MUNGIKI WA LIPUMBA WAVAMIA “PRESS” YA CUF, WAPIGA WAANDISHI WA
HABARI NA VIONGOZI, MUNGIKI MMOJA AJERUHIWA NA WANANCHI WENYE HASIRA
KALI!
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI.
(Imetolewa na Julius Mtatiro, Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi, The Civic United Front - CUF) 22 April 2017.
Ndugu zangu, Leo, Jumamosi, 22 Aprili 2017, Mwenyekiti wa CUF Wilaya ya
Kinondoni, Mhe. Juma Mkumbi (ambaye pia ni Mjumbe wa Baraza Kuu la
Uongozi la Taifa) alikuwa anazungumza na vyombo vya habari katika Hotel
ya VINA iliyoko Kata ya Mabibo, wilaya ya Kinondoni (jijini Dar Es
Salaam), juu ya masuala mbalimbali yanayohusu wilaya yake.
Akiwa
anaelekea kumaliza mazungumzo na wanahabari, ghafla, watu waliovalia
KININJA/VINYAGO walipaki magari mawili karibu na hoteli na kuvamia
ukumbi wa PRESS ya Mhe. Juma Mkumbi.
Wavamizi hao maarufu kama
MUNGIKI, (ambao hutumwa na Prof. Lipumba) leo wakiwa na BASTOLA MOJA na
MAPANGA walianza kuwapiga viongozi wa CUF akiwemo Juma Mkumbi na
kuwasababishia majeraha kadhaa.
Watu waliopigwa zaidi kwenye
kadhia hiyo ni waandishi wa Habari, wengi wao wameporwa simu zao na
vitendea kazi mbalimbali. Hata hivyo, juhudi za wasamaria wema na
wananchi wa eneo hilo zilifanyika na wananchi wakapandisha ghorofani
baada ya kusikia kelele za kuomba msaada, MUNGIKI wa Lipumba wakazidiwa
nguvu na kukimbilia kwenye magari yao, wakatokomea kusikojulikana.
Katika kadhia hiyo, baadhi ya MUNGIKI hao walichelewa kuwahi magari
waliyokuja nayo na inasemekana walianza kukimbilia vichochoroni ambako
wananchi walishakusanyika, mifukuzano ikaanza. Tunaambiwa kuwa baadhi ya
MUNGIKI hao, ( akiwemo huyu pichani) wamejeruhiwa vibaya na wananchi.
The Civic United Front (CUF) tumepokea kwa masikitiko makubwa taarifa
hizo za kusikitisha, kughadhibisha na kutia aibu katika nchi yetu. Iweje
leo katika nchi hii watu wavamiwe na makundi ya wahuni na kupigwa na
kuumizwa? Iweje leo waandishi wa habari wazuiwe kuchukua habari za mambo
muhimu ilimradi tu kuna genge la wahuni limeachwa lifanye litakavyo?
Iweje leo, vyombo vya dola viendelee kulikumbatia kundi hili la Lipumba
ambalo linaajita “MUNGIKI” huku likiachwa tu lijiite hivyo na kutenda
hivyo.
Tukio hili la leo la Mabibo linanifanya niwakumbushe
matukio mengine kadhaa ambayo MUNGIKI wa Lipumba wameyasimamia tena
wakisaidia na POLISI ama wakati wa matukio hayo, au wakati wako chini ya
vyombo vya Ulinzi na Usalama. Nitawakumbusha baadhi ya matukio hayo:
1. TUKIO LA KWANZA
Tukio la kutekwa kwa mhe. Joran Bashange (Kaimu Naibu Katibu Mkuu -
Bara na Mkurugenzi wa Fedha wa chama). Watekaji walifanya tukio hilo
majira ya saa 1.30 asubuhi tarehe 16/08/2016 mtaa wa Madenge, Buguruni
wakiwa na PINGU na gari aina ya Noah yenye namba za Usajili T 670 CEX.
Walimbeba Mhe. Bashange mzobemzobe na kumuingiza kwenye gari.
Bashange aliokolewa na wananchi waliolizunguka gari hilo na kuliwekea
magogo, kisha wakawataka watekaji wajisalimishe na Polisi wakaitwa
wakawakamata kwenye eneo la tukio wakawakuta na PINGU za Polisi, mikanda
ya kijeshi n.k. Watekaji hao wanafahamika kwa majina ya Samweli
Richard, Ramadhan Said na Shaibu Issa (Maarufu Mrangi) na walipohojiwa
wakakiri kuwa wametumwa na Prof. Lipumba.
Bashange alipewa PF3
kwani aliumizwa kwenye zile purukushani, akapata matibabu kisha jalada
ya upelelezi la kesi ya jinai la RB Namba BUG/IR/5937/2016
likafunguliwa. Baada ya siku chache watuhumiwa wote wakaachiwa, chama
chetu kikaripoti suala hilo kwenye ofisi ya ZCO Dar Es Salaam,
akamuamuru OCD wa Buguruni awafikishe watuhumiwa hao kwa ZCO. Watuhumiwa
hao walipelekwa kwa ZCO na tokeo hapo hakuna kilichoendelea,
walishaachiwa huru na hawakuwahi kufunguliwa mashtaka yoyote.
__________________________
2. TUKIO LA PILI
Tukio la Lipumba na kundi la MUNGIKI likisaidiwa, likilindwa na
kuongozwa na POLISI lilipovamia, kupiga wajumbe wa Mkutano Mkuu wa CUF
mwezi Agosti 2016, kusababisha uharibifu mkubwa Blue Pearl Hotel,
kusababisha Mkutano Mkuu wa CUF uhairishwe kwa sababu za kiusalama kabla
ya kukamilisha ajenda ya pili ya mkutano ambayo ilikuwa imeanza, ya
uchaguzi wa nafasi ya Mwenyekiti wa CUF Taifa. Uhuni huo wa Mungiki na
Lipumba ulikisababishia chama kulipa Shs Milioni 8.5 kwa Hotel ya Blue
Pearl ili kufidia hasara ya uharibifu wa samani mbalimbali, lakini pia
likakisababishia chama hasara ya Shs Milioni 800 ambazo ziliandaa
Mkutano Mkuu huo maalum.
Tukio hili la uvamizi na upigwaji na
uumizwaji wa Wajumbe wa Mkutano Mkuu liliripotiwa Kituo cha Polisi
Magombeni na kupewa RB Namba MG/RB/9072/2016 ya 22/8/2016, maelezo ya
walipigwa na kujeruhiwa yalichukuliwa, wakapewa PF3 wakapata matibabu,
Jeshi la Polisi likapewa CD za tukio zima likionesha picha za video za
MUNGIKI waliovamia na kujeruhi watu pamoja na majina yao, lakini hadi
leo hajakamatwa wala kufunguliwa mashtaka yeyote kati yao.
__________________________
3. TUKIO LA TATU
Tukio la Lipumba na MUNGIKI kuvamia Ofisi Kuu ya CUF Buguruni tarehe
24/09/2017. Katika uvamizi huo, walinzi wa ofisi na walinzi maalum wa
kampuni ya Ionsides Security Company walipigwa na kunyang’anywa Bunduki
moja (ambayo baadaye MUNGIKI waliikabidhi kwa jeshi la Polisi). Jambo la
kusikitisha ni kuwa, MUNGIKI na LIPUMBA walikuwa wanaongozwa na
kusaidiwa na maafisa wa Jeshi la polisi na Askari Kanzu ambapo Polisi
walikuwa na gari mbili wakiwa na silaha za moto, LIVE bila chenga!
Uvamizi huo ulihusisha kupiga na kuumiza vibaya walinzi wa zamu, na
walinzi maalum wa Ironsides Security, kubomoa milango na mageti ya Ofisi
kuu na kuharibu mali za chama (kwa kusindikizwa na kusaidiwa na
Polisi). Chama kiliripoti suala hili Kituo Kikuu cha Buguruni (kwa ajili
ya kutimiza matakwa ya kisheria – kesi ya nyani kwa ngedere) na
likafunguliwa jalada la uchunguzi kupitia RB Namba BUG/RB/8741/2016 ya
tarehe 24/9/2016. Hadi leo hii hakuna uchunguzi uliofanywa wala hatua
zilizochukuliwa.
__________________________
4. TUKIO LA NNE
Tukio la kutekwa mwanachama wa CUF Mohamed Said, ambalo lilitokea
tarehe 10/11/2016 katika eneo la Mahakama Kuu ya Tanzania mbele ya
Polisi, baada ya kundi la MUNGIKI kuendesha vurugu kubwa huku Polisi
wakishuhudia. Hii ilikuwa mojawapo ya siku ambazo kesi ya Bodi ya
Wadhamini ya CUF dhidi ya Lipumba, Msajili wa Vyama na wenzao, ilikuwa
inatajwa.
Baada ya Mohd Said kutekwa, alipelekwa hadi Ofisi Kuu
ya CUF Buguruni akaingizwa ofisini kwa Lipumba akahojiwa na Lipumba
kisha baadaye wakamuacha. Vipigo alivyopewa kwenye utekaji huo
vilipelekea apate majeraha makubwa usoni na mdomoni.
Bwana
Mohamed Said aliripoti Kituo cha Kati (Central Police) akapewa PF3 na
kwenda kupata matibabu ikiwemo kushonwa nyuzi kadhaa na jalada la
uchunguzi wa kijinai likafunguliwa kupitia RB Namba CD/CID/PE/88/2016.
Watekaji wale wanajulikana, polisi walipewa picha zao halisi za video
na mnato, tangu wakati wanamkamata Bwana Mohd Said hadi wanamuingiza
kwenye magari na kuondoka naye, bila ridhaa yake, tena mbele ya Polisi
waliokuwa wamtanda mahakamani ili kulinda hali ya usalama. Lakini hadi
leo hii, hakuna MUNGIKI aliyekamatwa wala kuhojiwa.
__________________________
5. TUKIO LA TANO
Tukio la kutekwa mhe. Joran Bashange (kwa mara ya pili) lililotokea
tarehe 14/12/2016 kata ya Buguruni mkabala ya Shule ya Msingi Hekima.
Kundi la MUNGIKI wa Lipumba zaidi ya 30 likajitokeza na kuanza
kumshambulia likimlazimisha aingie kwenye gari ambayo haikujulikana
(kwani ikimbia na baadhi ya watekaji waliotoroka).
Bashange
akapiga kelele na mayowe ndipo wananchi waliokuwa karibu wakawadhibiti
watekaji, wengine wakakimbia. Watekaji kadhaa waliowekwa chini ya ulinzi
na wananchi wakakamatwa na POLISI baada ya wananchi kuomba msaada kwa
njia ya simu. Walipohojiwa POLISI Kituo cha Buguruni wakadai wametumwa
na Prof. Lipumba.
Baadhi ya waliokamatwa kwenye eneo la tukio na
kufikishwa Kituoni wanajulikana kwa majina ya Twaha Ngozoma, Miraji
Mtwibiliko. Jalada la upelelezi lenye RB Namba BUG/PE/116/2016
lilifunguliwa katika Kituo cha Polisi Buguruni siku hiyo hiyo.
Watuhumiwa hao (MUNGIKI) wakiwa bado rumande alifika Prof. Lipumba na
kufanya mazungumzo na OCD kisha mmoja akaachiwa na mwingine akaachiwa
kesho yake. Hadi leo tuongeavyo, hakuna mtuhumiwa aliyefikishwa
mahakamani kutokana na tukio hilo la jinai.
__________________________
6. TUKIO LA SITA
Tukio la kuchomwa kisu mwanachama aitwaye Robert Samsoni eneo la
shingo, lililotokea tarehe 14/12/2016 eneo la Mahakama Kuu ya Tanzania,
mbele ya Polisi! Tukio hili lilifanywa na MUNGIKI wa Lipumba mbele ya
kamera za waandishi wa habari wakiwepo na waliripoti hadi kwa picha za
VIDEO, wachomaji na mchomwaji wako dhahiri kwenye video hizo.
Tukio hili lilianza baada ya MUNGIKI na Lipumba kuanza kupiga wanachama
wa CUF waliohudhuria mahakamani katika kesi ya Bodhi ya Wadhamini wa CUF
dhidi ya Lipumba na wenzake, ambapo mkakati wao ni kuhakikisha kwamba
wananchama wanaogopeshwa ili wao tu (Mungiki) na Lipumba ndiyo
wahudhurie mahakamani.
Tukio likaripotiwa Kituo cha Polisi Kati
(Central Police) na PF3 ikatolewa, majeruhi akashonwa nyuzi takribani 12
(jeraha kubwa sana), majina ya MUNGIKI waliompiga na kumchoma kisu
yakawasilishwa polisi, picha zao, makazi yao n.k.
Polisi
wakafungua majalada ya uchunguzi namba CD/RB/12671/2016 na
CD/IR/4567/2016 yote ya tarehe 14/12/2016. Hadi hivi leo tuzungumzavyo,
hakuna mtuhumiwa aliyekamatwa wala kuhojiwa, sembuse kufikishwa
mahakamani.
______________________________
Matukio yote
haya ni ushahidi tosha kwamba, Vyombo vya Dola ndivyo vinalilea, kulipa
mbinu na kuliendekeza hili kundi la Lipumba, na kwamba vinashirikiana
nalo kuleta vurugu, kuumiza watu na kutisha wananchi kwa kutumia mgongo
wa kile kinachoitwa "Mgogoro wa Uongozi ndani ya CUF."
Mathalini,
Katibu wa CUF wa wilaya ya Kinondoni, hivi karibuni yeye na mtu
mwingine aitwaye Ali Makwiro, waliongea na vyombo vya habari wilayani
Kinondoni na kusisitiza kuwa wao wawili wanamuunga mkono Lipumba na
harakati zake za sasa. Chama chetu na uongozi wake (Mimi na Kamati ya
Uongozi ya chama, Katibu Mkuu Maalim Seif, Baraza Kuu, Kamati ya
utendaji ya Taifa, Bodi ya Wadhamini), hata siku moja hatukuwahi kukaa
na kufikiria achilia mbali hata kupanga HUJUMA zozote juu ya wanachama
wachache wanaomuunga mkono Lipumba, au viongozi wachache wanaomuunga
mkono, bali hata kuombea jambo hilo litokee.
Pamoja na Usaliti
alioufanya Lipumba kwa chama, pamoja na kuungwa mkono na dola ili
akivuruge chama, pamoja na upuuzi na ujinga wote aliousimamia tangu
alipotangaza kuwa anarejea kuwa Mwenyekiti kwa lazima, sisi viongozi wa
chama tunaotambulika na vikao vyote halali vya chama, hatukuwa kufikiria
ku OPT njia ya mapambano na umwagani damu kama namna ya kumshinda
Lipumba na genge lake.
Mara zote tumekuwa tunawasisitiza
wanachama wetu kuwa watulivu na wasijihusishe na vitendo vya matumizi ya
nguvu na vurugu. Hata wabunge wetu na wanachama wa Dar Es Salaam
walipopanga tarehe ya kwenda kuipokonya Ofisi Kuu ya Buguruni kutoka kwa
Lipumba, nilijitokeza hadharani na kuzuia zoezi hilo na mnakumbuka
nilisisitiza kuwa siko tayari kuona damu ya hata mwanachama mmoja wa CUF
inamwagika ati kwa sababu sisi ni wengi na tunataka kutumia wingi wetu
kumtoa Lipumba na kigenge chake pale Buguruni.
As long as, Makao
Makuu ya chama (Headquarter) yanayotambulika kikatiba yako Zanzibar,
niliwaambia wanachama kuwa tumuachie Ofisi Kuu (Main Office) ili yeye
atambe kwa kusaidiwa na dola na nikasema mimi ntafanyia shughuli zangu
na Kamati ya Uongozi kutokea Makao Makuu na nikatoa mfano kwamba mbona
CCM wanaendesha chama chao kutokea Dodoma? Msimamo huu ndiyo pia msimamo
wa Katibu Mkuu wa CUF.
_______________________
Sisi ambao
tunatambuliwa na vikao vya chama tumeamua kutumia njia sahihi kutatua
mgogoro huu wa kutengenezwa, kwa nini upande huu unaoungwa mkono na
vyombo vya dola, na serikali na chama kinachoongoza dola, unatumia njia
za hatari namna hii katika kumpigania Lipumba waliyemtengeneza?
Kwa nini basi Mkutano wa Mwenyekiti wa Wilaya ya Kinondoni (anayeunga
mkono chama na kumpinga Lipumba) uvamiwe na kuhujumiwa na watu
waliotumwa na Lipumba huku nchi yetu ina vyombo vya dola? Mbona ule wa
Katibu wa Kinondoni (anayemuunga mkono Lipumba) sisi hatukutuma wahuni
wauvamie? Kwani sisi hatuwezi kufanya hivyo? Kwani kazi ya vyombo vya
dola ni kusimamia wavaa vinyago na wabeba silaha za moto na baridi ili
kuvamia shughuli halali za vyama au utoaji wa maoni?
Chama chetu
kinasikitishwa sana na vitendo hivi vya watu kuvamiwa na MUNGIKI
wanaoongozwa na Lipumba, kupigwa, kuchomwa visu, kutekwa n.k. ambapo
kwenye masuala yote hayo, vyombo vya dola vimeendelea kumlinda Lipumba
na genge lake dhidi ya chama na viongozi wake.
Kubwa kuliko yote,
tumesikitishwa mno na kitendo cha hatari sana cha leo ambapo waandishi
wa habari na viongozi wa chama wakiongoza na Mwenyekiti wa CUF wilaya ya
Kinondoni, wavamiwa na kupigwa na kundi hili la Lipumba lijiitalo
“MUNGIKI’ (kama ilivyotokea leo Mabibo). Je, tukio hili lina maana gani?
Lina maana kuwa waandishi wa habari wanatakiwa kuripoti habari za
Lipumba tu, na kuhudhuria mikutano yake - na kwamba wasithubutu
kusogelea mikutano ya viongozi halali wa chama (kama ilivyokuwa Mkutano
huu wa leo wa Mkt wa CUF Kinondoni). Je, watanzania wanaona hali hii ni
sawa tu? Je tukae kimya tu?
Je, dola, hata kama imewekeza nguvu
kubwa kabisa kwenye mpango wa kuisambaratisha CUF kwa kumtumia Lipumba,
na kwamba nguvu hiyo inawauma na lazima wamtumie wawezavyo hadi mwisho,
kwa nini basi zisitumike mbinu za hujuma za kawaida kuliko hizi za
kuteka viongozi, kuwapiga, kuwajeruhi, kuwavamia, kuwachoma visu na
kuzuia shughuli zao?
Kwani usalama wa Taifa, ambao wanampangia
Lipumba hujuma za namna hii hawana mbinu mbadala za kukimaliza chama cha
siasa kisichotakiwa bila kutumia nguvu hii na makundi yenye mapanga na
silaha za moto? Hivi unapotaka kukiua chama fulani cha siasa, ni lazima
utumie nguvu za kijinga namna hii, zinazoweza kupelekea umwagaji damu
bila sababu?
Natoa wito kwa IGP Mangu, Kamishna Sirro wa kanda
maalum na ZCO wa Dar Es Salaam, kwamba haya yanayoendelea hivi sasa hadi
viongozi wa juu wa CUF na waandishi wa habari kuanza kuvamiwa na
mapanga na silaha za moto, kupigwa na kujeruhiwa, kutekwa, kuchomwa visu
na kuumizwa, ni matunda ya JESHI LA POLISI ya kulilea kundi linalojiita
MUNGIKI, lililoasisiwa na Lipumba na ambalo huenda linapata msaada
mkubwa sana wa kiutendaji kutoka SERIKALINI!
Ndiyo maana mtu
anaweza kushangaa, iweje kundi hilo litende mambo yote hayo, mpaka haya
ya leo na hakuna MUNGIKI hata mmoja ambaye amewahi kufikishwa
mahakamani. Mtanzania wa kawaida anaweza kujiuliza, MUNGIKI hawa wa
Lipumba wanapata wapi Bastola za kutumia kuvamia mikutano halali kabisa?
Dola inadhani kuwa tumeshasahau kitendo cha Nape Nauye kutolewa bastola
na Ofisa wa Usalama wa Taifa?
Dola inadhani kuwa tumeshapoteza
kumbukumbu kuwa watekaji wa msanii ‘Roma Mkatoliki’ na wenzake
waliwatishia kwa Bastola kabla ya kuwatoa Tongwe Records. Hizi bastola
ambazo sasa viongozi wa CUF na waandishi wa habari wanatishiwa na kundi
la “Lipumba na Mungiki” tena hadharani mchana kweupe, wamepewa na nani?
Hawaogopi dola?
Siku kundi hili la MUNGIKI litakapoendesha MAUAJI
ntasikitika sana ntajapoona IGP na wenzake wakijitokeza kulaumu mauaji
hayo na kudai kuwa wanawasaka wauaji. Nimeshaeleza huko awali kuwa
wauaji huanza polepole, huanza kuvamia wakalindwana dola; hupiga na
kuumiza wengine wakalindwa na dola; huteka, kutisha, kuchoma watu visu
na wakalindwa na dola, huvamia mikutano halali na bastola na mapanga na
kuumiza watu na wakalindwa na dola, na mwisho huanza kuua.
Tusubiri kundi hili la Lipumba lianze uuaji ndipo tubane pua kuwa
tunalisaka! Na ifahamike kuwa chokochoko hizi ambazo zimefanywa na kundi
la MUNGIKI tangu Agosti mwaka 2016 hadi leo bila kuchukuliwa hatua, ni
uthibitisho mwingine dhahiri kuwa DOLA, POLISI n.k. wana HISA za kutosha
kwenye kila kinachoitwa "Mgogoro wa Ndani ya CUF".
Mwisho, kwa
niaba ya The Civic United Front (CUF) napenda kutoa pole zangu za dhati
kwa waandishi wote wa habari waliopigwa katika kadhia hiyo,
kunyang’anywa simu zao, vitendea kazi na fedha. Nawaomba waandishi wa
habari na majukwaa yao tushikamane pamoja kuvibana vyombo vya dola
vichukue hatua kali dhidi ya wahuni na MUNGIKI wote waliopanga njama na
kutekeleza tukio la leo.
Naviomba pia vyombo vya habari
vitathmini kama ipo haja ya kuendelea kutangaza habari za kundi hili la
IBRAHIM LIPUMBA ambaye ndiye kiongozi mkuu wa kundi hili la MUNGIKI.
Lakini Ofisi ya Katibu na sisi Kamati ya Uongozi tutatoa ushirikiano
wote ambao unahitajika kwa viongozi wa vyombo vya habari na majukwaa yao
katika kuhakikisha kwamba wahuni hawa wanaofugwa na Lipumba na dola,
wanafika mwisho wao.
Nampa pole Mwenyekiti wa CUF wilaya ya
Kinondoni, Mhe, Juma Mkumbi, yeye na viongozi na wanachama wa CUF
TAASISI walioko Kinondoni. Nameshawapigia simu na kuwataka waweke
kumbukumbu sahihi za matukio yote yaliyotokea leo ikiwa ni pamoja na
kusaidiana na Ofisi ya Katibu Mkuu kuyaripoti kwa IGP Mangu na wenzake
ili kuweka rekodi sahihi bila kujali kuwa jeshi la Polisi litachukua
hatua zozote au la!
(Pichani, ni mmoja wa MUNGIKI akiwa ameumizwa
na mamia ya wananchi wenye hasira kali ambao walijitokeza kuwaokoa
viongozi wa CUF na waandishi wa habari dhidi ya uvamizi. Nimejulishwa
kuwa pia, wananchi hao wamepasua na kuharibu magari mawili yaliyokuwa
yakitumiwa na MUNGIKI na kwamba MUNGIKI wengine walifanikiwa kutoroka,
akiwemo yule aliyekuwa na BASTOLA. Kijana huyu anayeonekana pichani
huonekana akimlinda LIPUMBA sehemu nyingi aendazo).
Julius Mtatiro,
Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi,
22/04/2017.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
0 comment:
Post a Comment