Bukobawadau

WATAALAMU WA MAJENGO WA DIT KUFANYA UTAFITI UHARIBIFU WA MAJENGO KAGERA.


Mkurugenzi Idara ya Kuratibu Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Brigedia Jenerali Mbazi Msuya akiongea na Wataalamu wa majengo kutoka Chuo cha Teknolojia Dar es Salaam (DIT), (hawapo pichani) ambao wapo mkoani Kagera kufanya utafiti wa uharibifu wa majengo uliosababishwa na tetemeko la ardhi ili kujua hali halisiilivyo hadi sasa.
 Mkurugenzi Idara ya Kuratibu Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Brigedia Jenerali Mbazi Msuya akiongea na Wataalamu wa majengo kutoka Chuo cha Teknolojia Dar es Salaam (DIT) wakiongozwa na Mhandisi Dkt. Johnson Malisa (wa kwanza kulia) ambao wapo mkoani Kagera kufanya utafiti wa uharibifu wa majengo uliosababishwa na tetemeko la ardhi ili kujua hali halisiilivyo hadi sasa. Wa kwanza kushoto ni Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Kagera Nesphory Bwana akifuatiwa na Dkt. Asinta Manyele na Mhandisi Dkt. Johnson Malisa wa DIT.
.

(Picha na Eleuteri Mangi, MAELEZO, Bukoba)


WATAALAMU WA MAJENGO WA DIT KUFANYA UTAFITI UHARIBIFU WA MAJENGO KAGERA.
Na Eleuteri Mangi, MAELEZO, Bukoba
Timu ya wataalamu wa majengo kutoka Chuo cha Teknolojia Dar es Salaam (DIT) wamewasili mkoani Kagera kufanya utafiti wa uharibifu wa majengo uliosababishwa na tetemeko la ardhi ili kujua hali halisiilivyo hadi sasa.
Timu hiyo iliyyongozwa na Dkt. Asinta Manyele na Mhandisi Dkt. Johnson Malisa wa DIT wapo mkoani humo ili kuwajionea hali halisi ya majengo katika wailaya zilizoathiriwa na tetemeko la ardhi lililotokea Septemba 10 mwaka huu na hali ilivyo hadi sasa baada ya tukio hilo.
Wakiwa katika kituo cha kukabiliana na maafa mjini Bukoba, wataalamu hao wamemwabia Mkurugenzi Idara ya Kuratibu Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Brigedia Jenerali Mbazi Msuya kuwa utafiti wao unalenga kufanya tathmini ya kujua namna nyumba zinavyopaswa kujengwa ili kukabiliana na atahri za tetemeko la ardhi ambalo kwa Tanzania ni tukio la kwanza ambalo limekuwa na madhara mengi yakiwemo majengo ya taasisi za umma na za watu binafsi, nyumba za watu binafsi, miundombinu ya maji, umeme pamoja na barabara.
Zaidi ya hayo, watafiti hao wamemwambia Brigedia Jenerali Msuya kuwa nia yao pia ni kuchunguza aina za udongo katika mkoa wa Kagera na kutoa ushauri wa aina za majengo yanayotakiwa kujengwa kwa kuzingatia tahadhari za athari za tetemeko la ardhi. 
Aidha, watafiti hao wametoa ushauri kwa waandaaji wa sera, waandae sera inayohusu maelekezo ya ujenzi wa majengo ambayo yolenga kuhimili athari za tetemeko la ardhi ili yaweze kustahimili nguvu ya tetemeko la ardhi endapo litatokea.
Kwa upande wake Mkurugenzi Idara ya Kuratibu Maafa Ofisi ya Waziri Mkuu Brigedia Jenerali Mbazi Msuya amewataka wataalamu hao watumie elimu waliyonayo kuelimisha jamii katika kujua aina ya majengo wanapojenga nyumba zao ili ziwe imara.
Katika kurejesha hali baada ya tetemeko hilo, Brigedia Jenerali Msuya amesema kuwa kituo chake kinashirikiana na Kamati ya Maafa ya Mkoa kwa kuwa na mikutano kila siku pamoja na kuratibu mambo mbalimbali ikiwemo kupokea na kugawa misaada inayotolewa na wananchi, taasisi za kidini na za watu binafsi na mataifa mengine yakiwemo Kenya, Burundi, Uganda, India na Uingereza.
Halmashauri za mkoa wa Kagera ambazo zimeathiriwa na zaidi na tetemeko la ardhi ni Bukoba Vijijini, Manispaa ya Bukoba, Muleba, Kyerwa, Misenyi na Karagwe.

Next Post Previous Post
Bukobawadau