Bukobawadau

BODI YA FILAMU YAANZA NA KIMINI CHA AUNTY EZEKIEL.

BODI ya ukaguzi wa filamu na michezo ya kuigiza imeanza kuwashukia wale wote wapenda kuvaa vimini na kushiriki katika filamu za Swahiliwood, hayo yameongewa na katibu wa Bodi ya filamu nchini Bi. Joyce Fisso baada hivi karibuni kukutana na mwigizaji na mtayarishaji wa filamu Aunty Ezekiel.

Msanii huyo aliitwa na Bodi baada ya filamu hiyo kufika hapo kwa ajili ya ukaguzi wa filamu hiyo na kukutana na jopo la wakaguzi waliompata ushirikiano kwa kumshauri sehemu za kuzirekebisha bila usumbufu, jambo lilomfurahisha Aunty Ezekiel.

Aunt Ezekiel ameeleza kuwa amefurahishwa na Bodi ya Filamu Tanzania kwa kufanya majadiliano mazuri juu ya filamu yake ya Scola kwa kubaini mapungufu baadhi yaliyopo na kumuelekeza cha kufanya.

“Nashukuru bodi wamekuwa waelewa ,wamenielekeza kurekebisha baadhi ya vipengele ili kuboresha filamu yangu naahidi kuirekebisha kwani vinarekebishika.”alisema Aunt Ezekiel.

Aidha Aunt Ezekiel ameomba radhi kwa kutopeleka script yake ya filamu hiyo mpya ya SCOLA Bodi ya Filamu na amesema atakuwa akiwasilisha miswada yake kabla ya kutengeneza filamu zake. Aidha amewahakikishia watanzania kuwa atakuwa mfano bora katika kutengeza filamu bora na zenye maadili.
.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Bodi hiyo Bi.Joyce Fissoo ameeleza kuwa kuna umuhimu wa wasanii kufuata sheria na taratibu za filamu kabla ya kuanza kutengeneza na kuzitoa filamu zao ambapo sheria inawataka kuwasilisha mswada (script) Bodi ili na kupewa idhini yakuendelea na kazi hiyo.


“Wasanii mnatakiwa kuzingatia sheria na kuwasilisha script ili zikaguliwe na kupata ruhusa kwa mujibu na taratibu za sheria kabla ya kuanza kutengeneza filamu kwa sababu sheria Na 4 ya mwaka 1976 ya Filamu na Michezo ya kuigiza pamoja na kanuni zake zinaelekeza wasanii kutotoa au kutengeneza filamu kabla ya kupeleka mswada (script ) Bodi ya Filamu ili ipitiwe.

Aidha Katibu huyo alifafanua kuwa wasanii wanapotengeneza filamu kupitia script ambazo hazijakaguliwa kuna uwezekano mkubwa wakuwepo sehemu ambazo zinakiuka maadili ya mtanzania,ikiwepo uvaaji wa mavazi mafupi yaliyopitiliza kwa waigizaji wanawake,lugha mbaya na baadhi ya vitendo vingine visivyofaa kuoneshwa kwa umma.

Aliwataka wasanii nchini kutengeneza filamu zinazozingatia maadili ya Kitanzania ikiwemo kutocheza picha zenye mavazi yanayoopitiliza kwa ufupi,kubana au zinazoonesha maumbile ya muigizaji mara kwa mara.

Kikao hiki pia kiliwashauri Bodi ya Filamu kukutana na wasanii wa kike ili kujadili masuala ya mavazi yasiyo nastaha, Bodi imeridhia ombi hilo
Next Post Previous Post
Bukobawadau