Bukobawadau

MAHAKAMA YAMGANDA YUSUF MANJI

-NA KULWA MZEE -DAR ES SALAAM
MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imekataa kutoa amri ya kumwachia huru kwa muda mfanyabiashara, Yusuf Manji badala yake imeamuru kusikiliza maombi yake ya kupinga kuwekwa kizuizini.
Uamuzi huo umetolewa leo baada ya kupokea maombi yaliyowasilishwa na Wakili wa Manji, Hudson Ndusyepo kwamba walishangazwa na kitendo cha kumweka chini ya ulinzi Manji akiwa Hospitali ya Agha Khan ambapo anashikiliwa isivyo halali hivyo wanaiomba mahakama kumwachia huru.
Maombi hayo yalitakiwa kusikilizwa leo lakini upande wa Idara ya Uhamiaji ukiwakilishwa na Wakili wa Serikali Mkuu, Osward Tibabyekomya uliomba kuwasilisha majibu ya hati kinzani. Jaji Ama –Isario Munisi alikubali kuwapa muda hadi Jumatatu wiki ijayo wawe wamewasilisha majibu hayo na kesi itaanza kusikilizwa saa nane mchana siku hiyo lakini pia alikataa kutoa amri hiyo na kuamuru maombi ya kupinga kuendelea kuwepo kizuizini kusikilizwa siku hiyo hiyo.
Katika hatua nyingine kesi ya kutumia dawa za kulevya aina ya heroin inayomkabili Manji katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi, Cyprian Mkeha imeahirishwa hadi Aprili 18, mwaka huu.
Katika hati ya mashtaka inadaiwa mshtakiwa alitenda kosa hilo kati ya Februari 6 na 9, mwaka huu, maeneo ya Upanga Sea View wilayani Ilala katika Mkoa wa Dar es Salaam, ambako alitumia dawa za kulevya aina ya heroin.
CHANZO.Gazeti la Mtanzania.17/3/2017
Next Post Previous Post
Bukobawadau