

SERIKALI YAANZA KUCHUKUA HATUA ZA AWALI ZA KUREJESHA MIUMDOMBINU YA SHULE MBILI ZILIZOHARIBIWA VIBAYA NA TETEMEKO LA ARDHI MKOANI KAGERA


Serikali  kupitia Kamati ya Maafa ya Mkoa  ikishirikiana  na Idara  ya Uratibu wa Maafa  Ofisi ya Waziri Mkuu imeanza kuchukua hatua  za kurejesha  miundombinu  ya Shule za Sekondari  Ihungo na Nyakato kwa kuanza kubomoa majengo yaliyoharibiwa na tetemeko la ardhi lililotokea Mkoani Kagera Septemba 10, 2016.
Hatua za kuanza kubomoa majengo ya shule hizo  zimeanza kuchukuliwa leo tarehe 20.09.2016 baada ya Kamatti ya Maafa kupiga hatua kubwa katika kukabirina na janga la tetemeko kwa kutoa misaada mbalimbali kama huduma za afya kwa majeruhi, huduma za mahema na matrubali pamoja na chakula ili wahanga waweze kujihifadhi walipoteza nyumba zao au nyumba hizo kuwa hatarishi.
Katika kuhakikisha miundombinu ya shule za Ihungo na Nyakato inarejea katika hali yake ya awali Serikali kuu imeamua kusimika mzizi mkoani  hapa kwa Mawaziri watatu  wa Serikali kuamua kuungana na Kamati ya maafa kuhakiksha urejeshwaji wa miundombinu hiyo unarejea na wanafunzi wanarejea  katika shule hizo ili kuendelea na masomo yao.

Mawaziri hao ni Waziri wa Elimu, Sayansi Teknolojia na Ufundi,  Profesa Joyce Ndalichako, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI Mhe. George Simbachawene  na Mhe. Jenester Muhagamma  Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana,  Ajira na Walemavu.
Akiongea na Waandishi wa Habari katika Sekondari ya Ihungo iliyoharibiwa kabisa na tetemeko la ardhi Waziri Muhagama alisema kuwa Serikali imeanza kuchukua hatua za kubomoa na kusafisha  majengo yaliyoharibiwa ili ujenzi uanze mara moja baada ya Kamati ya Maafa kuwa imefanya kazi kubwa ya kukabiliana na athari za tetemeko kwa wananchi .



Katika kukabiliana na janga lolote kuna hatua tatu mhimu, hatua ya kwanza ni kuzuia  na katika hatua hiyo hulenga kupunguza athari za janga. Hatua ya pili ni kukabiliana na athari wakati wa janga ambapo Kamati ya Maafa ilivyofanya wakati wa tetemeko. Hatua ya Mwisho ni kurejesha miundombinu iliyoharibiwa na janga husika .
Akifafanua hatua hizo katika eneo la Shule ya Sekondari Ihungo Mkurugenzi wa Idara ya Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu  Brigedia Jenerali Mbazi Msuya alisema kuwa Serikali imeanza hatua ya kurejesha miundombinu huku ikiendelea kutoa misaada ya maafa. Aidha alitoa wito kwa wananchi wa Mkoa wa Kagera kuanza kurejesha miundombinu yao kama Serikali ilivyoanza kufanya.


Katika kurejesha miundombinu iliyoharibiwa na tetemeko la ardhi  Kamati ya Maafa imezipa kipaumbele shule mbili za Sekondari  Ihungo na Nyakato kwasababu shule hizo ziliharibiwa sana na kupelekea kufungwa baada ya kuonekana kuwa majengo yke hayafai kutumika. Aidha, majengo yote ya umma na Serikali yatarejeshwa kwa utaratibu ili kurudisha hali iliyokuwepo awali.
Tetemeko la ardhi lilitokea Mkoani Kagera Septemba 10, 2016 na kusababisha vifo bvya wananchi 17, Majeruhi 440 na hadi sasa wamebakia majeruhi 17 ambao wanaendelea na matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa .
Pia tetemeko hilo lilisababisha nyumba 2,072 kuanguka, Nyumba zenye uharibifu hatarishi 14,595. Nyumba zenye uharibifu mdogo 9,471 (Jumla ya nyumba zilizoanguka na zilizopata uharibifu hatarishi ni 16,667). Aidha, wananchi walioathirika na kuhitaji misaada ili waweze kurudi katika mfumo wa kawaida wa maisha yao ni 126,315.


Next Post Previous Post
Bukobawadau