Bukobawadau

JK AZINDUA RASMI TAASISI YA MAENDELEO YA JAKAYA MRISHO KIKWETE (JMKF)

 Rais mstaafu wa Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete (kulia), akizungumza alipokuwa akizindua rasmi Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete Foundation (JMKF) ikiwa ni sehemu pia ya uzinduzi wa taasisi hiyo kwenye Hotel ya Hyatt Kempinsk The Kilimanjaro Dar es Salaam leo. Kikwete ni Mwenyekiti wa Taasisi hiyo.PICHA ZOTE NA RICHARD MWAIKENDA;KAMANDA WA MATUKIO BLOG
 Mwenyekiti wa Taasisi hiyo, Jakaya Kikwete, alisema kuwa Taasisi hiyo pamoja na mambo mengine  itajihusisha na masuala ya Maendeleo ya Binadamu nchini, Afrika na Duniani.


Na. Immaculate Makilika- MAELEZO

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne Mhe. Dkt. Jakaya Kikwete amesema kuwa anapenda kuendelea kufanya shughuli zinazosaidia kuleta maendeleo kwa watu na jamii.

Akizungumza na waandishi wa habari  leo Jijini Dar es salaam, wakati alipokuwa  akizindua Taasisi yake ya Jakaya Kikwete (Jakaya Mrisho Kikwete Foundation)  alisema kuwa kwa muda mrefu amekua akipenda na kujihusisha na shughuli mbalimbali za maendeleo ya watu na hivyo Taasisi yake itamsaidia katika kufikia malengo yake.

“Nimetumia muda wangu kwa ajili ya maendeleo ya watu, baada ya shule, nilikitumikia Chama cha Mapinduzi(CCM), nilitumikia Jeshi na baadae Serikali, kwangu Taasisi hii imekuwa chombo kitakachonisaidia kuendeleza maono yangu na kutimiza ndoto zangu katika kuendelea kusaidia watu” alisema Dkt. Kikwete.

Akiizungumzia taasisi hiyo Kikwete alisema kuwa, Taasisi yake ina wajumbe 9 kutoka sehemu mbalimbali duniani wenye nyadhifa na heshima kubwa katika nchi zao.

Ameongeza kuwa Taasisi hiyo imejikita kusaidia jamii katika maeneo makubwa manne, maendeleo ya jamii  hasa katika kujikita kuondoa umaskini, mabadiliko ya hali ya nchi na kilimo  kwa wakulima wadogo.

Pia Taasisi hiyo imejikita katika huduma za afya, kutokomeza malaria na afya ya mama na mtoto.

Maeneo mengine ambayo Taasisi hiyo inajihusisha nayo ni  ni elimu kwa  vijana ili  kukuza vipaji vyao na kuwapa mafunzo kuhusu uongozi bora, usawa wa kijinsia na namna ambavyo Serikali inavyotoa huduma kwa wananchi.

Aidha, alisisitiza kuwa Taasisi yake itaisaidia Serikali, mashirika na Taasisi mbalimbali ili kushirikiana kuwaletea maendeleo watanzania na watu mbalimbali duniani.

Dkt. Kikwete amewataja Wajumbe wa Bodi ya Udhamini ya Taasisi yake kuwa ni Balozi Ombeni Sefue aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi, Profesa Rwekaza Mukandala Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Willium Mahalu Mhadhiri Mwandamizi  katika Chuo Kikuu cha Tabibu cha Bugando.

Wengine ni Balozi Mwanaidi Maajar aliyewahi kuwa Balozi wa Tanzania nchini Uingereza, Abubakar Bakhresa, Mkurugenzi Mtendaji wa Kundi la Makampuni ya Bakhresa, Genevieve Sangudi  Mtaalamu wa Masuala ya kibishara ya Kimataifa kutoka Marekani.

 Pia wapo Dato’ Sri  Idris Jala, Waziri asiyekuwa na Wizara Maalumu nchini Malyasia,  Balozi Charles R. Stith aliyekuwa Balozi wa zamani wa Marekani nchini Tanzania pamoja na Dkt. Carlos Lopes ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Taaisi ya Mafunzo na Utafiti ya Umoja wa Mataifa (UNITAR).

Taasisi ya Maendeleo ya Jakaya Kikwete ilisajiliwa tarehe 17, Februari 2017, na hii ni mara ya kwanza kwa wajumbe wa bodi ya wadhamini kukutana tangu kuanzishwa kwake.
 Kikwete akizungumza na baadhi ya wajumbe wa Bodi ya Wadhamini wa Taasisi yake ya JMKF
 Jakaya Kikwete akikumbatiana na Mjumbe wa Bodi ya Wadhamini wa Taasisi hiyo, Balozi wa zamani wa Marekani nchini Tanzania, Charles Stith
 Mwenyekiti wa Taasisi ya JMKF, Jakaya Kikwete akisalimiana na mjumbe wa Bodi hiyo, Mfanyabiashara maarufu Mtanzania aishie Marekani, Genevieve Sangudi
 Mwenyekiti wa Taasisi ya JMKF, Jakaya Kikwete akisalimiana na mjumbe wa Bodi hiyo ya Wadhamini , Dato' Sri Idris Jala, Waziri asiye na Wizara Maalumu Ofisi ya Waziri Mkuu wa Malaysia na Mtendaji Mkuu wa Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (Pamendu) nchini humo.
 Mwenyekiti wa JMKF, Jakaya Kikwete akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Baraza la Taasisi hiyo.
 Jakaya akijadiliana jambo na Balozi Charles Stith
 Kikwete akizungumza wakati wa uzinduzi wa Taasisi hiyo.
 Jakaya Kikwete akifafanua mambo mbalimbali kuhusu Taasisi hiyo

 Dato' Sri Idris Jala kutoka Malaysia
 Genevieve Sangudi kutoka Marekani
 Mwanasheria Maarufu nchini, Balozi Mwanaidi  Sinare Maajar. Alikuwa Balozi wa Tanzania nchini Uingereza 2006 na Marekani 2013



 Daktari Bingwa wa Upasuasi, Profesa Wiliam Mahalu
 Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa  Rwekaza Mukandara
 Mkurugenzi Mtendaji wa Kundi la Makampuni la SS Bakhresa, Abubakar Bakhresa
 Balozi wa zamani wa Marekani nchini, Charles Stith
Next Post Previous Post
Bukobawadau