Bukobawadau

Mbunge wa Geita ataka bangi, mirungi vihalalishwe

Mbunge wa jimbo la Geita Vijijini Joseph Msukuma Kasheku (CCM) ameiomba serikali kufanya utafiti wa kina kati ya madawa ya kulevya ya mirungi,bhangi na pombe za makaratasi maarufu kama viroba nini kina madhara zaidi kwa vijana.
Mbunge huyo ameyasema hayo katika kikao cha 5 cha bunge la 11 linaoendelea na vikao vyake katika ukumbi wa bunge mjini Dodoma.

''Mheshimiwa mwenyekiti zao la mirungi na bhangi kuna nchi zinaruhusu mfano majirani zetu wa Kenya ndege mbili kubwa hutua nchini humo kuchukua mirungi na kupeleka ulaya sasa kwa nini sisi tusiendeleze zao hili linalopatikana Geita na maeneoya Bunda mkoani Mara na maeneo mengine nchini ili wananchi wanufaike kwa kuuza zao hilo lakini nchi ipate fedha za kigeni pia''

Msukuma ameongeza kuwa ''kwa wasukuma kule kwetu mtu akitumia bhangi analima sana hata hekari mbili lakini inakatazwa na wakati huo huo vijana hawa wanadhoofika kwa viroba hivyo tufanye utafiti ili kama viroba ndivyo vyenye athari zaidi vipigwe marufuku.
 Wakati huo huo Naibu Waziri Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Ustawi wa Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto katika Dkt Khamis Kigwangalla amesema madawa ya kulevya ya bhangi na mirungi yana athari kubwa sana za kiafya na hasa afya ya ubongo na serikali kwa namna yoyote haitakubali kuruhusu au kujadili kwa namna yoyote kuhalalishwa kwa madawa hayo.

Next Post Previous Post
Bukobawadau