Bukobawadau

UFISADI WAKWAMISHWA KCU

Na Prudence Karugendo
>
> Ushirika nchini umeandamwa na majaribu ya kila aina, katika
> baadhi ya maeneo majaribu hayo yameunyofoa roho ushirika na
> kuua kabisa.
>  Katika hali ya kushangaza waliopaswa kuwa walinzi wa
> ushirika ndio maranyingi wamekuwa kikwazo cha ushirika
> kuimarika na kushamiri nchini. Ushirika umekuwa ukihujumiwa
> na waliopaswa kuwa kinga ya hujuma dhidi yake!
>  Mara kadhaa nimeandika juu ya kinachojionyesha wazi kuwa ni
> ufisadi katika chama kikuu cha ushirika cha KCU (1990) Ltd.
> cha mkoani Kagera, kiasi cha baadhi ya watu wanaojifanya ni
> wadau wa ushirika huo, ambao lakini nahisi wananufaika na
> ufisadi unaofanyika katika chama hicho, kufikia kuniuliza
> kwamba sichoki  kuuandika ufisadi ndani ya chama hicho
> cha ushirika?
>  Jibu langu kwa wote wenye mtazamo huo limekuwa ni moja,
> nitachokaje kuandika juu ya ufisadi ndani ya KCU (1990) Ltd.
> wakati ufisadi wenyewe ukizidi kukomaa ndani ya ushirika
> huo? Naamini kwamba kama wanaofanya ufisadi ndani ya chama
> hicho hawatachoka kuufisidi ushirika huo hata mimi
> sitachoka  kuandika.
>  Hivi majuzi niliandika mahojiano niliyofanya na mwakilishi
> wa chama cha msingi cha Kamachumu,  Muleba, Kagera,
> Archard Felician Muhandiki, ambaye amekuwa mwiba mkali kwa
> mafisadi ndani ya KCU (1990) Ltd. kiasi cha kufanyiwa
> mizengwe na kufukuzwa kwenye mkutano mkuu wa chama hicho cha
> ushirika ilhali akiwa mjumbe halali, mwakilishi wa chama
> chake cha msingi.
>  Na baada ya kutolewa nje ya mkutano bado viongozi wa wa
> chama kikuu wakaendelea kufanya mizengwe ili mwakilishi huyo
> afukuzwe uanachama katika chama chake cha msingi.
>  Katika hali ya kushangaza chama chake cha msingi cha
> Kamachumu kikakubali kuyapokea maelekezo hayo ya kimizengwe
> kutoka chama kikuu na kumuita Muhandiki ili ajieleze kwa
> nini asifukuzwe uanachama.
>
> Wakati anaondoka kwenda kwenye kikao hicho cha kujieleza
> mbele ya wajumbe wa bodi ya chama chake cha msingi
> akatayarisha utetezi wake ambao ameutoa uchapishwe gazetini
> ili wanaushirika, popote walipo nchini, wausome na kuelewa
> namna ya kukabiliana na mizengwe inayotokana na ufisadi
> unaoendeshwa kwenye vyama vya ushirika. Anasema ameamua
> kufanya hivyo kwa vile anaamini yanayotokea kwenye chama
> chake kikuu cha ushirika pia yanatokea kwenye vyama vingine
> nchini.
>  Ufuatao ndio utetezi alioutayarisha na kuuwasilisha kwa
> wajumbe wa Bodi ya chama chake cha msingi cha Kamachumu.
> “Waheshimiwa wajumbe wa Bodi ya chama cha msingi
> Kamachumu; kwa masikitiko makubwa napenda nichukue fursa hii
> kuwajulisha rasmi juu ya dhuluma kubwa na udhalilishaji
> nilivyofanyiwa na mwenyekiti wa KCU (1990) Ltd. kwa
> kunifukuza kama mbwa katika mkutano mkuu wa makisio wa chama
> chetu kikuu uliofanyika tarehe 14 / 5 / 2013, kwa madai
> kwamba nimekuwa nikiiyumbisha KCU (1990) Ltd. kwa njia
> mbalimbali ikiwemo kuifungulia kesi pamoja na kutoa tuhuma
> mbalimbali dhidi ya uongozi wa chama.
>  Awali ya yote,  napenda nitamke wazi kwamba mimi kama
> mwakilishi wa chama chetu hiki cha Kamachumu ni mjumbe
> halali wa mkutano mkuu wa KCU (1990) Ltd.. Hivyo kitendo
> alichonifanyia mwenyekiti cha kunifukuza kwenye mkutano ni
> cha ubabe na ukiukwaji mkubwa, sio tu wa sheria za vyama vya
> ushirika, bali pia ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu kama
> zinavyoainishwa katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa
> Tanzania.
>
> Ikumbukwe kwamba tuhuma nyingi ambazo muda wote nimekuwa
> nikizitoa dhidi ya KCU (1990) Ltd. zinamhusu moja kwa moja
> mwenyekiti, John M. Binunshu. Kwahiyo haiingii akilini jinsi
> yeye kama mtuhumiwa anavyoweza pia  kuwa mwamuzi katika
> suala hili.
>  Mbali na hiyo, mimi kama mwakilishi wa wakulima wa kahawa
> wa eneo langu katika KCU (1990) Ltd., ni jukumu langu kupiga
> vita kwa nguvu zangu zote vitendo vyote vya ubadhirifu na
> ufisadi vinavyofanywa na uongozi wa chama chetu kikuu cha
> ushirika dhidi ya wakulima. Maana ni vitendo hivyo ambavyo
> vimekuwa vikimpunguzia mkulima kipato katika zao la kahawa.
> Katika hali hiyo uongozi wa KCU (1990) Ltd. hauna haki hata
> kidogo kisheria kunizuia nisitekeleze jukumu hilo nililopewa
> na wakulima wenzangu wa chama hiki cha msingi cha
> Kamachumu.
>  Kama baadhi yenu mnavyofahamu, tuhuma ambazo nimekuwa
> nikizitoa dhidi uongozi wa chama chetu kikuu ni nzito. Kwa
> sababu vitendo vya uongozi huo ambavyo muda wote nimekuwa
> nikivilalamikia vimechangia kwa kiasi kikubwa kudidimiza
> kipato cha mkulima kinachotokana na zao la kahawa hapa
> mkoani kwetu. Katika kufafanua jambo hilo nataka niorodheshe
> baadhi ya tuhuma hizo.
>
> Kupindisha sheria na kanuni za vyama vya ushirika kwa ajili
> ya kumwezesha mwenyekiti aliyepo kuendelea na wadhifa wake
> huo. Kwa mujibu wa sheria za vyama vya ushirika na kanuni
> zilizotungwa chini ya sheria hiyo, uwakilishi wa Bw. John M.
> Binunshu kwenye mkutano mkuu wa KCU (1990) Ltd. ulikuwa
> umefikia tamati wakati wa uchaguzi wa theluthi, na Binunshu
> kisheria alikuwa anazuiwa kugombea tena.
>
> Katika kumwezesha agombee tena zilipikwa njama za kuongeza
> idadi ya wawakilishi kutoka wawili hadi watatu ili Binunshu
> agombee tena kupitia nafasi hiyo iliyoongezwa. Nyongeza hiyo
> ya wajumbe ilifanyika bila ya kufuata utaratibu wa kisheria.
> Kwahiyo mimi kwa kujua athari ambazo zingetokana na
> upindishaji huo wa sheria kwa manufaa ya mwenyekiti
> nikafungua kesi mahakamani kuubatilisha upindishaji huo wa
> sheria. Kwa bahati mbaya wakili wangu alifungua kesi hiyo
> katika Mahakama ya Hakimu Mkazi badala ya Mahakama Kuu na
> hivyo kesi hiyo kutupiliwa mbali kwa sababu za kiufundi.
>
> Pamoja na hayo, ukweli unabakia palepale, kwamba hatua hiyo
> iliyochukuliwa na Mrajis Msaidizi wa vyama vya ushirika,
> Kagera, kuongeza idadi ya wawakilishi kutoka 250 hadi 375
> katika jitihada za kumnusuru swahiba wake, inambebesha
> mkulima mzigo mkubwa wa gharama za kuendesha mikutano ya KCU
> (1990) Ltd. Mathalan, katika mikutano mikuu ya mizania na
> makisio iliyofanyika hivi karibuni kila mjumbe alilipwa Tsh.
> 530,000. Hii maana yake ni kwamba posho zilizolipwa kwa
> wajumbe 125 walioongezeka kutokana na hatua hiyo ya Mrajis
> Msaidizi ni Tsh. 66, 250, 000. Hiyo ni mbali na gharama za
> vinywaji baridi na vitafunwa wakati wa mkutano.
> Hii ni gharama kubwa hasa ikizingatiwa kwamba mizania ya
> chama hicho inaonyesha kuwa kimekuwa na matumizi makubwa
> kuliko kipato halali na hivyo kukifanya mwaka hadi mwaka
> kiwe kinafanya kazi ya kufidia naksi inayojitokeza kati ya
> mapato na matumizi kwa kupora fedha za mkulima na malipo
> yake ya nyuma. 
> Kwa miaka nenda rudi KCU (1990) Ltd. imekuwa na matumizi
> makubwa kuliko mapato yake halali. Kwa mujibu wa hesabu za
> KCU (1990) Ltd. zilizokaguliwa, katika kipindi cha miaka
> mitano iliyopita,  chama hicho kimetumia karibu Tsh.
> Bilioni 3 zaidi ya mapato yake kama inavyoonyeshwa hapa
> chini.
>
>
>
>
>
> MWAKA/MSIMU    MAPATO   
> MATUMIZI    ZIADA YA MATUMIZI
> 2011 / 10    892,553,227   
> 1,473,904,496    581,351,259
> 2009 / 10    764,363,893   
> 1,398,447,523    634,083,630
> 2008 / 09    950,202,482   
> 1,418,072973    467,870491
> 2207 / 08    448,830,414   
> 1,296,027,087    847,196,637
> 2006 / 07    600,196,621   
> 926,826,549    326,629,928
> JUMLA YA MATUMIZI YA ZAIDI   
>         2, 857, 131, 991
>
> Pengine wengi wenu hamjui nini maana ya KCU (1990) Ltd. kuwa
> na matumizi makubwa kuliko mapato yake halali. Ukweli wa
> jambo hili ni kwamba chama hicho kikuu cha ushirika, bila
> ridhaa ya wakulima ambao kwa hapa ndio wanaushirika,
> kimekuwa muda wote kikipora pesa za wakulima za malipo ya
> nyuma kufidia hayo matumizi ya kifisadi. Jambo hili haliwezi
> kukubalika na kuachwa liendelee hata kidogo, kwa kuwa
> limechangia sana kudumaza maendeleo ya mkulima. Ndiyo maana
> nimeamua kulivalia njuga. Kama uongozi wa KCU (1990) Ltd.
> unanichukia kutokana na umakini wangu huo siwezi kuizuia
> chuki hiyo, kwani kazi niliyopewa ni kusimamia maslahi ya
> wakulima wenzangu walionichagua na wala sio kuulinda
> udhalimu wa viongozi wa KCU (1990) Ltd.
> Suala lingine ambalo nimekuwa nikililalamikia ni matumizi
> mabaya ya fedha zinazotokana na Biashara ya Soko la Haki
> (Fair Trade). Kama mjuavyo, soko hilo linatoa ruzuku ya aina
> mbili. Ya kwanza ni kufidia bei ya wakulima wakati bei ya
> kahawa inapokuwa imeshuka sana, na ruzuku ya pili inalenga
> kugharamia mradi wowote ulioridhiwa na wakulima wenyewe,
> ulio na maslahi kwao.
> Kwa miaka nenda rudi ruzuku hiyo, ruzuku hiyo inayotolewa
> kufidia kushuka kwa bei hailipwi kwa mkulima kiukamilifu.
> Badala yake  ni sehemu ndogo tu ya ruzuku hiyo
> inayotumika kwa wakulima, lakini sehemu kubwa imekuwa
> ikitumika kivingine.
> Aidha,  hata hiyo ruzuku inayotumika kwenye miradi
> iliyopaswa kuwa na maslahi kwa wakulima imetumika zaidi
> kwenye miradi iliyoteuliwa na uongozi wa KCU (1990) Ltd.
> bila ridhaa ya wakulima na miradi iliyo mingi haina maslahi
> yoyote  kwa wakulima.
> Chukua kwa mfano, mradi wa Hoteli Yasila. Hoteli hiyo
> imenunuliwa kwa Tsh. Milioni 500, na wakati hoteli hiyo
> inanunuliwa KCU (1990) Ltd. ilikuwa ikimiliki hoteli
> nyingine iitwayo  Lake Hotel ambayo imetelekezwa kwa
> sababu ambazo hazielezwi.
> Hii ni mifano michache ya matumizi mabaya ya pesa za
> wakulima ambayo nimekuwa nikiilalamikia.  Hatua yangu
> hiyo imezua uhasama mkubwa kati yangu na uongozi wa KCU
> (1990) Ltd., ndiyo maana umechukua hatua ya kutaka
> kuning’oa kwenye uwakilishi wangu. Lakini kwangu mimi hilo
> halinipi tatizo. Ila ieleweke kwamba mimi nilichaguliwa na
> wakulima, hivyo  uongozi wa KCU (1990) Ltd. au Bodi hii
> havina madaraka yoyote ya kuniondoa kwenye uwakilishi wangu
> wa chama hiki cha msingi.”
> Hivyo ndivyo Mzee Archard Felician Muhandiki alivyofanikiwa
> kuzima jaribio la kifisadi la kutaka kumuondoa kwenye
> uwakilishi wa chama chake cha msingi lililopangwa na
> kuratibiwa na KCU (1990) Ltd.
prudencekarugendo@yahoo.com
> 0784 989 512
Next Post Previous Post
Bukobawadau