Bukobawadau

NENO LA KIHAYA 'OKUHONGA'

Katika maana yake ya kiasili, Okuhonga katika jamii ya Wahaya, hakukuhusiana na kutoa rushwa, kufanya vitendo vya kifisadi au kununua mapenzi ya mwanamke. Enzi kabla ya ujio wa Wazungu walioleta na kutupandikizia imani na taratibu zao za kumuabudu, kumcha na kumtukuza Mungu, nasi Waafrika tulikuwa na taratibu zetu za kuwaenzi miungu yetu.
Okuhonga, kulikuwa ni utaratibu wa kuwatolea miungu sadaka na zawadi mbalimbali ili iwapendeze kututunuku baraka na kutujalia neema na rehema tele katika maisha yetu ya kila siku. Na katika jambo hili, Waafrika hatukutofautiana sana na Wazungu wa Ulaya, karne za kale (eila lya kalanda).
Miungu ya Wahaya, ilikuwa ni pamoja na kasi (mungu wa ardhi na kilimo), ilungu (mungu wa nyika na wanyamapori), lyangombe (mungu wa mifugo, hasa ng’ombe), mugasha (mungu wa Ziwa Lweru- Victoria), nyakalembe, (mungu wa ustawi wa wanawake na mambo ya uzazi), n.k.
Katika Agano la Kale, tunasoma sana habari za dhabihu na matambiko ya kuchoma na kuteketeza kwa ajili ya Mungu? Wahenga wetu nao hawakuwa mbali katika kuwatambikia miungu yao ili iwajalie neema walizozihitaji ili kukidhi shida zao lukuki maishani mwao na kuondokana na maangamizi yaliyowazinga? Na ndiyo tunavyofanya hata sisi leo, chini ya madhehebu yetu mbalimbali - kwa kutoa zaka na sadaka kwa ajili ya kusifu na kushukuru ? Kimsingi, ni dhana ile ile?
Kwa kuhitimisha maelezo haya ya utoaji na upaji kwa ajili ya miungu, okuhonga, Wahaya hawakukosa kukiri imani yao katika uweza wa miungu hao. Kila walipobanwa na matatizo na kuelekea kukosa suluhu ya kutokea, walisikika wakiungama na kujinyenyekeza: “ tubihongele mukama mungu”.
Maelezo ya mifano hiyo hapo juu, yatoshe kuonyesha jinsi utamaduni wa Kihaya ulivyosheheni utajiri mkubwa katika nyanja ya ukarimu na upaji, okuha.
Next Post Previous Post
Bukobawadau