Bukobawadau

MISAADA ISIYO KUWA NA TIJA MUTUKULA NA MAPAPA WANAOPETA

 Muonekano wa Jengo la Afrika Mashariki ambalo liko mbioni kukamilika.
Trekta lililotelekezwa linaendelea kuhujumiwa

Wadau kama mtandao wa kijamii tunawashukuru kwa kuibua matatizo mbalimbali ya kijamii kwani baadhi yanapatiwa ufumbuzi kwa kipindi kifupi. Mfano halisi, wiki mbili zilizopita tulizungumzia tatizo la choo iliyotelekezwa na ufumbuzi sasa umepatikana. Tatizo hilo sasa limekwisha baada ya wakubwa kulishughulikia. Wiki hii nimefikiria suala la hujuma inayoonekana katika halmashauri mbalimbali nchini kuhusu vyombo/vifaa vya msaada (donation).Inaonesha wenye dhamana ya kuvisimamia vyombo hivyo hawana uchungu navyo labda kwa sababu hawakuvitolea jasho. Mfano halisi ni halmashauri ya wilaya ya Misenyi ambayo imepatiwa trekta la kusombea taka kutoka mradi wa mazingira wa umoja wa mataifa (UN HABITAT) tangu 2008. Sina uhakika kama trekta hilo lilitembea zaidi ya km 5 baada ya kukabidhiwa kwa mamlaka husika. Badala yake, limetelekezwa kwenye viwanja vya mamlaka ya kodi ya mapato Mutukula ambapo hadi hivi sasa linaendelea kuhujumiwa na wapita njia. Swali ni kwanini viongozi wa halmashauri walikubali kupokea chombo ambacho hakina tija kwa jamii husika? Kama walionelea suala la kusomba taka ni la kugawa tenda kwa mtu binafsi ambaye husomba taka kwa roli mara moja kwa wiki au baada ya wiki mbili kwa nini trekta hilo lisigawiwe kwa uongozi wa vijiji jirani na likatumike kwa mambo mengine kama kusaga nafaka au kilimo (power tiller) badala ya kuachwa liendelee kuoza na kuhujumiwa.?Tatizo la uchafu bado ni kiini macho kumalizika kabisa katika mji mdogo wa Mtukula hii ni kutokana na tatizo la baadhi ya watenda kazi waliopewa dhamana na serikali kushindwa kuhamasisha jamii na badala yake wanatumia sheria kandamizi. Kuna sababu gani Afisa Afya kumtoza mfanya biashara mdogo katika soko la Mutukula faini isiyokuwa na stakabadhi kati ya shilingi 10,000/= na 20,000/= kwa kosa dogo la kushindwa kupanga bidhaa yake katika utaratibu ambao anautaka? Kwa nini kuwaonea wadogo wakati mapapa wanapeta? Matatizo ya msingi yanatakiwa yatafutiwe ufumbuzi badala ya kujali maslahi binafsi kwani baada ya siku chache zijazo Mutukula litakuwa soko kubwa la kibiashara la Afrika Mashariki hivyo ubabaishaji hautakuwa na nafasi.
Fumbuka
Next Post Previous Post
Bukobawadau