Bukobawadau

ATANGAZA NIA KUMRITHI MAMA TIBAIJUKA

Anaitwa Roderick Lutembeka. Ni mzaliwa wa kijiji cha Buganguzi kata Buganguzi wilayani Muleba mkoani Kagera.
Anatarajia kugombea ubunge wa jimbo la Muleba Kusini kwa tiketi ya Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). Mbunge wa sasa ni Prof. Anna Tibaujuka ambaye kimsingi hana tena 'credibility' ya kuwa mbunge wa Jimbo hili kwa kile kinachotajwa na wengi kuwa tangu awe mbunge hajawahi kuitisha mkutano wa wananchi wake kusikiliza kero zao, hajafanya lolote la maana la kukumbukwa na mbaya zaidi amechafuka kwelikweli kutokana na sakata la Escrow lililopelekea kung'olewa kwenye kiti chake cha uwaziri.
Aidha ile kauli yake aliyoitoa kwenye baraza la maadili lililopelekea kuvuliwa wadhifa wake wa UNEC- CCM, ya kutumia milioni kumi (10,000,000/=) kwa ajili ya mboga tu imechefua wengi na hivyo kutafsiriwa kama MTU anayejikweza, mwenye dharau, mwingi wa kiburi na majivuno kwa watanzania hususani wale wa Muleba Kusini anaowawakilisha bungeni.
Hivyo kwa kuwa habari ya mjini ni CHADEMA, basi kuna uwezekano mkubwa mbunge ajaye atatoka chama hiki na chaguo la wanachama na wana Muleba walio wengi ni huyu ndugu Roderick Lutembeka; mwenye hekima na busara za hali ya juu, mwanasiasa mzalendo, mwadilifu na msomi nguli na mahiri mwenye uwezo jadidi na uzoefu wa kutosha katika masuala ya Uchumi na Fedha pamoja na Uongozi.
Ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo, Lutembeka ni Katibu Mkuu wa Baraza la Wazee Taifa na hii inampa nafasi ya kuwa miongoni mwa 'mainjinia' wa Chama hiki kinachokua kwa kasi ya roketi!

ELIMU YAKE:
Shule ya Msingi: Mubango, Buganguzi
Shule ya Kati (middle school): Biirabo, Nshamba
Shule ya Sekondari (O-Level): Balimi Sekondary, Bukoba
(A- Level): Ndanda High School, Songea
Alijiunga na chuo kikuu cha Dar-es-Salaam kuchukua shahada ya Uchumi, BA(Economics) akahitimu mwaka 1987 na kuajiriwa na Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi yaani National Board of Accountancy and Auditors (NBAA) kama Muhasibu Msaidizi hadi mwaka 1995 ingawa alihudumu pia kama Muhasibu Mkuu wa Taasisi ya Uhasibu Arusha mwaka 1990.
Wakati akiwa Muhasibu Msaidizi wa Bodi ya Uhasibu na Ukaguzi (NBAA) alipata fursa ya kujiendeleza kielimu.
Mwaka 1993 alitunukiwa Certificate in Programming (UK) na akaongeza Diploma in System Analysis and Design (UK)
Mwaka 1994 alitunukiwa Stashahada ya juu katika masomo ya Kompyuta, yaani Advanced Diploma in Computer Studies (UK)
Mwaka 1995 alienda Chuo Kikuu cha Salford (UK) kusomea Shahada ya Uzamili MSc (Business Management and Information Technology)
Alirudi nchini Tanzania akafanya kazi kama Mshauri (Consultant) katika Kampuni ya Price Waterhouse Coopers hadi mwaka 2009 alipong'atuka rasmi na kuanzisha Kampuni binafsi ya masuala ya Ukaguzi ambapo alifanya kazi kama Auditor au Freelance Consultant hadi 2014 alipoombwa na Chadema kushiriki katika harakati za Ukombozi wa Taifa na kuchaguliwa kuwa Katibu wa Taifa wa Baraza la Wazee la Chama, nafasi anayoishikilia hadi sasa.
UZOEFU:
Akiwa Mshauri na Mkaguzi wa masuala ya Fedha na Uchumi, ndugu Lutembeka amesaidia mashirika ya umma na ya binafsi kuboresha utendaji wao wa kazi.
Ameshiriki katika ukaguzi wa Hesabu za Serikali kwenye Halmashauri mbalimbali za wilaya, mikoa, manispaa, wizara na taasisi mbalimbali za umma na hivyo kupata uzoefu wa kutosha kuhusu utendaji wa Serikali na Usimamizi wa Fedha za Umma.
Aidha, ndugu Lutembeka ni mwanzilishi wa Taasisi isiyo ya Kiserikali (N.G.O) ya Maendeleo Buganguzi yenye jina Buganguzi Development Association (BUGADEA). Ni taasisi inayojishughulisha na Uhamasishaji wa matumizi ya raslimali zilizopo kwa Maendeleo ya Wilaya ya Muleba.
Kwa sasa BUGADEA inafadhili ujenzi wa Kituo cha Afya kata Buganguzi, mradi unaokadiriwa kutumia kiasi cha shilingi milioni mia NNE (400,000,000/=)
Huyu ndiye Roderick Lutembeka, mrithi wa Prof. Anna Tibaijuka.
Muungeni mkono kwa Maendeleo na ustawi wa Jimbo la Muleba Kusini.
Wana wa Muleba Kwetu na wafuatao mnakaribishwa KUTOA MAONI yenu
Next Post Previous Post
Bukobawadau