Bukobawadau

SIRI NZITO CCM 2015

Dar na Z’bar. Vikao vya Kamati Kuu ya CCM na Kamati Maalumu ya NEC Zanzibar vinaonekana kuwa huenda vikaiweka hadharani siri nzito za urais wa Jamhuri ya Muungano.
Mkutano wa sekretarieti ndiyo utakaoanza leo ukifuatiwa na Kamati Maalumu ya NEC Zanzibar huku Kamati Kuu ya CCM ikitarajiwa kukutana Jumanne wiki ijayo katika Ofisi Kuu ya CCM Kisiwandui kujadili na kutathmini hali ya kisasa kuelekea Uchaguzi Mkuu mwaka huu.
Kikao hicho kimekuja huku wagombea wa nafasi ya urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia chama hicho wakipishana kwa usafiri wa ndege na boti kwenda Zanzibar kutafutwa kuungwa mkono na wajumbe wa NEC na waliopo visiwani humo.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai alithibitisha kikao hicho kufanyika Zanzibar na kitaoongozwa na Mwenyekiti wake Rais Dk Jakaya Kikwete ambaye amebakisha muda mfupi kumaliza muhula wake wa uongozi tangu aingie madarakani mwaka 2005.
Vuai alisema Kamati Kuu ya CCM itakutana, itatanguliwa na Kikao cha Kamati Maalumu ya NEC Zanzibar.
Alisema suala kubwa ambalo watalijadili ni kuangalia mwenendo wa utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010/2015 tangu kumalizika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010.
Hata hivyo, Vuai alisema hayuko tayari kuzungumzia ajenda ya kikao cha Kamati Kuu kwa vile majukumu hayo yako kwa Katibu wa Itikadi na Uenezi Taifa, Nape Nnauye.
Pia, alisema Kamati Maalumu ya NEC Zanzibar itakuwa na ajenda ya mengineyo itakayojadili hali ya kisiasa tangu kumalizika uchaguzi mkuu uliopita ambapo kikao hicho tayari matayarisho yake yamekamilika kabla ya kuanza kamati Kuu kukutana visiwani humu.
Nape
Hata hivyo, Nape alisema jana kuwa Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya CCM, inakutana leo jijini Dar es Salaam kupanga ajenda zitakazojadiliwa kwenye mkutano wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama hicho itakayokutana Zanzibar Jumanne ijayo.
Alisema kuwa kikao hicho ni cha kawaida cha siku moja chini ya Mwenyekiti wa CCM Rais Jakaya Kikwete.
Kikao cha Kamati Kuu kinakutana na kukiwa na patashika ya makada wa CCM wanaotajwa kuwania nafasi ya urais wakipishana kwa safari za usafiri wa majini na angani na wapambe wao kukutana na wajumbe wa NEC na mkutano mkuu katika vikao vya faragha Pemba na Unguja kuomba ushawishi wa kuungwa mkono.
Hali ya kisiasa Zanzibar, inadaiwa kuchafuka na kuhatarisha uimara wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) baada ya vigogo wa Serikali hiyo kuanza kunyosheana vidole hadharani.
Inaelezwa kuwa joto la uchaguzi wa urais ndilo ambalo limesabasisha hali hiyo itokee. Makamu wa Kwanza wa Rais Maalim, Seif Shariff Hamad na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein huenda wakachuana katika uchaguzi wa urais mwaka huu.
Sauala lingine zito ambalo linaweza kujadiliwa katika vikao hivyo ni la kashfa ya escrow ambayo imewakumba mawaziri na baadhi ya madaka wa chama hicho.
Mawaziri ambao wamekumbwa na kashfa hiyo ni pamoja na aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka ambaye ni Mjumbe wa Kamati Kuu na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospter Muhongo.
Profesa Tibaijuka tayari ameondolewa kwenye nafasi yake ya uwaziri baada ya kupokea kiasi cha Sh1.6 bilioni kutoka kwa Mfanyabiashara maarufu nchini, James Rugemarila ambaye ni mbia wa Kampuni ya Kufua Umeme ya IPTL.
Mwingine anayetajwa kuhusika ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, Andrew Chenge, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Sheria na Katiba, William Ngeleja na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo.
Mbali na wahusika wa Akaunti ya Escrow, vikao hivyo huenda vikajadili ripoti ya maadili ya viongozi ikiwamo waliokumbwa zuio la kujihusisha na kampeni za kuwania urais mapema kwa miezi 12, huku mienendo yao ya kisiasa ikifuatiliwa.
Waliozuiwa kufanya kampeni ni Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi, Teknolojia January Makamba, Waziri Mkuu Mkuu wa zamani, Edward Lowassa na Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye.
Wengine ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), Steven Wassira na aliyewahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini ambaye ni Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja.
Hata hivyo, Nape alipoulizwa kuhusiana na wagombea wa urais kufanya kampeni za nguvu na wengine kutumia mitandao ya simu kusambaza ujumbe, alikataa kuzungumza chochote kuhusiana na suala hilo pamoja na sakata la escrow iwapo litapewa nafasi katika vikao hivyo vya chama.
Mtikisiko Zanzibar
Maalim Seif hivi karibuni alikaririwa akisema atapambana na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein kwenye vikao vya Serikali na kulalamika kuna baadhi ya masheha, wakuu wa wilaya na mikoa wakiwanyima wananchi haki ya kupata vitambulisho vya Uzanzibari mkaazi na kutoandikisha kwenye Daftari la Kudumu la Kupiga.
Akijibu dai hilo, Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Balozi Seif alisema hakuna wananchi wanaokatazwa kupata Vitambulisho vya Mzanzibari mkaazi na kueleza kuwa chini ya Sheria Namba 7 ya mwaka 2005 hakuna mtu ambaye anaweza kupewa kama siyo mkaazi wa Zanzibar kwa miaka mitatu.
Balozi Seif alisema Serikali haitakubali kupata hasara ya kuzalisha vitambulisho kutokana na idadi kubwa ya zaidi kuandikishwa watu ambao siyo wakazi ya Pemba, wakati kuna vitambulisho vingi vimeshindwa kuchukuliwa na wenyewe ambao alisema ni mamluki.
Mjumbe mmoja wa NEC ambaye ameomba jina lake lihifadhiwe, alithibitisha vigogo wanaowania urais na wapambe wao kumshawishi kuingia katika kundi lao.
Wagombea urais
Vigogo wa urais waliofanya ziara kwa nyakati tofauti hivi karibuni visiwani Zanzibar ni pamoja na Waziri Mkuu Mstaafu Fredrick Sumaye, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Uhusiano) Stephen Wasira, Mbunge wa Sengerema William Ngeleja na Waziri Mkuu Mizengo Pinda ambaye amealikwa kuhudhuria Maulid ya Kuzaliwa Mtume Muhammad (SAW) leo yaliyoandaliwa na Mbunge wa Mpendae na Mafanyabiasha mashuhuri, Salum Turky.
Kadhalika Waziri Mkuu mstaafu Edward Lowassa ambaye wakati wa Sikukuu ya Krismasi ya mwaka jana alikuwa Zanzibar.
MWANANCHI.

Next Post Previous Post
Bukobawadau