Bukobawadau

NECTA YATANGAZA MFUMO MPYA

Dodoma. Baraza la Mitihani la Taifa (Necta), limeanza mfumo mpya wa kupanga matokeo ya kidato cha nne mwaka huu na ya kidato cha sita mwakani, ambapo sasa madaraja yatapangwa kwa wastani wa pointi (GPA) badala ya jumla ya pointi.
 Hayo yalisemwa jana na Katibu Mtendaji wa baraza hilo, Dk. Charles Msonde katika mkutano wa wadau wa kampeni ya elimu kwa watoto wa kike walio katika mazingira magumu (Camfed).
Dk Msonde alikuwa akitoa mada kuhusu uwekaji alama za ufaulu unaotekelezwa na Necta.
Alisema mfumo huo siyo mpya kutumiwa na Necta kwa sababu umekuwa ukitumiwa katika kupanga matokeo ya wanafunzi wa vyuo vya walimu.
“Mfumo utakaotumika kupanga madaraja ya mitihani kwa wanafunzi wa kidato cha nne wa mwaka huu na kidato cha sita mwakani na kuendelea utakuwa si ule wa kutumia jumla ya pointi badala yake utakuwa ni wastani wa pointi,” alisema na kuongeza:
“Utaratibu huu siyo kwamba ni mpya kwa baraza la mitihani, tumefanya hivyo kwa matokeo ya ualimu na hata tunapopanga shule bora tumekuwa tukitumia GPA... Hatubadilishi thamani ya madaraja.”
Alisema kuwa thamani ya madaraja itabaki kuwa ni ile ile bali sasa watakuwa na mfumo unaolingana na kupanga matokeo ya ualimu.
Dk Msonde alisema lengo la kutumia mfumo huo ni kuwezesha kuwa na mfumo unaofanana katika ngazi zote za elimu nchini.
“Lengo jingine ni kuwarahisishia wenzetu wa TCU na Necta na wadahili wengine wawe wanatumia mfumo unaofanana na wa kwetu wasianze tena kubadilisha vyeti,”alisema.
Alisema lengo lingine ni kuelimisha Watanzania kuhusu mfumo huo mpya wa upangaji wa matokeo.
ya mtihani ambapo kwa kutumia mfumo wa jumla ya pointi ilikuwa ni vigumu kuuelewa.
Dk. Msonde alisema kwa mfumo wa kutumia jumla ya pointi watanzania wengi walikuwa wanafikiri mtu akipata pointi nyingi ndio amefaulu zaidi ya wale waliopata pointi chache.
 Alisema tayari wametoa mafunzo ya uelewa juu ya mfumo huo kwa wadau mbalimbali wa elimu na kwamba wanautambua.
MWANANCHI
Next Post Previous Post
Bukobawadau