Bukobawadau

KATIKA KUENDELEZA MILA NA DESTURI TUNAGUSIA NENO 'OKULONGOLA' PIA 'OKUTANGILILA'

       
 Okulongola: 

Okulongola, ni kitendo cha hiari alichokifanya mtu kwa kusudi la kumuonyesha mwenzake jinsi alivyoridhishwa na kitendo kingine ambacho yeye mwenyewe alipata kutendewa huko nyuma. Waingereza hukiita kitendo kama hicho reciprocity. Sisi hatuwezi kukosea kukiita Nipe - Nikupe. Ni kitendo cha kurudisha fadhila.
Mfano mzuri hapa, ni mila nyingine ya Kihaya, ambayo kwayo mwanamke hutoka na kwenda porini (wakati wa msimu wa musenene) na kukamata senene kwa ajili ya mumewe. Baada ya kuwaandaa wale senene na kuwawasilisha kwa mumewe kwa wakati muafaka, hutazamiwa mume naye aonyeshe kufurahi na kuridhishwa na juhudi za mkewe, kwa kumnunulia mkewe zawadi maalum, hususan doti ya kitenge au khanga. Akifanya hivyo, anakuwa ametekeleza mila ya okulongola. Mambo yalikuwa vivyo hivyo kwa maswahiba walioshibana.
Okutangilila 
Katikanchi ya Wahaya’ (Buhaya), pengine hakuna mila ambayo imeenea na kuzingatiwa zaidi kuliko Okutangilila. Huwezi kuingia katika mji wa Muhaya ukatoka bila kutangililwa, yaani kulakiwa kwa kahawa au pombe, kama ishara ya ukarimu na upendo. Hata awe masikini kiasi gani, Muhaya atafanya juhudi kubwa kuhakikisha anaweka nyumbani kwake akiba ya kahawa (emwani) za kutafuna kwa ajili ya wageni wanaoweza kumfikia hata bila taarifa; haijalishi wageni hao wanatoka masafa ya mbali au karibu.
Kaya masikini iliyotembelewa na mgeni inaweza kutindikiwa na huduma nyingine yoyote, ikiwa ni pamoja na kitoweo, kiasi cha mgeni huyo kulazimika kula chakula ‘maluma’, jambo ambalo ni fedheha ya kutosha kwa mwenyeji, lakini kahawa ya mgeni kutafuna itapatikana tu, japo iwe nusu ya kibaba. Miaka hii, pombe, hasa gongo (enkonyagi), inatumika zaidi kukidhi haja, lakini mila inakuwa timilifu ikihusisha pia kahawa za kutafuna.
  MDAU  MSOMAJI TANGAZA NASI KAMPUNI YAKO AU BIASHARA YAKO UPATE KUNUFAIKA ZAIDI!!
Next Post Previous Post
Bukobawadau